Maoni

MAONI: Ukishirikiana na polisi kutenda uovu ujue ipo siku watakukujia

Na DOUGLAS MUTUA June 18th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

VIJANA ambao hivi majuzi wameungana na polisi jijini Nairobi kukabiliana na waandamanaji waliojitokeza kupinga kuuawa kwa mwanabloga Albert Ojwang’ wanapaswa kuwa waangalifu sana.

Wapo watu wanaodhani wana jukumu la kuitetea serikali dhidi ya lawama za raia wenzao, na hilo ni jambo zuri likisalia katika majibizano ya mitandao ya kijamii tu, lakini mambo yanakwenda tenge pale majibizano yanapogeuka makabiliano ya kivita.

Unawapigia nini watu walio na cha kuandamania, wewe ambaye umeridhika na mambo yanavyokwenda nchini? Mbona usishiriki shughuli za kujijenga kiuchumi na vinginevyo ikiwa mazingira yanayowafanya wengine kuandamana yanakufaa?

Raia wa kawaida unapopinga maandamano ya kulaani uovu katika jamii, una maana kwamba huamini uovu upo, au uko sawa na uovu huo ukiwatendekea wengine.

Nikidhani mtu anayeiamini serikali yake kabisa anapaswa kuiaminia na uwezo wa kujitetea, hasa katika hali ambapo matumizi ya nguvu yanahitajika, kwa kuwa ina ukiritimba wa zana za vita na korokoro za kuwafungia watu. Mbona unaisaidia?

Ukweli unaopaswa kutuingia akilini sote ni kwamba kuandamana si uhalifu, hasa ikiwa waandamanaji hawatishii maisha wala mali za watu, lakini raia wenzao kuwapiga, hata ikiwa waandamanaji wenyewe wanavunja sheria, ni kosa la jinai.

Kulinda usalama wa nchi ni jukumu la vikosi vya usalama pekee, kwa hivyo unapojitiatia shughulini kwa mawe, marungu na silaha nyinginezo za kishamba unashirikiana sako kwa bako na watu watakaokutia nguvuni na kukushtaki jazba zikitulia.

Nina tajiriba ya kutosha kumuasa yeyote anayetaka kunisikiliza kwamba ni jambo la kijinga kudhani unaweza kushirikiana na polisi kuvunja sheria wanazolipwa ili kuzilinda. Walifunzwa chuoni kukabiliana na magenge, hivyo wewe ni adui yao daima.

Mwisho wa siku, kelele na fujo za mtaani zikitulia, hao-hao polisi ndio wanaochukua jukumu la kuwasaka na kuwawajibisha watu ambao walionekana kwenye kamera za runinga au CCTV wakivunja sheria. Na haijalishi unavunja sheria ukiwa upande gani.

Usiwahi kamwe kuungana na polisi kutenda kitu chochote unachojua ni kinyume cha sheria. Ikiwa huniamini, jiulize kwa nini polisi wanaowaua raia kiholela hadharani wanakamatwa, kuvuliwa sare za kazi na kushtakiwa kama wahalifu wa kawaida tu.

Jeshi la polisi lenyewe limejaa mifano ya vikosi maalum vilivyoundwa kwa ajili ya kukabiliana na wahalifu kwa njia zisizokubalika kisheria, mathalan kuwaua Mungiki, hatimaye vikosi vyenyewe vikamalizwa kwa njia mbalimbali vikishamaliza kazi vilizoundiwa.

Unafaidi ukuruba wao kwa muda ambao wanataka kukutumia kutimiza wajibu fulani, lakini ghafla utageuziwa kibao alfajiri njema, ukamatwe, ufunguliwe mashtaka ya kila nui, ulioshirikiana nao wakupandishe kizimbani na kutoa ithibati ulivyo mhalifu sugu.

Unafika wakati wa kila mmoja wenu kunena na nafsi yake, aliyekula kiapo kulinda usalama wa nchi akakumbuka kiapo chake, aliyeshiriki uhalifu kwa sababu za kisiasa au iwe yawe tu akakosa kwa kutorokea.

Mazoea ya raia kujiunga na polisi ili kukabiliana na waandamanaji yalianza miaka michache iliyopita na sasa inaonekana yamekuwa desturi yetu.

Bila shaka polisi wakitaka watamaliza tabia hiyo, lakini hatujui watataka lini. Matokeo ya hali ya sasa ni kwamba uhalifu utaongezeka kwa kuwa Kenya haikosi watu wenye mafedha tele wanaoweza kuyalipa magenge hayo.

Nayo magenge yako radhi kumtumikia yeyote anayelipa, hivyo tunawalea mamluki wa mitaani wanaoweza kuua kwa ada ya Sh2,000 pekee. Maisha ya binadamu yamekosa thamani.

Huo ni utamaduni hatari. Vijana wetu wanapaswa kukataa kutumiwa katika vitendo vyovyote vya kihalifu kwa kuwa wanachangia kuivunja nchi yao.

Ikiwa serikali inadhani vijana wana nguvu za kuisaidia nchi, basi na wawasajili rasmi kwenye polisi, wawape mafunzo chuoni na wawalipe mishahara mizuri. Vinginevyo, tunatumiana tu.

[email protected]