Siasa

Dalili Rais Ruto ni ‘Jenerali bila wanajeshi’ Mlimani

Na MWANGI MUIRURI March 31st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KUZOMEWA kwa baadhi ya wabunge wa Mlima Kenya katika Kaunti ya Kiambu mwishoni mwa juma lililopita kumefichua kuongezeka kwa hasira miongoni mwa wakazi, hali inayoonyesha hatari inayowakabili viongozi kuelekea uchaguzi wa 2027 hasa washirika wa Rais William Ruto.

Wachambuzi wa siasa wanasema tukio hilo linaonyesha mazingira tata ya siasa katika eneo la Mlima Kenya, ambako malalamishi ya wananchi, ushindani wa kisiasa wa kaunti na matamanio ya kitaifa vinakutana, na kuunda mazingira tete kwa viongozi wanaojaribu kudumisha uungwaji mkono.

Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa Kimani Ichung’wah, wawakilishi wa wanawake wa Murang’a na Kiambu Betty Maina na Anne Wamuratha mtawalia, pamoja na mbunge wa Thika Town Alice Ng’ang’a, walikuwa miongoni mwa washirika wa rais waliopigiwa kelele za kuzomewa hadharani.

Bw Ichung’wah alilalamikia utamaduni wa kuzomea viongozi hadharani katika eneo hilo, akisema unachochewa na viongozi wanaompinga rais na ajenda yake ya maendeleo.

“Tunaweka mikakati ya kukomesha kelele hizi na kuwasaidia wananchi wetu kuona fursa kubwa waliyonayo chini ya uongozi wa rais mwenye nia njema kwa taifa. Tutageuza kelele hizi kuwa sherehe,” alisema.

Hata hivyo, wachambuzi wametofautiana kuhusu iwapo kuzomewa kwa washirika wa rais mbele yake kunaashiria mwelekeo wa kisiasa katika eneo hilo na athari zake kwa kura zake kuelekea 2027.

Mwanahistoria na mchambuzi wa siasa Profesa Macharia Munene alisema kuwa ingawa tukio hilo linaweza kuhusishwa na siasa za Kiambu, kuna dalili kuwa lina mizizi mipana zaidi.

“Wapo watakaosema hili ni suala la Kiambu pekee. Lakini Bi Maina anatoka Murang’a. Hivyo, kuna mambo mengine zaidi yanayoendelea,” alisema.

Profesa Munene aliongeza kuwa kuna mwenendo unaokua ambapo viongozi wanaompinga aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua wanakumbana na uhasama kutoka umma.

Hali hiyo ilizidi kuchochewa na matamshi ya Bw Gachagua, aliyedokeza kuwa anachangia kuzomewa kwa washirika wa Rais William Ruto.

Akizungumza akiwa Kirinyaga, Bw Gachagua alisema aliwatelekeza wakazi wa Mlima Kenya kuruhusu mikutano ya rais kwa masharti ya kupata fedha na miradi ya maendeleo, huku akiwahimiza kupuuza viongozi anaowaita wasaliti wa kisiasa.

“Nimeanzisha operesheni ya kuwaondoa wasaliti wa kisiasa Mlima Kenya. Wote wanapaswa kuangushwa 2027. Tumsikize rais pekee lakini awe tayari pia kuondoka pamoja na washirika wake,” alisema.

Mbunge wa Laikipia Mashariki Mwangi Kiunjuri alikosoa kauli hizo, akizitaja kuwa za mgawanyiko na tishio kwa umoja wa kitaifa.

“Mwelekeo wa Bw Gachagua ni hatari. Anasambaza sumu ya kisiasa na kuchochea ukabila. Ni lazima akomeshwe,” alisema.

Mchambuzi wa siasa Gasper Odhiambo alimshauri Rais Ruto kutathmini upya mkakati wake katika eneo la Mlima Kenya, hasa viongozi anaowategemea.

“Kuna hali ya taharuki ndani ya timu ya rais. Badala ya kuwashawishi wananchi, wanawakabili, jambo lisilosaidia,” alisema.

Mchambuzi mwengine wa siasa Bw John Okumu alisema rais anapaswa kupitia upya washirika wake na kuwaondoa waliogeuka mzigo wa kisiasa.

Mwenyekiti wa Baraza la Wazee wa Kikuyu Wachira Kiago aliwataka wanasiasa kuwa waangalifu katika matamshi yao na kuepuka kauli zinazoweza kuwatenga wapigakura.

“Tangu 2024, mikakati imekuwa dhaifu. Uamuzi wa kuwaweka kando baadhi ya viongozi umepunguza nguvu aliyokuwa nayo 2022 alipopata asilimia 87 ya kura,” alisema.

“Lazima tuwe waangalifu. Wananchi tayari wamefanya maamuzi yao. Kuwachokoza hakutasaidia,” alisema.