Siasa

Kundi la Sifuna laongeza kasi, lapokelewa Mombasa na umati mkubwa

Na BRIAN OCHARO March 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

VIONGOZI wa mrengo wa Linda Mwananchi waliongeza kasi ya kampeni zao kisiasa kwa kuzuru jijini Mombasa, wakisisitiza kuwa kujitenga kwao na chama cha Orange Democratic Movement (ODM) hakuwezi kuzuilika.

Viongozi hao walidai kwamba hatua hiyo inalenga kurejesha misingi na maadili ya awali ya chama hicho.

Katika ziara hiyo ya Pwani, viongozi hao walivutia umati katika viwanja vya Tononoka kueleza msimamo wao na kukosoa vikali uongozi wa sasa wa ODM pamoja na serikali ya kitaifa.

Gavana wa Siaya James Orengo na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna walidai kuwa msingi halisi wa kisiasa wa ODM sasa imo ndani ya mrengo wa Linda Mwananchi.

Walisema kundi linalohusishwa na kiongozi wa sasa wa ODM, Oburu Oginga, halina msingi thabiti wa kisiasa wala uungwaji mkono wa wananchi.

Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi alithibitisha kuwa hatapeleka kesi mahakamani kupinga kuondolewa kwake kama Naibu Kiongozi wa ODM.

Badala yake, alitangaza kujiunga rasmi na vuguvugu hilo jipya.

“Sitaenda mahakamani kupinga kuondolewa kwangu. Nimeamua kuachilia. Kuanzia leo mimi ni Naibu Kiongozi wa Linda Mwananchi,” alisema.

Bw Osotsi aliwashutumu wapinzani wao kwa kutumia fedha kununua viongozi wa kisiasa kuwaunga mkono, lakini akasema wananchi hawawezi kununuliwa.

“Unaweza kununua wabunge, lakini hauwezi kununua wapiga kura,” alisema.

Kwa upande wake, Bw Sifuna alihoji uhalali wa ODM kumuondoa Osotsi, akisema kuwa aliteuliwa katika nafasi hiyo na kiongozi wa zamani wa chama hicho Raila Odinga.

“Osotsi aliteuliwa na Raila Odinga mwenyewe. Ni nani sasa ana mamlaka ya kumuondoa?” aliuliza.

Sifuna, ambaye bado anashikilia wadhifa wa Katibu Mkuu wa ODM, alisisitiza kuwa hatambui chama hicho bila uwepo wa Raila Odinga.

“Mimi sitambui ODM bila Raila Odinga. Siwezi kuhudumu kama Katibu Mkuu wa chama kilichopoteza mwelekeo,” alisema.

Aliendelea kusema kuwa hawezi kuhudumu chini ya uongozi wa sasa, akimtaka Oburu Oginga kuteua mtu mwingine kushika wadhifa huo.

“Nimehudumu chini ya Raila kwa miaka tisa. Siwezi sasa kuhudumu chini ya Oburu. Thamani yangu iko juu. Atafute mtu mwingine,” aliongeza.

Katika hotuba yake, Sifuna alikosoa vikali serikali ya Rais William Ruto, akisema matatizo ya wananchi yanatokana na kushindwa kwa serikali kutekeleza ahadi zake.

“Wakenya wamekataa serikali hii si kwa misingi ya ukabila, bali kwa sababu imeshindwa kutimiza ahadi. Viwanda vya Pwani vimekufa kutokana na uongozi mbovu,” alisema.

Aliahidi kuwa mrengo wa Linda Mwananchi utafufua viwanda vya Pwani ili kuunda nafasi za ajira kwa vijana.

Gavana Orengo naye alielezea hali ya sasa ya kisiasa kama usaliti wa makubaliano ya awali kati ya Rais Ruto na Raila Odinga.

Alidai kuwa makubaliano hayo hayakutekelezwa kama ilivyotarajiwa.

“Makubaliano yaliyotolewa hayakuwa ya kweli. Raila alitaka ajenda vipengele kumi itekelezwe kabla ya ushirikiano wowote, lakini hilo halikufanyika,” alisema.

Orengo alionya kuwa upinzani hautategemea tena mahakama kupinga matokeo ya uchaguzi kama ilivyofanyika hapo awali.

“Mwaka 2027 mjitayarishe. Hatutakubali wizi wa kura. Tutahakikisha mabadiliko yanapatikana kupitia kura,” alisema.

Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino alizungumzia hali ngumu ya maisha inayowakumba wananchi, akisema wengi wanahangaika kupata kipato cha kujikimu.

“Wanawake wanahangaika kutafuta riziki na kurudi nyumbani mikono mitupu. Wazazi hawawezi kulipa karo, na wanafunzi wa vyuo vikuu wanateseka kutokana na ukosefu wa ufadhili,” alisema.

Aidha, alikosoa jinsi Bandari ya Mombasa inavyosimamiwa, akisema haijawanufaisha wakazi wa eneo hilo ipasavyo.

“Bandari ina uwezo wa kuajiri wengi, lakini wakazi hawafaidiki. Ni wangapi hapa mmeajiriwa?” aliuliza.

Seneta wa Kisii Richard Onyonka alisema Linda Mwananchi inalenga kuleta mabadiliko kitaifa na kuboresha uchumi wa nchi.

“Tunataka taifa bora zaidi. Ikiwa Wakenya watapiga kura 2027, uongozi wa sasa utaondoka madarakani,” alisema.

Mbunge wa Suba Kusini Caroli Omondi alidai kuwa baadhi ya viongozi wamesaliti ODM na kujaribu kutumia jina la Raila Odinga kwa manufaa yao binafsi.

“Wapo wanaotaka kutumia urithi wa Raila vibaya. Sisi tunawakilisha maadili halisi ya chama,” alisema.

Aliwahakikishia wakazi wa Pwani kuwa rasilimali za eneo hilo zitatumika kuwanufaisha wenyeji, akiahidi pia kufuta leseni haramu za uchimbaji madini.

Viongozi hao walihimiza wananchi, hasa vijana, kujisajili kama wapiga kura wakisema hiyo ndiyo njia kuu ya kuleta mabadiliko ya kisiasa mwaka 2027.

Walidokeza kuwa baada ya kukamilika kwa kampeni za uhamasishaji kote nchini, mrengo wa Linda Mwananchi utatoa tangazo kubwa la kisiasa litakaloathiri mwelekeo wa siasa za taifa.