Habari za Kitaifa

Ruto aagiza familia za wanafunzi waliofariki motoni Nyeri zisaidiwe maafa yakifikia 17

Na BENSON MATHEKA September 6th, 2024 1 min read

IDADI ya wanafunzi waliofariki katika mkasa wa moto ulioteketeza bweni la Shule ya Hillside Endarasha Academy, Kaunti ya  Nyeri imefikia 17.

Rais William Ruto ameagiza idara zinazohusika kuchunguza kwa kina kisa hicho cha kuhuzunisha na kuchukua hatua za kisheria kwa waliohusika.

“Tunafariji familia za watoto waliopoteza maisha yao katika mkasa wa moto katika shule ya Hillside Endarasha Academy, Nyeri,” Rais Ruto alisema katika ujumbe aliotuma kutoka China.

Alisema kuwa wizara ya usalama wa ndani itafanya kila juhudi kusaidia familia zilizoathirika.

Msemaji wa Huduma ya Kitaifa ya Polisi Dkt Resila Onyango  alisema timu ya maafisa wa uchunguzi imetumwa katika shule hiyo iliyoko eneobunge la Kieni, Kaunti ya Nyeri.

Wanafunzi 16 walithibitishwa kufariki ndani ya bweni na mmoja akafariki alipofikishwa hospitalini.

“Kumi na sita walichomeka kiasi cha kutotambulika, huku mmoja akifariki alipokuwa akipelekwa hospitalini,” Msemaji wa polisi aliambia Nation FM.

“Tunachunguza kilichosababisha moto huo na tutachukua hatua zinazohitajika,” aliongeza.

Timu ya wachunguzi inaongozwa na Naibu Mkurugenzi wa Idara ya Upelelezi wa Jinai  (DCI), John Onyango, na maafisa kutoka Afisi ya Inspekta Jenerali wa Polisi.

“Moto ulizuka katika bweni, ulizuka usiku na bado hatujabaini kilichousababisha,” alisema Dkt Onyango.

Kuna hofu kuwa huenda idadi ya waliokufa ikaongezeka huku wanafunzi 14 wakilazwa hospitalini.