Kalonzo na Wamalwa wadai kuna njama ya kumtia pingu Gachagua
VIONGOZI wa upinzani jana walidai kuwa kuna mpango wa kumkamata aliyekuwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua na kumfikisha kortini.
Wakiongea katika Kaunti ya Murang’a jana, wanasiasa wa muungano wa upinzani walidai Bw Gachagua analengwa ili kuzima siasa zake kali na kulemaza umaarufu wake Mlima Kenya.
Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka na Mwenzake wa DAP Eugene Wamalwa walisema iwapo masaibu hayo yatamfika Bw Gachagua, watasimama naye jinsi walivyofanya alipotimuliwa uongozini Oktoba 2024.
Wawili hao jana waliungana na Bw Gachagua katika Kanisa Katoliki la Kahuro ambapo halafu walihutubia mikutano ya umma.
Akiongea katika Kaunti ya Kericho mnamo Jumamosi, Seneta wa Kericho Aaron Cheruiyot alimtaka aliyekuwa naibu rais aanze kuzoea maisha ya gerezani.
“Namwambia aanze kuzoea sare ya gerezani kwa sababu ni muda tu kabla afike huko,” akasema Bw Cheruiyot.
Bw Musyoka alidai mpango wa kumnyaka Bw Gachagua unasukwa ili kuridhisha eneo la Nyanza ambalo serikali kwa sasa inasaka uungwaji mkono.
“Mimi najua watu wa Nyanza baada ya kufanya kazi na Raila kwa kipindi kirefu. Hawatakupigia kura kwa sababu ya nafsi zao.”
“Baada ya kumwondoa Bw Gachagua serikalini kwa njia haramu, sasa unapanga kumkamata. Hakuna njia utakayotumia kumnyamazisha Bw Gachagua,” akasema Bw Musyoka.
Bw Wamalwa naye alimwambia Rais ajiandae kwa athari hasi iwapo Bw Gachagua atanyakwa huku wakiahidi kusimama naye katika hali zote.
“Tunajua hesabu zako mbaya na huwezi kufanya zitimie kwa kutishia upinzani. Ukimnyaka Gachagua, matatizo yako yataongezeka kuliko yalivyo kwa sasa,” akasema Bw Wamalwa.
Bw Gachagua naye aliwataka wafuasi wake wakae ange, akidai Rais Ruto ni mwanasiasa katili anayeweza kufanya chochote ili kutimiza maslahi yake ya kisiasa.