Viongozi wajizoeshe kutofautisha rasilimali za serikali na za vyama
KUANDALIWA kwa mkutano wa wanaosaka tikiti ya UDA Ikulu kumeibua mjadala nchini. Ikulu inawahudumia Wakenya wote au chama tawala?
Ikulu ni afisi ya Rais wa Jamhuri. Yeye ni kiongozi wa taifa lote, si wa chama chake pekee.
Ingawa Rais pia ni kiongozi wa chama cha kisiasa, majukumu haya mawili hayawezi kuchanganywa bila athari.
Pale Ikulu inapogeuzwa kuwa jukwaa la shughuli za chama, kunajitokeza hisia kwamba, dola nzima imetwaliwa na chama kimoja.
Ipo mipaka kati ya serikali, vyama vya siasa na taasisi za umma. Hata hivyo, mipaka hii inaonekana kufifia.
Mkanganyiko huu hauishii Ikulu pekee. Waziri wa Fedha, anayehusishwa kisiasa na ODM anatumia jukwaa la chama—YouTube ya Azimio—kuendesha mjadala wa umma kuhusu bajeti.
Hapa tena, swali linajirudia: sera ya serikali inajadiliwa kama ajenda ya taifa au kama mradi wa kisiasa wa muungano fulani?
Bajeti ni suala la kitaifa linalogusa raia wote bila kujali mwelekeo wao wa kisiasa. Hufaa kuwasilishwa kupitia taasisi rasmi za serikali, kwa kutumia majukwaa ya umma yaliyo huru na vyama.
Pale mjadala wa kitaifa unapopelekwa kwenye majukwaa ya vyama, unageuzwa kuwa chombo cha propaganda au uhalalishaji wa kisiasa badala ya mjadala huru wa wananchi.
Kutumia rasilimali za vyama kutangaza ajenda za serikali, au kutumia majukwaa ya serikali kuhalalisha maamuzi ya vyama ni kupalilia mchanganyiko katika uongozi.
Chama tawala kinapotumia Ikulu na rasilimali zake, je, vyama vya upinzani vina fursa sawa? Kama mawaziri wanatumia majukwaa ya vyama kueleza sera za serikali, je, wananchi wasio wanachama wa vyama hivyo wanahesabiwa vipi?
Mwandishi ni msomi na mtafiti wa Kiswahili, tafsiri na ukalimani