Sara Mose hashikiki mashindano ya kuogelea kitaifa 50m Freestyle
SARA Mose, ambaye ni muogealaji wa pili kwa kasi nchini Kenya katika mbio za mita 50 mtindo wa Freestyle, alidhihirisha ubabe wake katika mbio hizo kwa kundi la wenye umri wa miaka 18 na zaidi katika Mashindano ya Taifa ya Kuogelea yaliyoandaliwa na Kenya Aquatics katika Kituo cha Kuogelea cha Kimataifa cha Kasarani, Jumamosi, Mei 31, 2025.
Akiwakilisha klabu ya Fit Hub, Sara alikamilisha kitengo hicho kwa sekunde 26.10, na kuwazima wenzake waliobobea, akiwemo Imara Bella Thorpe, 24, kutoka Barracuda Aquatics (27.02) na Victoria Okumu wa USIU-A Dolphins SC (29.28) waliomaliza nafasi ya pili na ya tatu, mtawalia.
Sara alizaliwa nchini Poland na ana baba Mkenya na mama kutoka Poland.
Muogeleaji huyo mwenye umri wa miaka 18 alirejea Kenya wiki mbili kabla ya mashindano hayo ili kujizoesha na kufanya mazoezi akilenga kufuzu kwa Mashindano ya Dunia yatakayofanyika baadaye 2025.
Ingawa alikiri kuwa ushindani ulikuwa mkali, alieleza furaha yake ya kushindana na waogeleaji wenye viwango vya juu katika kundi lake. Pia, anapanga kushiriki katika mbio za mita 100 Freestyle, mita 50 mtindo wa Butterfly na mita 50 mtindo wa Breaststroke katika mashindano hayo ya Kasarani.
Katika mbio za mita 200 Butterfly kwa wasichana, Havya Shah,11, kutoka Shule ya Kenton aling’ara kwa dakika 3:16.32. Aliwabwaga Salima Omar wa Bandari SC (3:26.65) na Leyna Borega wa North Coast SC (3:41.51).
Havya alieleza kuwa kushiriki mashindano hayo ya kitaifa ni jambo la kunyenyekea na alieleza ndoto yake ya siku moja kuiwakilisha Kenya katika ulingo wa kimataifa.
Mkurugenzi wa mashindano ya kitaifa, Max Kanyerezi, ambaye pia ni mjumbe wa Kamati ya Ufundi ya World Aquatics na mwenyekiti wa Africa Aquatics Zone 3, alisifu maandalizi ya Kenya na ubora wa bwawa na miundombinu.
Mkurugenzi wa Ufundi wa Kenya Aquatics, Omar Omari, ambaye pia ni kocha wa Shule ya Crawford International, alifurahishwa na idadi ya waogeleaji zaidi ya 400, akisema hilo linaonyesha kuongezeka kwa mvuto wa mchezo huo nchini.
Mashindano hayo ya siku tatu yatakamilika Juni 1, ambapo matokeo yatatumika kuchagua timu zitakazowakilisha Kenya kwenye Mashindano ya Dunia kwa watu wazima nchini Singapore (Julai 2025) na vijana nchini Romania (Agosti 2025).