Siasa

Kimeumana ODM Sifuna akipokewa kishujaa, Oburu akisema kundi lake ndilo lina roho ya Raila

Na STANLEY NGOTHO, BRIAN OCHARO February 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

UBABE na tofauti kali za kisiasa jana ziliendelea kuandama ODM huku mkutano ulioandaliwa Kitengela, Kaunti ya Kajiado na viongozi waasi wa chama ukitibuliwa na maafisa wa usalama.

Kinara wa ODM Dkt Oburu Oginga aliwaongoza wanasiasa wanaoegemea mrengo wake katika mkutano mkubwa wa kisiasa uwanja wa Tononoka eneobunge la Mvita jijini Mombasa.

Kwa upande mwingine, akthari ya wafuasi wa ODM walifurika mjini Kitengela kwenye mkutano uliosheheni ghasia. Mkutano huo ulihudhuriwa na Katibu Mkuu wa chama anayekabiliwa na utata Edwin Sifuna pamoja na kundi la viongozi waasi wa ODM na baadhi kutoka upinzani.

Mkutano wa Kitengela ulikuja baada ya Bw Sifuna kuondolewa kama katibu mkuu wiki jana lakini akapata faraja ya muda kortini.

Jijini Mombasa, Dkt Oginga alijitosa kwenye mjadala wa kutimuliwa kwa Bw Sifuna akisema Katibu Mkuu anayetambuliwa na chama ni Mbunge Mwakilishi wa Kaunti ya Busia Catherine Omanyo.

“Sisi katibu wetu mkuu ni Bi Omanyo kwa sababu uamuzi ulifanywa kuwa aliyekuwa katibu wetu akae nje kutokana na utovu wa nidhamu. Hatujamfukuza kutoka kwa chama ila wadhifa wake ndio tumempokonya,” akasema Dkt Oginga.

Alikuwa akizungumza katika ibada ya Kanisa la Shalom. Dkt Oginga alisema sheria za chama lazima zifuatwe na wote na wale ambao wanakosa kuziheshimu lazima waadhibiwe.

“Suala la Sifuna tumelimaliza na ukikosea lazima uadhibiwe wala chama hakiwezi kuongozwa na uoga wa kukutimua. Hakuna mtu ambaye hawezi kuadhibiwa na chama akiwemo mimi,” akaongeza Dkt Oginga, nduguye marehemu Kinara wa chama hicho Raila Odinga.

“Nikikosa heshima basi lazima nifurushwe chamani. Hakuna mtu ambaye ni mkubwa kuliko chama kwa sababu chama kinabuniwa kwa sababu ya watu. Hakuna mtu ambaye ataogopwa au kufikiria yuko juu ya sheria ODM,” akasema seneta huyo wa Siaya.

Mwenyekiti wa ODM Gladys Wanga naye alisema chama kitaendelea kusimamia falsafa ya uongozi wa Raila na kuwatetea Wapwani.

Kinara wa ODM Oburu Oginga akiwasili uwanja wa Tononoka na Gavana wa Mombasa Abdulswamad Nassir Februari 15, 2026 kwa mkutano wa Linda Ground. Picha|Hisani

“Raila hakuwa akifanya chochote bila kushauriana na Dkt Oburu ndiyo maana tunajua kiongozi wetu wa sasa hawezi kutuelekeza vibaya,” akasema akiwataka viongozi kutoka Pwani waendelee kuwa nyuma ya ODM.

Dkt Oginga na viongozi wanaounga mkono Serikali Jumuishi wamekuwa wakiongoza mrengo wa Linda Ground, kampeni inayolenga kuhakikisha ODM inalinda ngome yake ya kisiasa.

Kitengela nako kuligeuka uwanja wa vitoza machozi, polisi wakiwafurusha wafuasi wa Linda Wananchi ambao walikuwa wahutubiwe na Bw Sifuna na wenzake.

Awali katika ibada ya kanisa, baadhi ya waliohudhuria na kuendelea kukosoa uongozi wa Dkt Oburu ODM ni Gavana wa Siaya James Orengo, Seneta wa Vihiga Osotsi Atsieno, wabunge Babu Owino (Embakasi Mashariki), Caleb Amisi (Saboti), Anthony Kibagendi (Kitutu Chache Kusini), Oundo Ojiambo (Funyula), Joshua Kimilu (Kaiti) na Seneta wa Kisii Richard Onyonka.

Ghasia zilianza baada ya Bw Sifuna kupewa mapokezi ya shujaa mjini Kitengela. Umati huo ulionekana kulemea polisi huku baadhi ya vijana wakiwarushia polisi mawe.

Watu kadhaa walijeruhiwa polisi walipowakabili vijana hawa huku Bw Sifuna na viongozi wenzake wakitimka mbio na kuenda zao.

“Hata wakinimaliza leo, najua kuna zaidi ya watu milioni 15 ambao najua wataendeleza uanaharakati huu. Waliharibu jukwaa letu asubuhi pamoja na vipaza sauti na sasa wametibua mkutano wetu, bado tutaendelea kupambana,” akasema Bw Sifuna.

Bw Orengo naye alivamia Dkt Oginga akidai chama ‘kimeuzwa’ kwa Rais Ruto lakini akasisitiza ataendelea kwenye mkondo wa mapambano.

“Hili vuguvugu letu halihusiani na 2027 bali ni la kukomboa taifa sasa. Ni waoga tu ndio watawazima wanasiasa wanaochipuka na mrengo huu wa Sifuna ndio utaleta mabadiliko kwa nchi,” akasema Gavana Orengo.

Bw Owino alisema hata kama mkutano wao umesambaratishwa, bado wataendelea kuwafikia vijana na wanawake kuhusu kura ya 2027.

“Oburu Odinga na wenzake huenda wana nguzo za chama lakini sisi tuna wanachama na wafahamu hatutayumbishwa na uoga. Wanauza chama chetu lakini hatutakuwa sehemu ya mpango huo,” akasema Bw Owino.

Mbunge wa Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA) Winnie Odinga, mwanawe Raila hakuwa Kitengela katika mkutano ambao ulihudhuriwa na zaidi ya wabunge 20 na madiwani wa Bunge la kaunti mbalimbali.

Jana taharuki ilitanda Kitengela huku polisi polisi wakiwafurusha baadhi ya vijana waliodaiwa walisafirishwa kutoka Ongata Rongai kutibua mkutano huo.

Watu wasiojulikana pia waliondoa bango lililokuwa na picha za viongozi wa vuguvugu la Linda Mwananchi kwenye mzunguko wa barabara ya Mombasa.