Habari

Mhubiri agunduliwa mkulima wa bangi shambani mwake

April 1st, 2018 1 min read

KNA na PETER MBURU

Polisi mjini Naivasha wamepata bangi ambayo ina thamani ya Sh500, 000 ikienda kuuzwa na kutetekeza nyingine ya thamani ya mamilioni katika shamba la mhubiri mmoja.

Bangi iliyoharibiwa katika shamba la mhubiri huyo ilikuwa tayari kuvunwa.

Kutokana na operesheni hiyo, polisi waliweza kugundua mfumo wa wauzaji wa dawa za kulevya mjini Nakuru. Kiongozi wa kundi hilo anaaminika kuwa mhubiri wa dini la Akorino.

Akiongoza maafisa wa polisi kutoka kitengo cha Polisi wa Utawala (AP), Naibu Kamishna wa Naivasha Richard Oguoka alisema maafisa wa polisi walidokezewa kuhusu bangi hiyo na wananchi wa eneo hilo.

Wakazi hao walihoji kuwa mhubiri huyo alikuwa akipanda mmea huo katika shamba lake lililokuwa karibu na ufuo wa Ziwa Naivasha.

Akihutubia wanahabari baada ya uvamizi huo, Bw Oguoka alisema ufanisi huo uliimarisha kampeni dhidi ya matumizi ya mihadarati eneo hilo.

Aliongeza kuwa wakati wa uvamizi huo, mshukiwa alitoroka kwa kutumia boti. Alisema maafisa watafanya juu chini mpaka watakapohakikisha kuwa wamemkamata.

“Tumefahamishwa kuwa mhubiri huyo ametoka katika kanisa la Akorino na inakaa amekuwa akifanya biashara hiyo kwa muda mrefu hasa kutokana na habari tuliyopata leo,” alisema Oguoka.

Alisema operesheni hiyo itaendelezwa hadi maeneo mengine Naivasha ili kuhakikisha kuwa mji huo ni salama, kwa kusema kuwa wauzaji wa mihadarati wanatishia vizazi.

Naibu kamishna huyo alisema machifu wataendelea na operesheni hiyo kwa kuingia kila boma eneo hilo.