• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 7:50 PM
Makocha wa timu za raga Kenya watangaza vikosi vya Hong Kong Sevens

Makocha wa timu za raga Kenya watangaza vikosi vya Hong Kong Sevens

Na GEOFFREY ANENE

MAKOCHA wakuu wa timu za taifa za raga za Kenya za Innocent Simiyu (wanaume) na Kevin Wambua (wanawake) wametangaza vikosi vitakayoshiriki mashindano ya Hong Kong Sevens na Jumuiya ya Madola mwezi Aprili.

Simiyu amefanya mabadiliko mawili katika kikosi chake kilichofika fainali ya Raga za Dunia duru ya Vancouver Sevens nchini Canada mnamo Machi 11 akiita Ian Minjire na Augustine Lugonzo kujaza nafasi za Samuel Ng’ethe na Erick Ombasa.

Ni mara ya kwanza kabisa Minjire amejumuishwa katika kikosi kitakachoshiriki Raga za Dunia ambazo zitaingia duru ya saba mjini Hong Kong. Lugonzo alikosa duru za Marekani (Machi 2-4) na Canada (Machi 10-11) kwa sababu za kibinafsi.

Baada ya Hong Kong Sevens mnamo Aprili 6-8, Shujaa itaelekea mjini Gold Coast nchini Australia kwa mashindano ya Jumuiya ya Madola (Aprili 13-15) na kisha duru ya nane ya Raga za Dunia nchini Singapore (Aprili 28-29) kabla ya kurejea nyumbani.

Wambua ametaja wachezaji 12 kwa mechi za kufuzu kushiriki Raga za Dunia za wanawake mjini Hong Kong mnamo Aprili 5-6. Stacy Awuor atajiunga na Lionesses mjini Gold Coast.

Katika mechi za makundi za Hong Kong, Shujaa italimana na Australia, Uhispania na Canada nayo Lionesses imekutanishwa na Afrika Kusini, Mexico na Papua New Guinea.

Mjini Gold Coast, Shujaa itavaana na New Zealand, Canada na Zambia katika mechi za makundi nayo Lionesses ilimane na New Zealand, Canada na Afrika Kusini katika awamu hiyo.

Vikosi:

Shujaa

Oscar Ouma (Nakuru, nahodha), Samuel Oliech (Impala Saracens), Andrew Amonde (KCB), William Ambaka (Kenya Harlequins), Daniel Sikuta (Kabras Sugar), Arthur Owira (KCB), Collins Injera (Mwamba), Eden Agero (Kenya Harlequins), Billy Odhiambo (Mwamba), Jeffery Oluoch (Homeboyz), Nelson Oyoo (Nakuru), Ian Minjire (Impala Saracens), Augustine Lugonzo (Homeboyz).

Benchi la kiufundi – Innocent Simiyu (Kocha Mkuu), Will Webster (Kocha Msaidizi), Geoffrey Kimani (Kocha wa mazoezi ya viungo), Lamech Bogonko (Daktari), Erick Ogweno (Meneja wa Timu).

 

Lionesses

Philadelphia Olando (nahodha), Sheila Chajira (nahodha msaidizi), Grace Adhiambo, Judith Auma, Sinaida Aura, Doreen Remour, Celestine Masinde, Linet Moraa, Rachel Mbogo, Janet Owino, Janet Okello na Camila Cynthia. Stacy Awuor atajiunga na kikosi mjini Gold Coast. Benchi la kiufundi – Kevin Wambua (Kocha Mkuu), Samuel Njogu (Kocha wa mazoezi ya viungo), Ben Mahinda (Daktari), Camilyne Oyuayo (Meneja wa Timu).

You can share this post!

Chipu yabandua Madagascar kutinga fainali Namibia

Harambee Stars yarejea nchini baada ya matokeo ya kukera

adminleo