Hiki kiti hamkipati, najua nitakuwa Naibu Rais hadi 2032, Kindiki ajibu ODM
NAIBU Rais Profesa Kithure Kindiki amesema hatetereshwi na mjadala unaoendelea kuhusu wadhifa wake akisema binafsi yeye si mtu wa kutishwa na siasa za ubabe akisisitiza kwamba kiti chake kitasalia Mlima Kenya 2027.
Profesa Kindiki amesema kuwa kwa sasa kazi yake kuu ni kumsaidia Rais William Ruto kutimiza malengo yake kimaendeleo huku akiwaambia wafuasi wake kuwa atahudumu kama naibu rais hadi 2032 kisha ajipange ‘hapo mbele’.
“Nimesikia watu wameleta wasiwasi huku na ninawauliza kwa hii serikali mnajua mimi ndiye nambari mbili? Nasikia kuna watu wanaongea lakini nawaambia msiletewe wasiwasi na mambo madogo madogo ambayo watu wanaongea,” akasema Profesa Kindiki akiwa Kaunti ya Meru.
“Mimi ndiye naibu rais na hiki kiti hakuna mahali kinaenda. Unajua mimi nimekuwa kwa siasa kwa muda na mwanasiasa mzuri anajua siku ya kuongea na siku ya kunyamaza,” akaongeza.
Tamko hilo lilionekana kumlenga Kinara wa ODM Dkt Oburu Oginga ambaye Jumatano wiki jana alisema chama hicho kinalenga wadhifa huo kinapoendelea kujadiliana na UDA.
Profesa Kindiki hasa analenga kuletea Rais zaidi ya kura milioni moja za Mlima Kenya Mashariki na shinikizo za ODM zimesababisha wasiwasi kuwa huenda akakosa kuwa mgombeaji wa rais mnamo 2027.
“Ukiwa mwanasiasa unaongea kila siku basi huna akili. Kuna siku ya kupiga siasa na siku ya kupiga kazi, kitu kitatusaidia ni kufanya maendeleo kwa watu wetu,” akasema.
Kauli yake ilikuja baada ya baadhi ya viongozi kutoka Ukanda wa Mlima Kenya kutangaza Jumamosi kuwa wataondoka serikalini iwapo Profesa Kindiki hatakuwa mgombeaji mwenza wa Rais Ruto.
Aidha, wakati ambapo Rais Ruto alikuwa Kisumu mapema mwezi huu kusambaza pesa kupitia Mradi wa NYOTA, Dkt Oginga alimwambia Profesa Kindiki asiwe na wasiwasi kwa sababu ODM haindei kiti chake.
Hata hivyo, kinara huyo wa ODM anaonekana alighairi nia wikendi akiwa Pwani baada ya kusema kuwa wanalenga unaibu rais kwenye muafaka na Rais Ruto.
“Wale unasikia wakiongea wasiwatie wasiwasi. Sisi ndio mafundi wa siasa. Mkiniangalia mnaona mtu ambaye anaweza kutishwa? Tusifanye siasa ya kuonyeshana madharau,” akasema.
Wakati wa ziara hiyo Profesa Kindiki aliahidi ujenzi wa Daraja la Nithi akitaja kujengwa kwa Hospitali ya Meru na barabara kadhaa Imenti kama baadhi ya ahadi ambazo zimetimizwa na serikali.
Profesa Kindiki kando na kupambana asalie mgombeaji mwenza wa Rais Ruto pia anapambana kuhakikisha rais anapata kura za Mlima Kenya Magharibi anakotoka hasimu wake aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua.