Macho kwa Wanga akimteua mrithi wa Magwanga wiki hii
MACHO yote sasa yapo kwa Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga akijiandaa kumteua naibu wake wiki hii baada ya kujiuzulu kwa aliyekuwa naibu wake na mbunge wa zamani wa Kasipul; Oyugi Magwanga.
Bw Magwanga alijiuzulu Februari 26 akisema maafisa wakuu wa kaunti walikuwa wakimhangaisha kwa kufunga afisi yake na kumnyima magari ya kaunti.
Kwa mujibu wa Katiba, naibu gavana akijiuzulu, gavana ana siku 14 kumteua mshikilizi wa nafasi hiyo ambaye lazima apigwe msasa na kuidhinishwa na Bunge la Kaunti.
Kutokana na muda huo wa kikatiba, Bi Wanga ana hadi Machi 12 kumteua naibu wake ambaye atahudumu kwa miezi 17 ambayo imesalia kabla ya uchaguzi wa 2027 kuandaliwa.
Bi Wanga ambaye ni mwenyekiti wa ODM ndiye sasa ataamua iwapo mshikilizi mpya wa afisi hiyo atasalia naibu wake.
Tayari wengi wamejitokeza kumezea mate wadhifa huo ambao unahitaji uaminifu mkubwa kwa gavana.
Waziri wa Fedha wa Kaunti Solomon Obiero, Katibu wa Kaunti Prof Bernard Muok, Spika wa Bunge Polycarp Okombo, Afisa Mkuu kwenye Afisi ya Gavana Isaac Ongiri, Mfanyabiashara Hillary Alila ni kati ya wanaomezea mate nafasi hiyo.
Wengine ni Waziri wa Barabara wa kaunti Danish Onyango na Waziri wa zamani wa Afya Prof Richard Muga.
Inakisiwa kuwa Bi Wanga atamteua mrithi wa Bw Magwanga mnamo Jumatano atakapokuwa akitoa hotuba ya kila mwaka kwa Bunge la Kaunti.
Itabidi Bi Wanga azingatie maeneo yote kabla ya kuamua wa kumpa unaibu gavana.
Maeneo hayo ni Rachuonyo (Kabondo Kasipul, Karachuonyo, Kasipul), Ndhiwa, Suba (Suba Kusini na Suba Kaskazini) na Rangwe (Homa Bay Mjini na Rangwe).
Mnamo 2013, Gavana Cyprian Awiti kutoka Rachuonyo alishinda ugavana na akamteua Hamilton Orata kutoka Ndhiwa kama naibu wake.
Bi Wanga ambaye alikuwa akihudumu kama mbunge mwakilishi wa kike anatoka Rangwe naye Marehemu Seneta Otieno Kajwang’ anatoka Suba.
Marehemu Kajwang’ alipoaga dunia, kiti hicho kiliendea nduguye Moses Kajwang’.
Mnamo 2022, Bi Wanga alimteua Magwanga kutoka Kasipul (Rachuonyo) kama naibu wake na alilazimika kuzingatia usawa wa kieneo kwenye baraza lake la mawaziri.
Wachanganuzi wa masuala ya kisiasa wanasema naibu wa Bi Wanga anastahili kutoka Kasipul.
“Magwanga anatoka huko na baadhi ya wakazi huenda watamuunga 2027. Bi Wanga kwa hivyo, lazima amteue mtu ambaye anafahamu kuwasisimua raia na kupenya ili kupunguza ushawishi wa Bw Magwanga,” akasema Mchangunuzi wa masuala ya kisiasa Fred Omollo.