Siasa

‘Jicho Pevu’ aogelea kivyake akipambana kunasa ugavana Mombasa

Na WINNIE ATIENO February 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HUKU wanasiasa wa eneo la Pwani wakimpigia debe Rais William Ruto kushinda awamu ya pili ya uongozi, mbunge wa Nyali, Bw Mohammed Ali, ameamua kufuata upinzani.

Kwa miezi kadha tangu amalize matibabu baada ya kuvunjika mguu, Bw Ali amejitokeza wazi kupinga serikali, akishirikiana na upande wa upinzani unaoongozwa na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua na kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka.

Vilevile, mbunge huyo almaarufu ‘Jicho Pevu’ anayehudumu awamu ya pili mamlakani, amesema pia anashirikiana na vuguvugu la viongozi vijana akiwemo mbunge wa Embakasi Mashariki, Bw Babu Owino.

Kulingana naye, lengo lake ni kuungana na viongozi wanaotaka kukomboa Mombasa kutoka kwa utawala mbaya.

“Viongozi wetu ni wa kuleta leso, madera na pakiti za unga. Endeleeni kuzipokea kwa sababu ni mali yenu ya umma. Kuleni hivyo vitu wanavyowaletea lakini kura mnipe mimi,” alisema Bw Ali ambaye amepanga kuwania kiti cha ugavana Mombasa.

Mbunge huyo ambaye alichaguliwa katika awamu ya pili kupitia Chama cha UDA alisema ni sharti viongozi wazingatie siasa za maendeleo badala ya kufuata vigogo wa maeneo.

Msimamo wake wa kukaidi mwelekeo unaochukuliwa na wanasiasa wengi Mombasa au Pwani kwa jumla si jambo geni.

Mnamo mwaka wa 2017, alishinda ubunge wa Nyali kwa mara ya kwanza kama mgombea huru, akilalamikia kunyimwa tikiti katika chama cha ODM.

“Baba alikuwa ananipenda sana, lakini nyinyi ambao mlininyanganya tikiti, nikaondoka ODM mlimtumia vibaya sana. Sasa hayuko, tukutane debeni 2027. Enzi ya majigambo ya ukubwa wa kisiasa imekwisha,” alisema.

Alishinda ubunge licha ya kuambiwa kwamba Mombasa ni ngome ya ODM, suala ambalo lilirejelewa tena 2022 alipotumia tikiti ya UDA ambacho kilikuwa chama kipya kikiongozwa na Rais William Ruto.

Wakati huu, anapomezea mate nafasi ya ugavana Mombasa, anakumbwa na upinzani kutoka pande mbalimbali.

Hivi majuzi, Bw Gachagua alifichua kuwa, viongozi wa upinzani watamuunga mkono kwa pamoja na wataamua chama ambacho atatumia, kati ya chama chake cha DCP na Wiper.

Suala ibuka ni iwapo msururu wa ushindi ambao amekuwa akipata licha ya misimamo yake mikali ya kisiasa utaendelea kushuhudiwa 2027.

Kwa mujibu wa Bw Ali, siasa za Pwani zimeshamiri sarakasi badala ya utoaji wa huduma na maendeleo.

Akielezea sababu za kujitenga na wenzake, alisema, “Simba hatembei na kondoo, na jogoo hatembei na vifaranga,” akihalalisha kutohudhuria vikao vya viongozi wa Pwani ambao hivi karibuni walitangaza kumuunga mkono Rais na Bw Joho.

Mbunge huyo anaamini kwamba maendeleo aliyoleta katika eneobunge la Nyali pamoja na uongozi wa uaminifu aliodhihirisha utachangia kumsaidia katika kampeni zake.

“Tangu uhuru, viongozi wetu hawajawahi kuwekeza katika elimu. Waliwekeza katika anasa. Badala ya kuwapeleka watoto wa maskini shuleni ili wabadilishe maisha yao na kuketi kwenye meza ya ajira pamoja na watoto wa matajiri, waliamua kuwaletea dera, leso na pakiti za unga ili kuua kizazi chenu,” alisema.

Amesema aliposhinda ubunge mnamo 2017, eneobunge la Nyali lilikuwa na shule moja tu ya upili ya umma.

“Leo, Nyali ina zaidi ya shule 15, zikiwemo Mwembeni, Kongowea, Kengeleni na Pentrose,” alisema.