Kombora la Gachagua kwa Ruto
ALIYEKUWA Naibu Rais Rigathi Gachagua amedai kuwa vifo, uharibifu na ghasia zilizotokea wakati wa maandamano ya Jumatano zilipangwa na kufadhiliwa na Serikali.
Aidha, alimhusisha Rais William Ruto na uvamizi katika shamba la aliyekuwa Rais Uhuru Kenyatta mnamo Machi 2023 na kisha akaondoka nchini ili yeye (Gachagua) alaumiwe.
“Hakuna mtu anayeweza kugusa mali ya Uhuru Kenyatta – iwe shamba, usalama au nyumba – bila idhini ya Rais. Yeye (Ruto) ndiye alitoa agizo hilo na kisha akasafiri nje ya nchi ili ionekane kana kwamba sisi ndio tulihusika,” alidai Gachagua.
Maandamano ya Jumatano yaliyoandaliwa kuadhimisha mwaka mmoja tangu ghasia za Juni 25 2024 – ambapo vijana wa kizazi cha Gen Z walivamia bunge – yalisababisha vifo vya watu 16, zaidi ya 400 kujeruhiwa, na biashara nyingi kuporwa au kuharibiwa.
Hata hivyo, baada ya hali kutulia, vidole vya lawama vilielekezwa kwa Bw Gachagua, viongozi wanaounga serikali wakidai alifadhili magenge ya wahuni kuingilia maandamano ya amani kwa maslahi ya kisiasa.
Akizungumza katika mahojiano maalumu na runinga ya NTV, Bw Gachagua alikanusha madai hayo na badala yake akaishutumu Serikali, Rais William Ruto, na Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen kwa kupanga njama hiyo.
Alidai wahuni waliovuruga maandamano waliletwa na Serikali kwa pikipiki ili kuharibu jina la waandamanaji na kuzua hofu.
“Hawa Gen Z hawakuwa na vurugu. Vurugu zililetwa na watu waliolipwa, waliotumia pikipiki. Kama kweli wangekuwa wangu, wangekuwa wamepigwa risasi au kukamatwa na kuhojiwa,” alisema Gachagua.
Alihoji ni vipi vituo vya polisi vinavyolindwa kwa silaha viliweza kuvamiwa na waandamanaji wasio na silaha, akisema polisi walishirikiana na wahuni hao.
“Ni wazi kuwa baadhi ya polisi waliwaongoza na hata kuwaruhusu kuingia na kuchoma vituo vya polisi,” aliongeza.
Bw Gachagua alieleza kuwa mkakati huo ulipangwa na Murkomen kwa lengo la kupaka tope viongozi wanaopendwa katika eneo la Mlima Kenya, na kuongeza kuwa, hakuna afisa yeyote wa polisi aliyekamatwa kwa kuhusika na mauaji ya waandamanaji.
Alimtaja Murkomen kama “waziri chipukizi aliyepagawa na mamlaka” na kufichua kuwa, alipinga uteuzi wake kama Waziri wa Usalama wa Ndani.
“Nilitaka mtu mtulivu, mwenye busara, sio mtu anayependa makuu. Polisi hawapaswi kupiga risasi raia wanaoingia katika vituo vya polisi – ni taasisi za umma. Ukigundua mtu ana nia mbaya, mkamate, si kumuua,” alisema.
Aliendelea kushambulia Murkomen kwa agizo la ‘piga risasi uue’ dhidi ya waandamanaji, akisema ni agizo la kikatili lisilopaswa kufuatwa.
“Murkomen ni kijana mdogo anayependa pesa na mamlaka. Ukifuata maagizo yake haramu, utajikuta peke yako ukiadhibiwa. Awaagize kwa maandishi,” alisema Gachagua.
Alidai kuwa, maafisa wa vyeo vya juu waliotoa maagizo ya mauaji bado wako huru, ilhali wale wa chini wanazuiliwa.
Alipoulizwa kwa nini hakujiunga na waandamanaji, alisema alikuwa nyumbani akiangalia kwa mbali, akiheshimu wito wa Gen Z kwamba wanasiasa wasijihusishe.
“Gen Z ni vijana werevu mno. Wana akili timamu na najivunia kuwaunga mkono. Walipouawa, kunyanyaswa na kuitwa wahalifu na Rais Ruto, nilikuwa mmoja wa viongozi wachache waliowatetea hadharani, hata kwa kuhatarisha kazi yangu,” alisema.
Pia, alikanusha kuwa anafadhili maandamano hayo, akisema Gen Z hawana kiongozi, hawana muundo, na hawahitaji wafadhili wa kisiasa.
Alilaani hatua ya serikali ya kumpokonya walinzi Jaji Mkuu (mstaafu) David Maraga kwa kuunga vijana wa Gen -Z, akisema ni hatua ya ‘kipuuzi na ya kisasi.’
Aidha, alisema kuwa jitihada za Rais Ruto kuleta mgawanyiko miongoni mwa viongozi wa Mlima Kenya hazitafaulu.
“Watu wa Mlima sasa wamefunguka macho. Tulilishwa porojo hadi tukamgeuka Uhuru. Lakini sasa hawatadanganywa tena,” alisema.
Alikanusha kuwa yeye ni kiongozi wa kikabila, akisema chama chake cha Democracy for Citizens Party kina viongozi kutoka maeneo mbalimbali nchini.
“Mimi si kiongozi wa ukabila. Na hata nikiwaita watu ‘binamu’ siyo ukabila – ni njia ya kuunganisha Wakenya,” alisema, akiongeza kuwa, jamii nyingi zina uhusiano wa kifamilia wa kihistoria.
Kuhusu madai ya mapinduzi ya serikali, Gachagua alisema: “Sijawahi kushinikiza Rais Ruto aondolewe kwa njia isiyo halali. Nataka tu ang’olewe kwa njia ya kidemokrasia kupitia kura.”
Akasema: “Wakenya wameamua kuwa atakuwa ‘Wantam’ (muhula mmoja). Aondoke kwa heshima ama asubiri wananchi wamfurushe kwa kura.”
Alikosoa vikali hatua ya serikali kuzima matangazo ya moja kwa moja ya maandamano, akisema ilikuwa mbinu ya kuficha ukweli.
“Sijawahi kuwa adui wa vyombo vya habari. Mimi ni zao la vyombo vya habari. Kuzima matangazo ni ukatili dhidi ya uhuru wa habari. Demokrasia yoyote ya kweli inaheshimu haki ya wananchi kupata habari,” alisema.
Alimalizia kwa kusema: “Ruto asirudishe nchi hii kwenye enzi za zamani za giza ambapo watu waliteswa kwa kusema ukweli.”
Gachagua alikuwa akijibu wito wa wabunge wa Kenya Kwanza na ODM waliataka akamatwe wakidai ndiye kiini cha uporaji uliogubika maandamano ya GenZ, Jumatano.
Wabunge hao wanaojumuisha Didimus Barasa (Kimilili), Mark Nyamita (uriri), Japheth Nyakundi (Kitutu Chache) Ali Wario (Bura) na waakilishi wanawake Lilian Sioi (Trans Nzoia), na Fatuma Mohammed (Migori) walimshutumu Bw Gachagua kwa kutumia magenge ya wahuni kushinikiza siasa za kikabila Mlima Kenya.
“Tunataka aliyekuwa naibu rais akakamatwe. Amenukuliwa akichochea vita na vijana wetu dhidi ya wanaokataa kufuata mtazamo wake wa siasa duni,” alisema Bw Barasa.