Dalili Muungano wa Upinzani utatafuta jina jipya na kuachana na lile ‘Azimio’ kuelekea 2027
MUUNGANO wa Upinzani sasa unaelekea kuachana rasmi na Azimio la Umoja-One Kenya kama chombo chake cha kisiasa, na badala yake kuunda muungano mpya katika azma yao ya kumuondoa madarakani Rais William Ruto katika Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Msemaji wa muungano huo Dkt Mukhisa Kituyi amesema hakuna mjadala wowote uliofanyika kuhusu kufufua Azimio katika muundo wake wa sasa.
“La. Kama muungano wa upinzani hatujajadili kufufua Azimio. Tuna kikao cha mapumziko mwishoni mwa wiki kujadili masuala mbalimbali, likiwemo hili, na tutatoa taarifa kamili Jumatatu alasiri baada ya kikao chetu Naivasha,” alisema Dkt Kituyi.
Kauli yake inajiri wiki chache baada ya mwenyekiti wa Azimio, Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta, kumteua kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka kuwa kiongozi mpya wa muungano huo baada ya kifo cha aliyekuwa kinara wake, Raila Odinga.
Hatua hiyo ilionekana kama juhudi za kuimarisha Azimio kama mpinzani mkuu wa Kenya Kwanza katika uchaguzi ujao.
Hata hivyo, dalili zinaonyesha kuwa baadhi ya viongozi wa muungano huo wanapendelea jina na muundo mpya wa kisheria kwanza, wakidai kuwa Azimio ina kivuli cha kisiasa cha uchaguzi uliopita.
Naibu kiongozi wa DCP, Cleophas Malala alisema Azimio bado ni muungano halali unaotambuliwa chini ya Sheria ya Vyama vya Kisiasa, na kwamba hatua yoyote ya kuuvunja lazima ifuate utaratibu wa kisheria.
“Azimio ni muungano uliosajiliwa kisheria na una masharti yake. Kuvunjwa kwake lazima kufuate sheria. Lakini pia sheria inaruhusu kushirikiana na vyama vingine, kwa hivyo bado ni mchezo wa wazi,” alisema.
Alisisitiza kuwa lengo kuu la muungano huo ni moja: kuhakikisha Rais Ruto anahudumu muhula mmoja pekee.
“Mradi tu wanaamini katika ‘Wantam’, sisi tutafanya kazi na yeyote. Lengo ni moja—Ruto aondoke,” aliongeza.
Hata hivyo, ODM imeweka msimamo mkali dhidi ya mabadiliko yoyote katika Azimio bila idhini yake. Kiongozi wa ODM, Dkt Oburu Oginga alisema hakuna uamuzi wowote unaoweza kufanywa bila ushiriki wa chama hicho.
“Azimio ni sisi. ODM ndio chama kikubwa na chenye nguvu zaidi ndani yake. Huwezi kuteua kiongozi au kufanya maamuzi bila makubaliano yetu,” alisema.
Aliongeza kuwa kimsingi Azimio ilikoma kuwapo ODM ilipojiondoa, na kwamba chama hicho kitathibitisha rasmi kujiondoa kwake hivi karibuni.
Jana, chama hicho cha Chungwa kilitangaza kuwa kitajiondoa rasmi katika muungano huo.
Mchanganuzi wa siasa Chris Omore anasema mjadala huu si wa jina pekee bali ni wa ushawishi na udhibiti wa mwelekeo wa muungano.
“Hili si suala la chapa tu. Ni nani atakayeshikilia usukani wa muungano. Ikiwa Azimio itatumika, wale waliounda awali watakuwa na ushawishi mkubwa zaidi,” alisema.
Kikao cha Naivasha kinatarajiwa kujadili pia miundo kadhaa ya ugavi wa madaraka, ikiwemo Rais, Naibu Rais na hata Waziri Mkuu iwapo katiba itarekebishwa baada ya 2027.
Kwa upande wake, Rais Ruto amepuuza kauli mbiu ya “Wantam” akisema uamuzi wa mwisho uko mikononi mwa wapigakura.
Viongozi wa upinzani wamesema watawasilisha mgombea wao wa pamoja na mfumo wa ugavi wa madaraka ifikapo Desemba 2026, wakieleza kuwa kufichua mapema kunaweza kuvuruga mipango yao.