Siasa

Baraza kuu ODM kukutana kwa dharura baada ya Sifuna ‘kutikisa’ na Linda Mwananchi

Na MOSES NYAMORI February 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

BARAZA Kuu la chama cha Orange Democratic Movement (ODM) limeitisha kikao cha dharura leo Jumatano kujadili mivutano inayozidi kushika kasi ndani ya chama hicho pamoja na kile kinachotajwa kuwa mapinduzi ya kisiasa ndani ya muungano wa Azimio, yanayodaiwa kupangwa na Rais (mstaafu) Uhuru Kenyatta.

Maafisa wakuu wa ODM wamethibitisha kuwa kiongozi wa chama hicho, Seneta Oburu Oginga, ataongoza kikao cha Kamati Kuu ya Kitaifa (NEC) kitakachofanyika Mombasa.

Hata hivyo, uongozi wake unaendelea kupingwa na kundi pinzani linalojumuisha Katibu Mkuu wa chama Edwin Sifuna, naibu kiongozi wa chama Godfrey Osotsi, pamoja na Gavana wa Siaya James Orengo.

Kikao cha NEC kinajiri wakati inaripotiwa kuwa Dkt Oginga alifanya jitihada za haraka Jumatatu kupunguza mgawanyiko uliokuwa ukitishia kuvuruga chama, kufuatia mkutano wa hadhara uliofanikiwa kwa kiasi kikubwa mjini Busia ulioandaliwa na kundi pinzani.

Inadaiwa aliwaalika Bw Sifuna na Bw Osotsi kwenye kikao, ingawa Bw Osotsi alikana kufahamu kuhusu mkutano huo.

Wakati huo huo, wanachama wengine wa ODM, akiwemo Waziri wa Fedha John Mbadi, wametoa wito wa kumwondoa Bw Sifuna katika wadhifa wake wa Katibu Mkuu.

Hata hivyo, maafisa waliothibitisha kuhudhuria kikao cha leo walisema hakuna mpango wa kumuondoa afisa yeyote.

“Huu ni wakati muhimu sana. Kwa maslahi ya chama, baadhi ya watu lazima waondoke. Baadhi yetu tutahakikisha ODM inabaki imara kuanzia ngazi ya mashinani. Tutawaunganisha wanachama wetu kumuunga mkono Oburu Oginga, aliyesimama imara nyuma ya Raila Odinga licha ya kuwa kaka yake mkubwa,” alisema Bw Mbadi.

Taifa Leo ilipata ajenda ya awali ya kikao hicho, inayojumuisha maandalizi ya Mkutano wa Kitaifa wa Wajumbe (NDC) ambao sasa umezua mgawanyiko, tathmini ya utekelezaji wa ajenda ya vipengele 10 iliyotiwa saini kati ya ODM na UDA.