Siasa

Kati ya Uhuru, Gachagua na Ruto nani ndiye mwenye Mlima?

Na JUSTUS OCHIENG March 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS mstaafu Uhuru Kenyatta amejikuta tena katika mizunguko ya kisiasa ya Mlima Kenya, huku kuharibika kwa uhusiano kati ya aliyekuwa naibu rais Rigathi Gachagua na Rais William Ruto kukipanga upya ushawishi wa eneo hili kuelekea uchaguzi wa mwaka 2027.

Tangu alipotofautiana na Rais Ruto, Gachagua amejitambulisha kama kiongozi mahiri wa kuvutia wapiga-kura, viongozi na wanamaoni chini ya kauli kwamba eneo la Mlima linakandamizwa kisiasa na kiuchumi.

Huku mzunguko wa uchaguzi wa 2027 unavyoanza kukamilika, eneo hili limejikuta katikati ya mvutano wa pande tatu kati ya Rais Ruto, Gachagua, na Kenyatta.

Viongozi wa eneo hilo wanasema mabadiliko haya yanaonyesha mkakati wa kisiasa.

Mfano dhahiri ni Jeremiah Kioni, aliyekuwa mwaminifu kwa Kenyatta lakini hivi karibuni akaonekana kurudi upande wa Gachagua.

Wiki iliyopita, Kioni alifanya mazungumzo na Gachagua. Ingawa alikanusha kumtema Rais Mstaafu, wachanganuzi wanasema kuvuliwa wadhifa wa katibu mkuu wa Jubilee kulimfanya afikirie upya nafasi yake ya kisiasa.

Gachagua, kiongozi wa DCP, anaendelea kujitambulisha kama mtetezi wa kweli wa maslahi ya kisiasa na kiuchumi ya Mlima Kenya, huku akikabiliana na ushindani wa ndani kutoka kwa Prof Kithure Kindiki na shinikizo kutoka kwa wabunge wanaomuunga Ruto.

Kwa upande mwingine, Kenyatta anaendelea kujenga ushawishi kupitia mazungumzo ya siri, kuunda makubaliano ya kipekee na kuimarisha uhusiano na upinzani.

Hali hii imesababisha baadhi ya viongozi wa eneo hilo, kama vile Wambugu Ngunjiri (Nyeri Town) na Kimani Ngunjiri (Bahati), kurejea katika kambi ya Kenyatta baada ya kuungana na Gachagua kwa muda.

Vilevile, Kanini Kega (Kieni) amejiunga na DCP.

Martha Karua, kiongozi wa PLP, ambaye katika uchaguzi mkuu wa 2022 alikuwa mgombea mwenza wa Azimio la Umoja ametangaza kushirikiana na Gachagua kupitia muungano wa upinzani, jambo ambalo ni ishara ya mabadiliko kisiasa.

Wengine, kama Anne Waiguru (Kirinyaga) na Sabina Chege (Mbunge Maalum), wamebaki katika kambi ya Ruto, wakiwakilisha viongozi wanaoona manufaa ya kuendelea kuunga Rais wa sasa.

Mchambuzi wa siasa Chris Omore anasema, “Hali hii inaonyesha eneo la Mlima Kenya ni uwanja unaobadilika ambapo makubaliano hupimwa, kuachwa, na kujengwa upya.”

Uchaguzi mkuu wa 2027 unavyokaribia, uaminifu unaobadilika kati ya Gachagua, Kenyatta, na Ruto huenda usiamue tu mwelekeo wa kisiasa wa Mlima Kenya bali hata mustakabali wa taifa.

Kwa sasa, hakuna mmoja kati yao anayeweza kudai mamlaka kamili, hali inayoibua wasiwasi pamoja na fursa.

“Swali kuu sio kama Mlima Kenya kutakuwa na mshikamano, bali utaunganishwa na nani na kwa gharama gani,” anasema Mokua.