• Nairobi
  • Last Updated May 19th, 2024 9:01 PM
Thika Shakers Academy yasaidia vijana kujiimarisha katika talanta na nidhamu

Thika Shakers Academy yasaidia vijana kujiimarisha katika talanta na nidhamu

Na LAWRENCE ONGARO

NI kituo kimojawapo cha kukuza vipaji vya wanasoka chipukizi kwa kuinua mchezo wao wakilenga kuafikia viwango vya kimataifa baadaye.

Thika Shakers Academy ni kituo kilichoko mtaani Makongeni, Thika na kwa muda sasa kimekuwa chini ya kocha Swaleh ‘Betto’ Harub tangu mwaka 2018.

“Tuliunda kituo hiki kwa lengo la kukuza talanta za chipukizi hawa ikiwemo kuwafunza maadili mema katika jamii. Pia tunawaepusha na maovu kupitia kucheza soka,” akasema kocha.

Kufikia sasa kituo hicho kimezalisha wachezaji kadha ambao huenda watapata nafasi katika klabu maarufu za humu nchini hivi punde.

Kocha Harub anasema kituo hicho kina wanasoka chipukizi wapatao 150 ambao miaka yao kiumri ni 10 hadi 20.

Thika Shakers Academy yasaidia vijana kujiimarisha katika talanta na nidhamu. Picha/ Hisani

Kocha huyo anawahimiza wazazi kuzingatia mambo mawili kwa wana wao. Mambo hayo ni kuzingatia masomo na michezo hasa soka.

“Mambo hayo mawili yanastahili kuambatana pamoja ili mwanasoka yeyote aweze kupiga hatua kimaisha,” akasema kocha huyo.

Pia anawapongeza Bethwel Onyango na Kenneth Ambaye ambao kwa uwezo wao wamekuwa mstari wa mbele kuona ya kwamba chipukizi hao wanapiga hatua zaidi.

“Jambo muhimu ninalotilia mkazo ni nidhamu,” alisema kocha huyo.

Thika Shakers Academy kuna vitengo tofauti vya wachezaji. Kuna chipukizi wasiozidi umri wa miaka 10, 12, 15 na 20.

Kocha Harub ana ujuzi wa hali ya juu kwa sababu amenoa klabu kadha za humu nchini.

Kocha huyo amekuwa na West Kenya Sugar FC, Kericho Zoo FC, Timsales FC ma Pioneer High School FC ya Murang’a.

Licha ya pandashuka za hapa na pale kituo hicho kinajizatiti kufanya mema katika siku zijazo.

Thika Shakers wanategemea wanasoka Martin Kazungu, Arafat Harub, Jimmy Odera, Kelvin Kinoti, John Mutua na Joseph Shonko. Wengine ni Reuben Kyali, Joseph Ng’a ng’a, Eugene Rakwar na Austin Karanu.

Anasema yeye kama kocha anajitahidi kuhakikisha soka ya vijana hawa katika eneo la Thika inaleta mshikamano baina ya wakazi.

Kocha huyo anasema kikosi chake hufanya mazoezi mara tatu kwa wiki; Alhamisi, Ijumaa na Jumamosi katika uwanja wa ICT, Makongeni mjini Thika.

Anasema nidhamu ya wachezaji wa kikosi hicho ndiyo siri ya ufanisi.

“Tuko na nidhamu ya kutosha na hii huvutia wengi kutaka kucheza nasi,” akasema kocha huyo.

You can share this post!

Raila afafanua kuhusu mkanganyiko kwenye hotuba yake

Manchester City washinda Olympiakos 1-0