• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 11:33 PM
Man United walivyoponea kupigwa rungu na limbukeni Coventry gozi la FA

Man United walivyoponea kupigwa rungu na limbukeni Coventry gozi la FA

NA MASHIRIKA

MANCHESTER United watahitaji kurekebisha makosa mengi waliyofanya kwenye nusu-fainali ya Kombe la Shirikisho la Soka la Uingereza (FA Cup), baada ya kuipiku Coventry City kupitia mikwaju ya penalti uwanjani Wembley Jumapili.

Hizi ndizo kauli za kocha Erik ten Hag na kipa Andre Onana baada ya timu hiyo kufuzu kibahati fainali ya FA kwa mwaka wa pili mfululizo.

“Lazima tuwe makini zaidi katika mechi. Mara kadha katika gemu tulijiletea balaa wenyewe. Leo tumeponea kabisa,” alihoji Ten Hag ambaye chuma chake kingali motoni kutokana na msimu wao duni, huku kismati cha Jumapili kikikosa kutuliza tumbojoto la mashabiki wala wamiliki wapya wa Man-United.

Tathmini ya mkufunzi huyo raia wa Uholanzi iliungwa mkono na kipa Andrea Onana aliyekiri utepetevu wao ungeliwasomba Jumapili.

“Baada ya makosa mengi ya kibinafsi tuliruhusu mabao yao matatu. Tulipoteza udhabiti wa mchezo. Kitu muhimu zaidi ni kushinda. Sasa tunapiga darubini mbele kwa michezo inayokuja. Tunafurahi kuwa kwenye fainali. Tutarejea hapa kushinda, sisi ni Manchester United!” Onana alisema baada ya mechi.

Man-United walikuwa wakiselelea 3-0 zikisalia dakika 20 mechi ifike tamati kupitia magoli ya Scott McTominay, Harry Maguire na Bruno Fernandes.

Lakini ghafla bin vu mambo yakabadilika Coventry waliposawazisha kupitia Ellis Simms dakika ya 71, Callum O’Hare (79′) na Haji Wright (90’+5 penalti).

Mechi ikalazimika kuchezwa dakika 30 za ziada ambapo Coventry wangalivuna ushindi ila bao la Victor Torp likatupwa nje na refa wa video (VAR) kwa kuotea.

Baada ya dakika zote 120 bila kufungana tena ililazimu matuta ya penalti kuamua mshindi, ambapo pia mambo yangeenda mrama kwa Man-United kwani mkwaju wa kiungo mkabaji Casemiro ulinyakwa na kipa Bradley Collins.

Kuyoyomea nje

Hata hivyo, Onana alikuwa mwokozi alipodaka penalti moja ya Coventry na nyingine kuyoyomea nje kabla straika Rasmus Hojlund kutumbukiza la ushindi lililohakikisha Red Devils wanaondoa aibu ya kubanduliwa kombe hilo na timu inayoshiriki Ligi ya Daraja ya Pili (Championship).

Man-United maarufu Red Devils sasa watamenyana na mabingwa watetezi wa kombe hilo Manchester City katika debi nyingine ya Manchester ugani humo humo Wembley mnamo Mei 25.

Man-City ilifuzu Jumamosi baada ya kufinya Chelsea 1-0 uwanjani Wembley kufuatia bao la pekee la kiungo mshambulia Bernardo Silva dakika ya 84.

United sasa itamenyana na mabingwa watetezi wa FA Manchester City katika debi nyingine ya fainali ya Kombe la FA itakayochezwa ugani Wembley Mei 25, mwaka huu.

City ilifuzu Jumamosi baada ya kuinyorosha Chelsea 1-0 ugani Etihad. Kiungo Bernardo Silva alifunga bao la pekee la mchezo dakika ya 84.

Nayo United ilifuzu Jumapili baada ya ushindi wa 4-2 dhidi ya Coventry City kupitia mikwaju ya penalti, baada ya mechi hiyo kuishia sare ya 3-3 muda wa kawaida.

United iliponea kuondolewa kwenye nusu fainali dakika za lala salama muda wa nyongeza, lakini VAR ilitupilia mbali bao la Victor Torp. VAR ilionyesha kuwa, Haji Wright alikuwa ameotea kabla ya kumpa Torp pasi.

“Ni hisia tofauti. Ulikuwa mchezo mgumu mwishoni tulimakinika. Baada ya makosa mengi ya kibinafsi tuliruhusu mabao matatu. Kitu muhimu zaidi ni kushinda. Lazima tuangalie mbele kwa michezo inayokuja. Kwa namna fulani tulipoteza udhabiti wa mchezo. Sisi ni United. Lazima tushinde. Tunajisikia vizuri, tunajisikia furaha kuwa kwenye fainali. Tutarejea hapa kushinda,” Onana aliambia BBC baada ya mchezo huo.

Msimu jana, United ilikosa kufika fainali dhidi ya Manchester City ambapo City walipata ushindi wa 2-1 na kuingia fainali.

Arsenal ndio timu ya pekee ambayo imeshinda mataji mengi ya FA (14) ikifuatawa na City (12), Chelsea, Liverpool na Tottenheam ambao wanafunga tano bora na makombe manane kila mmoja.

  • Tags

You can share this post!

Watu sita waangamia, saba wakipata majeraha katika ajali ya...

Kaunti ya Samburu yageukia maombi ili kukabili ujangili

T L