Maoni

MAONI: Ufasaha wa Rais Suluhu kuhutubu unaficha maovu yanayoendelea Tanzania

June 9th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

UKIAMBIA Wajerumani kwamba kiongozi wao wa zamani, kachinja Adolf Hitler, aliwaua Wayahudi kwa mamilioni na kuanzisha Vita Vya Pili Vya Dunia wanaruka juu na kudai alikuwa mzaliwa wa Austria.

Ukiwaambia Watanzania kwamba Rais Samia Suluhu Hassan ameharibu sifa za taifa lao kwa utekaji, mauaji, ubakaji na ulawiti wa wanaharakati, watakwambia ni Mzanzibari!

Huko ndiko kunakoitwa kukimbia majukumu, yaani watu hawataki kuwajibikia maovu yao, hasa kwa kuwa ni fedheha kunasibishwa na mtu asiye na utu.

Hilo haliwezekani. Historia haisahau.

Maovu aliyotenda Hitler yangali yanawaathiri Wajerumani, miaka zaidi ya 90 baadaye. Wajerumani huhisi kana kwamba wana hatia kwa sababu wazee wao ama hawakufanya chochote kumkomesha nduli yule au walimuunga mkono.

Watanzania wanaomwita Rais Samia Mzanzibari wanapaswa kujua kuwa, mradi anaongoza, na anawania urais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, tena wengi wako radhi kumchagua, ni kiongozi wa nchi yao.

Wapo walioapa kufa naye kwa vyovyote vile, hata ikiwa atawaua watu, kisa na maana anawania urais kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na wamezoea sare za kijani za chama hicho, tena kikishinda chaguzi zote kwa uhuni wa kuajabiwa.

Hali ikiwa hiyo ya kufumbia macho mauaji ya watu wasio na hatia, na kutia nta masikioni ili wasisikie kelele za wahanga wa mateso wakipumua pumzi zao za mwisho, unasalitika kujiuliza: Tatizo ni Rais Samia, au Watanzania wenyewe?

Mengi yamesemwa kumkashifu Samia, kiasi cha Wakenya kumdhihaki kwamba anaringa na wadhifa wa marehemu kwa kuwa alirithi urais kutokana na kifo cha John Magufuli, ila msema kweli ni mpenzi wa Mungu, hivyo ni vyema tumhukumu kwa ukweli.

Mwanzo, japo inaaminika kuwa kiongozi wa nchi akiwa mwanamke mambo mengi huenda yanavyostahili, hakuna manufaa yoyote ambayo ameiletea Tanzania kutokana na jinsia yake.

Tulishuhudia uongozi bora wa mwanamke wakati ambapo Ellen Johnson-Sirleaf alichaguliwa rais Liberia, akaipatanisha nchi, mibabe wa kivita wakaacha uhasama, haki ikatamalaki, amani ikaandama, viongozi wakapokezana madaraka kisheria.

Rais Joyce Banda alichukua hatamu za uongozi wa Malawi wakati ambapo taifa hilo lilikuwa na msukosuko wa kisiasa, akaongoza kwa ustaarabu usionasibishwa na wanasiasa, akaachia madaraka aliposhindwa uchaguzi.

Marais Ellen na Joyce walikuwa na fursa za kufanya kampeni za kutetea nyadhifa zao, na walizitetea kweli, lakini hawakuwaua raia wala kuwafunga wapinzani wao. Waliheshimu katiba za nchi zao mpaka mwisho bila kuonyesha dalili za kujaa woga.

Rais Samia je? Ukimlinganisha na wenzake hao, tofauti zao ni kama mbingu na ardhi! Ufasaha wake wa kuhutubu unaoficha maovu yanayoendelea Tanzania unaudhi hadi ya kuudhi! Vijembe vyake havichekeshi tena.

Watu wanaulizana: Ni mwanamke wa aina gani huyu asiyeujua uchungu wa mwana? Iweje hajali watu wasio na hatia wanapotekwa nyara, kupotezwa wasionekane tena, kubakwa, kulawitiwa na kuuawa?

Ingawa inaaminika kuwa udikteta wake unatokana na hofu ya uwezekano wa kushindwa uchaguzi utakaofanyika Oktoba mwaka huu, ni sahihi kukariri kwamba Samia ana hulka ya mtu muovu.

Amefanya maovu mengi kuliko aliyofanya mtangulizi wake, Magufuli, ambaye aliishangaza dunia kwa kujipa hamnazo huku miili ya Watanzania wasio na hatia ikielea ndani ya Mto Rufiji na Bahari ya Hindi baada ya kutekwa na polisi wake.

Wanaofahamu siasa za Tanzania vizuri wanasema Samia anaonekana kuwa mwoga, hamwamini yeyote ndani na nje ya serikali, na ndiyo sababu anawashughulikia vibaya hata wanachama mashuhuri wa CCM.

Mbunge wa Kawe, Bw Josephat Gwajima, ambaye ni maarufu zaidi miongoni mwa miamba wa CCM wanaoaminika wangetaka kumpinga Samia ili wabebe mwenge wa chama hicho uchaguzini, juzi ametumiwa polisi wamhangaishe kwa kupinga utekaji.

Yeyote kati ya Bw Gwajima na kigogo wa upinzani aliye jela, Bw Tundu Lissu, anaweza kumshinda Samia kwa wepesi wa kupigiwa mfano katika uchaguzi huru na wa haki. Samia mwenyewe anajua hilo, ndiyo maana ana woga mkuu.

Zamani nilichukizwa na uzembe wa Watanzania, hasa wakipendelea kuisifu serikali badala ya kuihakiki ili wapate huduma bora, lakini naona wameanza kujizoazoa na kuikabili. Huo ndio mwelekeo unaostahili. Nduli hakupi chochote hadi umkabe koo!

[email protected]