Siasa

Kibarua kwa Kindiki, Gachagua akionekana ‘kuondoka’ na Mlima Kenya Mashariki

Na CECIL ODONGO June 24th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

ALIYEKUWA Naibu Rais Profesa Kithure Kindiki na wabunge kutoka ukanda wa Mlima Kenya Mashariki, wana kibarua kigumu cha kumhakikishia Rais William Ruto uungwaji mkono huku aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua akionekana kuteka eneo hilo kisiasa.

Kuanzia Ijumaa mpaka Jumapili, Bw Gachagua aliendeleza misururu ya mikutano ya umma ambapo alipokolewa vizuri na kumtaja Rais Ruto kama aliyetelekeza eneo hilo kisiasa.

“Mimi sikujua Rais Ruto atanitumia kupata kura zetu kisha anifukuze serikalini. Sasa anawatumia wabunge wenu, baadhi ambao mimi nilikuwa na ushawishi katika kuchaguliwa kwao kunipiga vita,” akasema Bw Gachagua katika eneobunge la Buuri.

Aidha Bw Gachagua alitaja kutotekelezwa kwa ahadi ya kufaulisha miradi mbalimbali ya serikali hasa sekta ya kilimo cha miraa na mingine ambayo walikubaliana.

Huku mrengo wa serikali ukiwa na uungwaji mkono wa wabunge wote wa Meru na Tharaka-Nithi, Bw Gachagua anajivunia uungwaji mkono wa aliyekuwa Seneta wa Meru na Waziri wa Kilimo Mithika Linturi pamoja na chama cha DEP almaarufu Bus chake Kiraitu Murungi na aliyekuwa Seneta wa Embu Lenny Kivuti.

DEP kupitia Bw Kivuti ilisema wiki jana kuwa inaegemea mrengo wa Bw Gachagua na itamsaidia kuhakikisha Rais Ruto anahudumu muhula moja pekee.

Kwa kuwa Profesa Kindiki anatoka eneo la Mlima Kenya Mashariki, ana kibarua cha kuhakikisha anamvunia Rais uungwaji mkono eneo hilo ili kudumisha nafasi ya mgombeaji mwenza.

“Rais akishatoka, Nitarudi hapa kupambana na watu hawa waliojaa kiburi na wanaendesha siasa za chuki,” akasema Profesa Kindiki mjini Meru baada ya mkutano wa Bw Gachagua.

Kulingana na mdadisi wa masuala ya kisiasa Martin Andati, mikutano ya Bw Gachagua na mapokezi aliyoyapata, inaonyesha Profesa Kindiki ana kibarua kumvunia Rais uto kura eneo hilo.

“Itakuwa vigumu sana kwa Profesa Kindiki kuweka eneo la Meru nyuma ya Rais ikizingatiwa wamekuwa wakipiga kura na wenzao kutoka Mlima Kenya Magharibi na pia utendakazi usioridhisha wa serikali,” akasema Bw Andati.

“Pia upande wa Bw Gachagua unatumia uwezekano wa unaibu rais kutoenda eneo hilo 2027 kumpiga vita Rais na Profesa Kindiki,” akaongeza Bw Andati.