Gor washindwa kumeza ‘boflo’ huku Naibois wakivuna MozzartBet
BB BREAD Jumapili, Machi 8, 2026 iliwaangushia ‘Goliath’ Gor Mahia kipigo cha 1-0 uwanja wa Kitaifa wa Nyayo na kufuzu raundi ya 16 ya Kombe la MozzartBet.
Mnamo Februari 10, timu hiyo ilibandua AFC Leopards kupitia mkwaju wa penalti na kufuzu raundi ya 32 kutoka ile ya 64.
Denis Cheni ambaye pia alifunga dhidi ya AFC Leopards ndiye jana alicheka na nyavu za Gor Mahia na kuwabandua kwenye MozzartBet.
“Tulijua tutakutana na timu kubwa na kocha amefanya tujiamini sana kwa sababu mbinu ni zake. Baada ya kutoa Gor na AFC, sasa sisi tunaona tukifika katika fainali,” akasema Chieni.
Kocha wa timu hiyo ni Azastine Okoba.
BB Bread inayoshiriki Ligi ya Shirikisho la Soka Nchini (FKF) Nairobi Magharibi sasa ni kati ya timu zinazoshiriki ligi za chini ambazo zimesalia katika mashindano hayo.
Hii ina maana kuwa Gor wamebanduliwa Kombe la MozzartBet na sasa nafasi yao ya mechi za CAF ni kushinda ubingwa wa Ligi Kuu Nchini (KPL).
Kando na masaibu ya Gor, timu nyingine zinazoshiriki KPL nazo ziliendelea kutamba dhidi ya wapinzani kutoka ligi za chini.
Mabingwa watetezi Nairobi United waliweka hai matumaini yao ya kuhifadhi taji hilo, wakiwashinda BMC All Stars 8-0 uwanja wa Ulinzi Sports Complex.
Mvamizi Benson Omala, Ashraf Thaire na Benard Magare waliyafunga mabao mawili kila moja huku Duncan Omala na Shami Kibwana wakiongeza mengine.
Humprey Aroko naye alifunga mabao manne na kusaidia Kariobangi Sharks kuwachapa KU Hardnuts 4-0 uwanja wa Kasarani.
Mabingwa wa 2023 Kakamega Homeboyz nao walishinda Kipchimchim FC 3-0 huku Oliver Majak akifunga mabao mawili na Eston Omengo akiongeza jingine uwanja wa Bukhungu.
Dinken Mwema alifungia Posta Rangers magoli mawili Oinopsos 2-0 uwanja wa Afraha Kaunti ya Nakuru.
Chebaiywa Lions nao waliwapiga Gucha Youth 2-0 uwanja wa DMI St Joseph’s Science School, Eldoret nao.
Murangá Seal walifunga Dynamo FC 1-0 uga wa SportPesa Arena kupitia goli la Victor Haki kipindi cha kwanza.