• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 11:33 PM
Thika Queens wajinusuru dhidi ya Makolanders

Thika Queens wajinusuru dhidi ya Makolanders

Na JOHN KIMWERE

MALKIA wa zamani katika Soka ya Ligi Kuu ya Kenya (KWPL), Thika Queens ilitolewa kijasho chembamba kabla ya kutwaa magoli 4-3 mbele ya Makolanders Uwanjani Camp Toyoyo Jericho, Nairobi.

Nayo Nyuki Starlets ilitia pointi nne kapuni ilipolaza Spedag Ladies mabao 3-1 kisha kugana sare tasa na Soccer Queens huku bingwa mtetezi, Vihiga Queens ikituzwa ufanisi wa mezani dhidi ya Vihiga Leeds. Thika Queens iliingia mzigoni kupiga gozi la kuchana nguo ili kufungua mbio zake vyema.

Mwanahalima Adams ambaye pia huchezea Harambee Starlets alipiga ‘hat trick’ wakati Rachel Mwema akitingia Thika Queens bao moja.

”Tulibeba alama zote lakini mechi hiyo iliashiria mambo siyo rahisi mwaka huu,” alisema kocha wa Thika, Benta Achieng na kuongeza lazima wajikaze kwa udi na uvumba. Naye Sharon Adhiambo wa makolanders alifuma kombora mbili huku Farida Nyarutso akifunga goli moja.

Nayo Wadadia ilinyamazisha Eldoret Falcons kwa mabao 2-1 kupitia Marion Abiola na Cynthia Ngaira naye Grace Khatete aliifungia Eldoret Falcons bao la kufuta machozi.

Kwenye mechi zingine, Kisumu Allstars ilibanwa mabao 3-1 na Trans Nzoia Falcons, GASPO ilipepeta Kibera Girls Soccer Academy (KGSA) magoli 5-1, Spedag Ladies ilitoka nguvu sawa bao 1-1 na Oserian Ladies huku Kayole Starlets iliagana sare tasa dhidi ya Mathare Women United.

  • Tags

You can share this post!

Butterfly FC na MKU Thika zavuna ushindi

LYDIA MUKAMI: Chipukizi mwenye ndoto ya kufikia upeo wa...

adminleo