Kenya kuandaa fainali, Tz mechi ya ufunguzi, UG wakiangukia ‘makombo’ CHAN
FAINALI ya Kombe la Afrika kwa wachezaji wanaocheza ligi ya nyumbani maarufuku kama CHAN itasakatwa Kenya.
Shirikisho la Soka Afrika (CAF) Jumanne lilitangaza kuwa fainali hiyo sasa itagaragazwa uga wa MISC Kasarani mnamo Agosti 30.
Mechi ya kwanza na sherehe ya ufunguzi wa kipute hicho kinachoonza Agosti 2 hadi Agosti 30 nayo itasakatwa kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa, jijini Dar es Salaam Tanzania.
Hii ina maana kuwa hata sherehe ya ufunguzi ya CHAN itafanyika kwenye uga wa Benjamin Mkapa, Tanzania.
Uganda nao watakuwa mwenyeji wa mechi ya kupigania nafasi ya tatu pamoja na mechi ya nne ya mashindano hayo. Mechi hizo zitaandaliwa katika uwanja wa Mandela, jijini Kampala.
Mara ya mwisho CHAN iliandaliwa kwenye ukanda wa Afrika Mashariki ni mnamo 2016 ilipofanyika kule Rwanda.
Aidha Zanzibar imeorodheshwa kati ya nchi ambazo zitakuwa mwenyeji wa kipute hicho. Uwanja wa Amaan Zanzibar utakuwa mwenyeji wa baadhi ya mechi ya makundi yanayofanyika Tanzania.
Uga huo uliandaa mkondo wa pili wa fainali ya Kombe la Mashirikisho Afrika (Caf) Mei mwaka huu. Mechi hiyo ilikuwa kati ya mabingwa RS Berkane na wenyeji Simba SC.
KUNDI A (Mechi zake kuchezwa Nairobi, Kenya)
Kenya, Morocco, Angola na DR Congo
KUNDI B (Mechi kuchezwa Dar es Salaam, Tanzania)
Tanzania, Madagascar, Mauritania, Burkina Faso, Jamuhuri ya Afrika ya Kati
KUNDI C (Mechi kuchezwa Kampala, Uganda)
Uganda, Niger, Guinea, Afrika Kusini na Algeria
KUNDI D (Mechi kuchezwa Zanzibar)
Senegal, Congo, Sudan na Nigeria