MAONI: Wakenya watahatarisha maisha kwa vyovyote kuhepa umaskini
MBONA sijashangaa baada ya kusikia kuwa kuna kijana Mkenya, Bw Festus Arasa Omwamba, 33, ambaye tayari amewasaidia Wakenya 1,000 kujiunga na jeshi la Urusi katika vita dhidi ya Ukraine? Hawaogopi kuuliwa vitani?
Katika pita-pita zangu mtandaoni, nimewahi kutazama wasifu wa kijana ninayemjua vyema, kutoka kwetu kijijini hasa, akijitangaza bila kificho kuwa anawasajili watu kujiunga na kundi linalodaiwa kuabudu shetani – Illuminati.
Mwanzo niliangua kicheko kwa maana kijana mwenyewe hana chochote wala lolote, labda anadaiwa kope si zake! Nilijiuliza inawezekanaje kipofu kuwaonyesha makengeza njia.
Iweje msajili mwenyewe anatembea kwa miguu kama mifugo ila anaahidi watu utajiri?
Ni baada ya kusoma machapisho yake kadha ambapo niligundua haukuwa utani, kijana wa watu aliaminia kikweli kuunda fedha kwa njia ya kuwaelekeza watu kwa shetani, tena hakuwaficha walengwa wake alikonuia kuwapeleka.
Nilitumia tajriba yangu ya uchunguzi kujua hasa msumuko wake ulikuwa gani, nikagundua hoja kuu ilikuwa pesa, kuukimbia umaskini.
Vijana wetu wamekosa kazi hivi kwamba wako radhi kuitwaa fursa yoyote inayotokea, hata ikiwa itahatarisha maisha yao.
Bw Omwamba ni mmoja tu kati ya vijana wengi ambao wanajaribu kila wawezalo – halali na haramu – kujikomboa kutoka kwa umaskini ambao wanadhani unahatarisha maisha yao kuliko hatari nyinginezo unazofikiria.
Ikiwa una shaka na hili, jaribu kupiga gumzo na Mkenya yeyote, hasa aliye na umri wa chini ya miaka 40. Utakumbana na swali hili: Wazee mnatoa pesa wapi ambako hamtaki kutuonyesha tutajirike?
Bila shaka kuna imani potovu miongoni mwa rika hilo kwamba kila aliye na uwezo wa kulisha familia yake, kuwalipia wanawe ada za shule na kuwanunulia mavazi, ni tajiri.
Hata hivyo, huo ndio ukweli wao. Binafsi nawaelewa kabisa kwa kuwa mwanamume wa miaka 40 asiyewahi kupata kazi, anaishi kwa wazazi wake na hana kipato chochote, anachotamani ni mahitaji ya kimsingi kama chakula na mavazi.
Wapo pia walio na umri mdogo zaidi, hasa kizazi cha Gen-Z, wanaokuuliza moja kwa hasira: Mbona wazee hamtaki kutuonyesha mnakotoa pesa, hata sisi tutajirike kama nyinyi? Wanadhani wanafichwa siri.
Ukiwaambia hata wewe unajaribu kuhifadhi pesa kadiri ya uwezo wako, kuwekeza hapa na pale ili baadaye uwe na utajiri wa kweli, wanakwambia hawana subira ya aina hiyo, si lazima wafanye mambo kama wewe ili wafanikiwe, wanachohitaji ni pesa, si hadithi ndefu!
Amini usiamini, vijana wengi nchini Kenya wanadhani kuna siri kubwa ya jinsi ya kufaulu maishani ambayo wazee wanawaficha, na jambo hilo linachochea ama hasira au ujasiri wa kufanya chochote, cha heri au shari, ili kuionyesha jamii kwamba pesa si za wazee pekee.
Wakati huu ambapo vyombo vya usalama vinajikuna vichwa na kujiuliza vitamkamataje Bw Omwamba kwa kuwasajili Wakenya kujiunga na jeshi la Urusi, anaonekana kama shujaa wa kuigwa na kupigiwa mfano machoni kwa vijana wasio na kazi.
Wanafanya hesabu zao na kupuuza maoni au ushauri mwingine wowote usiowaelekeza huko kwa kupata mafedha.
Kwa mfano, utawasadikishaje kwamba Bw Omwamba ni mhalifu ilhali anadaiwa kuwalipa makurutu kati ya Sh900,000 na Sh1.2 milioni pindi anapowasajili?
Nimetokea kijiji ambako utapata familia nyingi tu zisizoingiza Sh50 kwa wiki. Hii ina maana kwamba familia moja haipati hata Sh200 kwa mwezi! Sasa nenda huko ukawashawishi wakatae Sh1.2 milioni tuone kama utafaulu.
Usishangae wakikwambia wako radhi kuwatoa wanao wote ili watie vibindoni pesa hizo na kuondokana na umaskini kabisa. Walaumu ukitaka, lakini umaskini umewafikisha hapo na hawataki kujua utawachukuliaje.
Serikali – na hapa narejelea yeyote aliye katika nafasi ya uongozi – inapaswa kubuni fursa zaidi za kazi na kuweka mazingira rafiki yanayowawezesha wawekezaji binafsi kubuni fursa ili kuondoa hali ya kutamauka inayoshuhudiwa nchini.
Kufurukuta na kuanza kuwasaka washukiwa wa sakata kama hiyo ya makurutu wa Urusi ni kujaribu kutibu dalili za maradhi na kupuuza viini.
Wasiokwenda Urusi wanajitia vitanzi au kujiunga na magenge ya wanyang’anyi ili wasife maskini. Tatizo ni uongozi.
– Douglas Mutua ni mwanahabari Mkenya anayeishi Amerika (mutua_muema@yahoo.com)