Rising Starlets sasa ngangari kukabili Tanzania dimba la U-20
KOCHA wa Rising Starlets, Jackline Juma, amesema kuwa Kenya iko tayari kukabiliana na Tanzania katika mechi mbili za raundi ya tatu ya kufuzu kwa Kombe la Dunia la Wanawake la mwaka huu chini ya miaka 20.
Mechi ya kwanza itachezwa nyumbani Jumamosi hii katika Uwanja wa Michezo wa Ulinzi jijini Nairobi saa tisa alasiri, ikifuatiwa na mechi ya marudiano siku saba baadaye katika Uwanja wa Azam Sports Complex Chamazi jijini Dar es Salaam.
Mshindi wa jumla atasonga mbele hadi raundi ya nne na ya mwisho na atakabiliana na mshindi kati ya Cameroon na Botswana, huku mechi ya kwanza ikipangwa kufanyika Mei 1-3 na mechi ya pili Mei 8-10.
“Tunaheshimu Tanzania. Tunatambua kuwa wao ni timu ngumu, lakini tumejiandaa vizuri,” alisema Juma, mwenye leseni ya kocha wa kiwango cha A.
Hapo awali, Juma alitaja kikosi cha muda cha wachezaji 60, ambacho kilipunguzwa hadi kikosi cha mwisho cha wachezaji 23 ambao aliwataja kuwa kikosi cha mwisho Jumanne wiki hii.
“Uteuzi wa kikosi uliangazia utayari na uthabiti wa kimwili wa mchezaji, jambo ambalo lilisababisha kuondolewa kwa wachezaji ambao walihangaika kambini,” alisema Juma, akiongeza, “Wachezaji wanaocheza katika ligi hawakupata matatizo.”
Beki Jenevive Mithel anarejea kwenye timu ya taifa, akileta uzoefu wa kimataifa kutoka kwa kipindi chake na kikosi cha Kenya cha U17 Junior Starlets kilichoshiriki katika Kombe la Dunia la Wanawake la 2024 katika Jamhuri ya Dominican.
Mshambuliaji Hilder Natecho na Pauline Nelima pia watajiunga na Rising Starlets, na hivyo kujiunga na kikosi cha timu ya taifa kwa mara ya kwanza.
Ili kufika hatua hii, Kenya haikucheza raundi ya kwanza. Lakini, waliinyorosha Ethiopia 5-1 kwa jumla ya mabao katika raundi ya pili mnamo Novemba mwaka jana.
Tanzania, kwa upande wake iliishinda Angola kwa jumla ya mabao 7-0 katika raundi ya pili.
KIKOSI CHA MWISHO
Walinda lango
Christine Adhiambo, Velma Abwire (Ulinzi Starlets), Ephy Awuor (Soccer Assassins)
Mabeki
Jenevive Mithel (Nyakack Girls), Triza Ekesa (Gideon Starlets), Dorcas Glender (Ulinzi Starlets), Diana Anyango (Kenya Police Bullets), Elizabeth Ochaka (Kenya Police Bullets), Lorine Ilavonga (Ulinzi Starlets), Patience Asiko (Butere Girls), Pauline Namisi (Dessert Scorpions)
Viungo wa kati
Pearl Olesi (St Joseph’s Girls), Lornah Faith, Halima Imbachi (Kenya Police Bullets), Susan Akoth (Zetech Sparks), Jerrine Adhiambo (Mathare United Women), Vidah Akeyo (Kenya Police Bullets), Rebecca Odato (Kenya Police Bullets), Fasila Adhiambo (Simba Queens)
Washambuliaji
Valarie Nekesa (Soccer Assassins), Hilder Natecho (Arch Bishop Njenga), Emily Morang’a (Kenya Police Bullets), Elizabeth Mideva (Ulinzi Starlets)