Maoni

MAONI: Waafrika tutasaidianaje wakati wa dharura kutokana na vita?

Na DOUGLAS MUTUA April 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

JE, uhaba wa mafuta na bidhaa zake ukijiri leo kutokana na vita vinavyoendelea nchini Iran, hali iwe kwamba hakuna taifa lolote la Afrika Mashariki linalojitosheleza, tutakimbilia wapi?

Na, je, kwani visima vya mafuta nchini Kenya na Uganda ambavyo tukisifiwa kwa muda sasa, vinatoa mafuta ambayo hayawezi kutusaidia wakati huu ambapo kila mtu anaweza kutabiri kuwa mbele si kwema?

Miradi mikubwa ya kujenga mabomba ya kusafirisha mafuta kutoka Uganda hadi Bandari ya Dar es Salaam, na Sudan Kusini hadi Bandari ya Lamu au Mombasa, ilikwama, inaendelea, au vipi?

Hebu tafakari hili: kawaida mataifa haya huingiza mafuta kutoka nje kabla hayajasafishwa, yakasafishiwa huku na kuuzwa huku-huku.

Kwani hayo yetu yanayosafirishwa kwenda nje hayawezi kusafishiwa huku tukauziwa kwa bei nafuu?

Tunauza yetu; tunanunua ya watu? Vipi sasa? Huenda tunasafirisha mafuta nje, yanachakatwa kisha yanarejeshwa huku, halafu tunauziwa (mafuta yetu) bei ya kufa mtu?

Usishtuke ukipata ukweli ndio huo kwa maana kwa muda tukikuza mazao muhimu kama majani-chai na kahawa, yakisafirishwa nje kuchakatwa, bidhaa zilizo bora zikibaki huko, tukirejeshewa masazo, tena tukiuziwa bei ghali!

Wakenya wengi wanaoishi nje waligundua siri hii kitambo, wakawa wananunua hizo huko nje badala ya kuja nchini na kuondoka na zinazouzwa Kenya kwani viwango vya ubora viko chini.

Hiyo ni makala ya siku nyingine, ngoja tushughulikie mafuta kwa sasa.

Nauliza maswali mengi hayo kwa sababu serikali za eneo hili zinaendelea kukanusha habari kwamba kuna uhaba wa mafuta, na kutuhakikishia kuwa hakuna ugumu wa maisha utakaotokana na vita vya Waamerika, Waisraeli na Waajemi.

Unapoona serikali zikitoa taarifa kama hizo, unasalitika kujiuliza iwapo kwa hakika watawala wetu wanaelewa wanachokisema, wanatupotosha makusudi ili tusiishe matumaini, au wenyewe hawana uwezo wa kukadiria hatari inayokuja.

Uhaba wa bidhaa yoyote, au bei ikipanda mno kiasi cha watu kutoimudu kokote katika eneo la Afrika Mashariki, wanaoishi maeneo ya mipakani huvuka mipaka kwa miguu na kununua bidhaa husika kwa bei nafuu inakopatikana.

Kenya ilipoweka sheria kali za kudhibiti ulevi miaka kadha iliyopita, wapendao kinywaji chao wakahitaji ya ka kusubiri mpaka saa fulani ndio baa zifunguliwe, Wakenya wanaoishi karibu na Uganda wakivuka mpaka na kurejea wakiwa walevi kweli-kweli!

Si siri kwamba Wakenya wananunua mayai, nafaka, nguo, sigara na bidhaa nyinginezo nchini Uganda kila siku.

Maziwa yalipogeuka ghali mno nchini Kenya miaka kadha iliyopita, kampuni za uchakataji maziwa za Kenya ziliingia kaskazini mashariki mwa Tanzania na kuyanunua kwa fujo hadi marehemu Rais John Magufuli akasema tuwakome.

Saruji ilipokuwa ghali nchini Tanzania, Watanzania waliingia Kenya na kuinunua kwa bei nafuu kiasi kwamba serikali yao ilikuja juu na kutishia kuwachukulia hatua kali ili waache kuhujumu uchumi wao eti.

Suala hilo lilijadiliwa bungeni, huku wabunge wa maeneo ya mipakani wakisema hamna kosa kwa mwananchi kujitafutia bidhaa bora na ya bei nafuu kokote anakoipata.

Uhaba wa mafuta na bidhaa nyinginezo ukitukumba sote tutakimbilia wapi? Usafiri utakuwa ghali kwa kuwa magari hayawezi kutumia maji badala ya mafuta.

Ukisema upike kwa kuni na makaa, utaambiwa unaharibu mazingira. Tena, kuni na makaa zitumikeje mijini, hasa mitaa ya kifahari?

Afrika, kutokana na hali yake hafifu kidiplomasia, haiwezi kushinikiza Amerika, Israel na Iran ziache kupigana ili maisha yasituendee vibaya.

Wala hatuna ndege au silaha za kuwapa ili wapigane zaidi, ndio sababu hawatutafuti ili tuwaunge mkono. Utadhani hatima yetu imo mikononi mwao.

Uingereza na mataifa mengine ya Uropa yamekataa kujiunga na vita hivyo, yale ya kiarabu nayo yanasuasua hata baada ya kushambuliwa na Iran na kamwe hayawezi kuuza mafuta kote duniani kama mwanzo, hivyo sote tunasubiri mafahali wamalizane kisha tuendelee na maisha.

Muhimu zaidi, huu ni wakati wa Afrika kumuunga mkono mtoto wao, Aliko Dangote, ambaye hivi majuzi alianzisha kiwanda cha kuchakata mafuta, alipoyasafirisha Uropa yakakataliwa kwa kisingizio kwamba hayakutimiza kiwango cha ubora kitakiwacho.

Waafrika waliguna eti alionewa.

Hii ni fursa yetu kuanza kununuliana bidhaa sisi kwa sisi, pesa zetu zibaki huku barani. Dharura iliyoletwa na vita inaturuhusu kujitafutia suluhu za matatizo yetu bila kuwekewa vikwazo na mataifa tajiri.

Tusikwame na kusubiri kuambiwa tutakalofanya kama watoto wadogo.

Mwafrika wa kawaida, yaani ambaye hajazoea maisha ya kifahari, yuko katika nafasi bora ya kuvumilia ugumu ujao kwa kuwa tayari yeye na ugumu wanajuana.

Tajiri naye atalazimika kujirudi, atunze alichonacho, ikibidi atumie usafiri wa umma badala ya kuchoma mafuta akiwa peke yake ndani ya gari.

Kimsingi, ubadhirifu utatuumiza sote wakati huu, kwa hivyo tajiri aliye na akili razini anapaswa kuzitumia kwa manufaa yetu sote.

– Douglas Mutua ni mwanahabari Mkenya anayeishi Amerika ([email protected])