Maoni

MAONI: Ruto hakufaa kusema hataachilia mamlaka ila pia ni kweli upinzani hauna chochote

Na CECIL ODONGO June 16th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

KENYA imekuwa taifa ambalo linazingatia demokrasia tangu mfumo wa vyama vingi uanzishwe nchini.

Marais ambao wamekuwepo wamehakikisha kuwa kuna njia ya wazi ya upokezanaji wa mamlaka.

Wikendi, akiwa katika Kaunti ya Kakamega, Rais William Ruto alisema hawezi kutoa mamlaka kwa viongozi wa upinzani akisema mienendo yao ya uongozi haifai kwa taifa hili.

Viongozi wa upinzani ambao Rais Ruto alikuwa akiwarejelea ni aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua, Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka, aliyekuwa Waziri wa Usalama, Dkt Fred Matiang’i, Kiongozi wa PLP Martha Karua miongoni mwa wanasiasa wengine ambao wako upinzani.

Japo ninakubaliana na kauli ya Rais Ruto kuwa viongozi hao wa upinzani hawana sifa tosha za kuongoza nchi hasa kutokana na matamshi yao yaliyojikita katika kukosoa bila kupendekeza suluhu, wakimshinda hana budi kukubali.

Hata wakati ambapo alikuwa naibu wa rais, Bw Gachagua alikuwa akiyalinda tu maslahi ya Mlima Kenya kwa kuhakikisha kuwa teuzi za serikali zinaendea eneo lake hilo.

Bw Gachagua hata alikashifiwa kwa kudai serikali ni ya hisa ambapo walioichagua 2022 ndio walistahili kunufaika kwanza kabla ya waliopigia kura upinzani kupewa mgao wao.

Ni baada ya kutupwa nje ya serikali mwaka jana ndipo Bw Gachagua alianza kuikashifu serikali na kudai kuwa anawatetea raia.

Hata kuongezwa kwa ushuru na nyumba za gharama nafuu ni sera ambazo Bw Gachagua alishabikia alipokuwa serikalini.

Mbona wakati huo hakuzikosoa hadharani?

Vivyo hivyo, Bw Musyoka na Dkt Matiang’i hawana chochote kipya cha kuwapa Wakenya na hata wanaweza kuwa wabaya zaidi wakichukua mamlaka.

Bado Wakenya hawajasahau jinsi Bw Musyoka alivyowasaliti kwa kujiunga na Mwai Kibaki wakati ambapo upinzani ulikuwa ukisaka haki kuhusu matokeo ya uchaguzi mkuu wa mwaka wa 2007.

Bw Musyoka ni kiongozi asiyekuwa na msimamo na uungwaji wowote wa maana wa kisiasa nchini.

Dkt Matiang’i naye ajitakase na madai kuhusu mauaji yaliyotokea alipokuwa waziri wa Usalama wa Ndani. Watu walipotea na miili mingi ikapatikana imetupwa katika mto Yala.

Kwa ufupi, viongozi wa sasa wana zigo la dosari hata kuliko utawala huu wa Rais Ruto na hata ukitathmini matamshi yao, lengo lao ni kuchukua mamlaka wala hawamakinikii mabadiliko ya kiuchumi na maisha ya raia.

Hata wakiungana bado itakuwa vigumu sana kumbandua Rais Ruto madarakani kwa sababu hesabu zao za kura hazitoshi hasa kiongozi wa nchi akiungwa mkono na ngome za Kinara wa Upinzani Raila Odinga.

Ingawa hivyo, iwapo watajipanga na kushinda kura za 2022, basi Rais Ruto hatakuwa na budi ila kuwapa mamlaka.

Japo itakuwa historia hapa kwa rais kushindwa katika muhula wake wa kwanza, utawala wa sasa hautakuwa na jingine ila kujaribu bahati yake mwaka wa 2032.

Marehemu Daniel arap Moi alikubali kutoa mamlaka kwa Mwai Kibaki baada ya Uhuru Kenyatta kushindwa kura 2002.

Bw Kenyatta alifuata mkondo huo baada ya kumpa Rais Ruto mamlaka ilhali alikuwa akimuunga mkono Bw Odinga 2022.

Mkondo huu ndio unastahili kufuatwa ili Kenya isielekee kwenye njia ya mataifa ambayo yamesambaratishwa na mizozo ya uongozi.

Uzuri ni kwamba kila serikali inayochaguliwa inapokuwa mbaya, waliochagua ndio hukenua meno na kulilia mabaya yake.