• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 5:45 AM
Kocha wa Chemelil awataka vijana wake kufuata maagizo

Kocha wa Chemelil awataka vijana wake kufuata maagizo

Na CECIL ODONGO

KOCHA wa muda wa Klabu ya Chemelil Charles Odera amewataka wanasoka wake kukumbatia mbinu zake mpya za ukufunzi ili wasibabaike uwanjani jinsi walivyofanya katika mechi yao ya Jumamosi dhidi ya limbukeni Wazito FC.

Mkufunzi huyo ambaye alichukua nafasi hiyo kutoka kwa Patrick Odhiambo aliyekimbilia majirani zao na wanasukari wenza SoNy Sugar kama kocha mpya.

Mechi hiyo ikiwa ya kwanza kwake, Kocha Odera alikiongoza kikosi hicho kuwachabanga Wazito FC mabao 3-1 katika uwanja wao wa nyumbani.

Odera ambaye enzi zake alichezea timu hiyo na hata kutwaa mkoba wa unahodha alisema japo walitwaa ushindi, hakuridhishwa na jinsi wachezaji wake walivyosakata kabumbu duni.

“Kwa leo hatukucheza soka yetu. Niliwapa maagizo ya jinsi ya kuwakabili wapinzani wetu lakini hawakuyafuata,” alisema Odera akishiriki katika mahojiano baada ya mechi hiyo.

Hata hivyo alama hizo ziliwawezesha Chemelil kuimarisha nafasi yao ligini wakiwa sasa wapo katika nafasi ya sita alama moja tu nyuma ya nambari tano Sofapaka FC japo bado wana mechi moja hawajacheza.

Klabu hiyo mbili zinatarajia kugaragazana siku ya Jumamosi kwenye mtanange mkali wa ligi katika uwanja wa Chemeli Sport Complex kuanzia saa saba mchana.

Baada ya kupokezwa kichapo hicho Klabu ya Wazito ambayo wanashiriki msimu wao wa kwanza ligini sasa wameteremka hadi katika nafasi 12 kwenye msimamo wa jedwali la ligi.

You can share this post!

Korti yaruhusu NCIC na Kuria kusuluhisha kesi ya uchochezi

Rangers yalenga nafasi ya 3 ikimenyana na SoNy Sugar

adminleo