Siasa

Mkataba kutambua ODM na UDA kama washirika sawa, Wanga afichua

Na MOSES NYAMORI March 24th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MWENYEKITI wa ODM Gladys Wanga amesema kuwa ODM itajadiliana na UDA kama mshirika sawa na watamakinikia kutoingiliwa kwa ngome zao za kisiasa katika uchaguzi mkuu wa 2027.

Bi Wanga alisema muafaka kati yao na UDA utakuwa wa kina na utaangazia sera, masharti, muundo wa serikali kisha watawasilisha stakabadhi hiyo kwa Msajili wa Vyama vya Kisiasa.

“Makubaliano hayo lazima yawe na muundo wa kusuluhisha migogoro inayotokea ndani ya muungano. Pia kutakuwa na jukwaa la kushauriana kuhusu teuzi za mawaziri, bajeti na sheria badala ya majukumu hayo kuwa mikononi mwa chama cha rais,” akasema Bi Wanga kwenye mahojiano na Taifa Leo.

Baadhi ya wanachama wa ODM wamekuwa wakipinga pendekezo la chama kuachiwa ngome zake, wakihofia kuchezewa shere kwenye uteuzi wa chama.

ODM imekuwa na historia ya kutoa tiketi ya moja kwa moja kwa wagombeaji wake kwenye ngome yake pamoja na pia uteuzi ambao huandaliwa mara nyingi huingiliwa na kuvurugwa.

Bi Wanga hata hivyo, anasisitiza kuwa mara hii wanamakinika kuhakikisha wanapata kila kitu sawa na hata kuna kamati ambayo itasikiza na kuamua mizozo inayotokana na utata kuhusu mchujo.

“Kama tumeachiwa ngome zetu nasi lazima tumakinike kuwa sauti ya wananchi inazingatiwa na tutatumia sajili ya chama kuandaa teuzi zetu. Kuachiwa ngome hakufai kutumiwa kiimla na wawaniaji ambao si maarufu kulazimishiwa raia,” akasema Bi Wanga.

Ijumaa hii ODM itakuwa ikiandaa Kongamano la Wajumbe (NDC) na gavana huyo amewapuuza wanasiasa waasi ambao wanapanga kuandaa NDC sambamba.

Hata hivyo, alisema wataheshimu uamuzi wa korti iwapo kesi ambayo imewasilishwa itazima hafla hiyo.

“Wao ndio walikuwa wakitaka NDC wakilenga kutumia kongamano hilo kulipiza kisasi, kupinga uongozi wa chama na uamuzi wake. Waligundua kuwa hawawezi kutimiza baadhi ya matakwa yao pasipo kufuata sheria ya chama,”
“Mwanachama yeyote ambaye hafuati chama basi anapoteza dira na NDC ya mrengo wetu ndio unafuata sheria,” akaongeza.

Bi Wanga anahudumu muhula wa kwanza kama gavana na amekuwa akitajwa kama wale ambao huenda wakawa mgombeaji mwenza wa Rais William Ruto mnamo 2027.

Hata hivyo, alikataa kufunguka kuhusu suala hilo akisema ni chama ndicho kitaamua mshikilizi wa nafasi hiyo iwapo itakuwa sehemu ya makubaliano yao na UDA.