Siasa

Gachagua: Mimi na Uhuru ndio tulileta Ruto, ni mimi nitamrudisha Sugoi

Na MWANGI MUIRURI February 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KINARA wa DCP Rigathi Gachagua ameapa kukusanya kura milioni nane kutoka Mlima Kenya ili kumkabili Rais William Ruto katika Uchaguzi Mkuu wa 2027.

Kulingana na Bw Gachagua, Rais Ruto aliibuka mshindi Mlima Kenya kwa msaada wake na akisisitiza kuwa yeye na Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta wanafaa kulaumiwa kwa kumgeuza Dkt Ruto kuwa kipenzi cha Mlima Kenya.

“Isingalikuwa ni Bw Kenyatta, nisingalimjua Bw Ruto na bila shaka nisingajikuta nikimfanyia kampeni ya urais 2022,” alihoji Bw Gachagua jana katika mahojiano na Inooro TV.

Aidha, alisema, “Kama Ruto hangaliniteua kama mgombea mwenza, hangalikuwa rais hii leo. Na anajua. Na kama haamini, acha akabili Mlima Kenya 2027. Hapo ndipo atajua wakazi wa Mlima na mnato halisi wa umaarufu wangu.”

Bw Gachagua alisema anajutia hadi leo hii “kuhusu mkasa pacha wa Bw Kenyatta kumtambulisha Bw Ruto kwetu Mlima Kenya na mimi binafsi kumfanya Rais 2022…”

Alisema, “Nina hatia ya kuwaeleza watu wa Mlima Kenya kumpigia kura Ruto 2022. Kenyatta ana hatia ya kumtambulisha Ruto kwetu 2013. Lakini Uhuru sasa amestaafu. Nitarekebisha makosa yote mawili ya Uhuru na yangu kuhusu Ruto 2027.”

Bw Gachagua alisema “mshawasha wangu sasa ni kuhakikisha tunawezesha sajili yetu kufikisha kura milioni nane na kuhakikisha tunapiga kura pamoja ifikapo 2027 kwa mwaniaji yeyote isipokuwa Dkt Ruto.”

Mnamo 2022, Bw Kenyatta alijaribu kuwaonya wakazi wa Mlima Kenya kutomuunga mkono Dkt Ruto.

Alisema alinuia kurekebisha kosa alilofanya 2022 lakini vilevile anataka lirekebishwe 2027.

Katika ziara yake majuzi eneo la Mlima Kenya, Rais Ruto alisema hana nia ya kubururwa katika “majibizano ya kikabilia yasiyo na ajenda yoyote ya maendeleo.

Alisisitiza Bw Kenyatta alimtambulisha Mlima Kenya 2013 lakini Bw Gachagua hakumsaidia 2022, akiapa kusalia Mlima Kenya.