Hatutakunyang’anya kiti chako, Oburu aambia Kindiki
KAULI ya Kinara wa ODM, Dkt Oburu Oginga kuwa Naibu wa Rais Prof Kithure Kindiki hafai kuingiwa na wasiwasi kuwa wananyemelea wadhifa wake imezua mjadala kuwa chama hicho kitapewa makombo katika muafaka wake na UDA kuelekea katika uchaguzi mkuu wa 2027.
Dkt Oginga jana alimtaka Prof Kindiki kutoingiwa na wasiwasi kuwa wadhifa wake unapiganiwa na ODM huku akisema Naibu wa Rais ni rafiki wa chama hicho.
“Lakini Naibu Rais usifikirie kuwa tunataka kiti chako na kuwa tunataka kukufukuza. Wewe ni rafiki yetu,” akasema Dkt Oginga.
Seneta huyo wa Siaya alizungumza hayo mbele ya Rais William Ruto na Prof Kindiki jijini Kisumu, ngome ya kisiasa ya ODM.
Rais Ruto, Prof Kindiki na viongozi kadhaa serikalini walifika jijini Kisumu kusambaza pesa za vijana kupitia mradi wa Nyota.
Pesa zilizotolewa jana ni za kaunti za Kisumu, Homa Bay na Siaya.
Dkt Oginga, hata hivyo alisisitiza kuwa ODM itazungumza na UDA ili ipate sehemu ya serikali wala si mgao wa mtu yeyote.
“Tutazungumza na UDA na tutahakikisha kuwa tunapata mengi kuliko kile tulichonacho kwa sasa. Tulipata wizara hizi muhimu -ya Kawi na Fedha- ambazo ni kiini cha serikali kwani mojawapo huhusu mipango ya pesa,” akaongeza Dkt Oginga.
“(Samuel) Atandi Meli (Mbunge wa Alego Usonga) pia ni mwenyekiti wa kamati ya bajeti bungeni. Tunapoendelea hatutakubali kupewa kidogo na tutazunguza kupata kile ambacho chama chetu kinastahili,” akasema Dkt Oginga.
Dkt Oburu alizungumza hayo, siku moja baada ya Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga ambaye pia ni mwenyekiti wa ODM kusema kuwa chama hicho kitalenga kupewa nusu ya serikali katika mazungumzo ya kubuni muungano yanayoendelea.
“Tuko katika mazungumzo na UDA ila hatutalegeza kamba katika juhudi zetu za kupata ‘nusu mkate’ ya serikali,” alisema akiwa Nairobi mnamo Jumapili.
Dkt Oginga, nduguye marehemu Waziri Mkuu wa zamani Raila Odinga alisema ODM si chama cha kikabila hasa Waluo na kuongeza kuwa kitashiriki mazungumzo kwa nia ya kuzima ukabila.
“Hiki si chama cha Waluo na hatutaki vyama vya kikabila. Tutahakikisha kuwa kila mtu anapata haki yake kwenye mgao wa taifa,” akasema.
Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi wikendi alikuwa ameeleza Taifa Leo kuwa ana imani ODM ina viongozi ambao wamehitimu wanaoweza kuwasilishwa kama wagombeaji wa urais.
Matamshi hayo yanaenda kinyume na kauli ya Dkt Oginga aliyotoa mnamo Novemba mwaka jana kuwa ODM haiwezi kukubali wadhifa wa chini ya naibu rais.
Kwenye mahojiano ya awali na Dkt Oginga, alisema chama hicho kina umaarufu mkubwa maeneo mbalimbali nchini na katika ushirikiano wowote wa kisiasa wakikosa urais basi hawawezi kukubali chini ya wadhifa wa mgombeaji mwenza.
Mnamo Januari 20 akikutana na wajumbe wa ODM katika Kaunti ya Kakamega, baadhi ya wabunge walimwambia Dkt Oginga asikubali wadhifa wa chini ya unaibu rais katika mazungumzo na UDA.
“ODM ina historia, ufuasi na sura ya kitaifa. Kwa hivyo, tunapozungumza na UDA, usikubali chini ya wadhifa wa naibu rais,” akasema Mbunge wa Ikolomani, Bernard Shinali kwenye mkutano huo wa wajumbe.
Jana wakazi wa Kisumu waliidhinisha mazungumzo kati ya ODM na UDA wakiahidi kuwa 2027 wataunga mkono azma ya kuchaguliwa tena kwa Rais Ruto.
Kiongozi wa nchi naye alitumia hafla hiyo kukashifu upinzani kama wasiokuwa na ajenda akiahidi kuwa Nyanza haitakuwa upinzani tena.
“Wako upinzani na hawana namna au mipango ya kuwasaidia wananchi. Leteni mapendekezo yenu ya kuboresha nchi hata mnapokosoa serikali,” akasema Rais Ruto.
Profesa Kindiki naye alimsifu Rais Ruto kama kiongozi mchapakazi akisema ushirikiano wa UDA na ODM utafanya serikali kuwa imara.