MAONI: Sifuna anajaribu kiatu cha Raila kisiasa, je atafaulu?
MGAWANYIKO katika chama cha ODM umefika kileleni, katibu mkuu wa chama hicho Seneta Edwin Sifuna anazidi kutamba na kusherehekewa hasa miongoni mwa vijana wanaosisimuliwa na mbwembwe na makeke yake ya kisiasa.
Wanaojitambulisha naye kupitia kauli mbiu ‘Mimi ndio Sifuna’ wanashabikia mwito wake, kwani Linda Mwananchi inaonekana kuleta matumaini mapya, tofauti na mirengo mingine.
Seneta Sifuna amehakikisha amepata ushabiki mkubwa kwa muda mfupi sana.
Mbali na hayo, cheo chake kimekumbwa na utata. Tangu chama cha ODM kijiunge na chama cha UDA kuunda serikali ya muungano, Sifuna alikwenda njia tofauti na muungano huo.
Kwa sababu hiyo, kwa muda amekuwa akionekana kuwa katibu mkuu wa chama mwenye maoni tofauti na wanachama wenzake hasa uongozi wa ODM.
Upinzani huo umesababisha kuwepo kwa mkutano uliombandua mamlakani kama katibu mkuu na kumteua katibu mkuu Catherine Omanyo.
Iwapo kitendo hicho hakijaonekana kumpiga sifuna mfupa, huenda asidumu katika cheo hicho.
Katika maisha yake ya kisiasa, mwendo wake Sifuna una sura ya safari yake Raila Odinga ambaye kwa ujasiri alijiuzulu katika chama cha FORD Kenya na kupoteza kiti chake cha ubunge cha Langata mwaka wa 1994 wakati wengi hawakutarajia.
Raila alikigura chama cha baba yake Oginga Odinga na kujiundia chama chake cha NDP kilichompa ushindi katika mazingira magumu ya ushindani.
Naye Sifuna amekuwa mwanafunzi asiyelalia masikio. Guu lake moja liko nje ya chama cha ODM bali ni muda tu unaosubiriwa ili kipya kizaliwe kutokana na hamasa hii ya Linda mwananchi.
Nafuu aliyopata Sifuna kutoka kortini ni ya muda.
Kamati inayotatua migogoro ya chama mwishowe itaidhinisha kuondolewa kwake na pa kukimbilia patakuwa usiku wa giza asipojijengea pango lake la kujificha kisiasa.
Je, Sifuna atakamilisha safari yake ya kisiasa kwa kufaulu au jahazi lake litamezwa na dhoruba?
Sifuna atakuwa amefuata nyayo za mshauri na mlezi wake kisiasa Raila na kilichobaki ni kujiundia chama chake kitakachompeperusha kisiasa hadi apate ufuasi ulio imara sawasawa na Riala Odinga.
Kiongozi huyo amejitoa mhanga kukosa uongozi wa chama mradi aendeleze ajenda yake.
Iwapo atabanduliwa bila shaka siasa zitakuwa ngumu kwake hasa kuwania kiti cha useneta wa Nairobi kwani chama cha ODM kitakuwa na mwanasiasa akatakayeteuliwa kuwania cheo hicho.
Umaarufu wa Sifuna Nairobi unaoweza kumpa kura na kuwapiku wenzake utatatizwa na kuwepo kwa vyama vingine hasa chama cha DCP na Wiper ambavyo vitakuwa na watu wao.
Kinachosalia sasa, ni Sifuna kushirikiana na wenzake katika mrengo wa Linda Mwananchi na kuunda chama watakachotumia kama daraja la kuwavusha katika awamu nyingine ya siasa.
Jua lao la kisiasa tayari linazama kwa udhaifu mwingi ila wakiunda chama mapema kuwania viti katika uchaguzi wa 2027, huenda kisu cha ngariba kikawaepuka.
Sifuna ana njia ndefu ya kujijengea mustakabali wake kisiasa.
ODM imekuwa nyumbani kwake katika safari ya siasa. Iwapo ataondoka katika chama cha ODM na kufaulu kuafikia malengo yake, basi, juhudi na ujasiri wake utakuwa umezaa matunda.