Siasa

Mshtuko baada ya polisi wanaochunguza uvamizi wa Gachagua kuondolewa

Na MWANGI MUIRURI February 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SERIKALI imewaondoa polisi wanaochunguza uvamizi dhidi ya aliyekuwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua mnamo Januari 25 katika Kaunti ya Nyeri.

Bw Gachagua na wandani wake pamoja na waumini walilazimika kuchana mbuga baada ya Kanisa la Kianglikana la Witima eneobunge la Othaya, kuvamiwa.

Wanaume waliovalia kiraia na kujihami wakisindikizwa na magari ya polisi, walirusha vitoza machozi ndani ya kanisa, wakavuruga ibada iliyokuwa ikiendelea na kuharibu magari ya Bw Gachagua na wandani wake.

Licha ya shinikizo kutoka kwa wanasiasa wa upinzani yakiwemo makataa ya Februari 16 baada ya kukutana na Inspekta Jenerali Douglas Kanja, imebainika makachero wa Idara ya Upelelezi (DCI) wameondolewa, na suala hilo kuelekezwa kwa Mamlaka Huru ya Kuchunguza Utendakazi wa Polisi (IPOA).

Kamishina wa Ukanda wa Kati Joshua Nkatha alisema kutokana na kuhusishwa kwa polisi na uvamizi huo, maafisa hao wa usalama hawawezi kujichunguza.

Viongozi wa United Opposition wakifanya mkutano wa kisiasa Othaya baada ya ibada ya Jumapili, Februari 1, 2026. Picha|Gitonga Marete

“Uchunguzi umechukuliwa na IPOA kwa sababu polisi hawawezi kujichunguza,” akasema Bw Nkatha.

Hatua hiyo sasa ina maana kuwa wanasiasa na wahuni ambao huenda walifadhili ghasia hizo wameponyoka na sasa IPOA itaelekeza juhudi zake katika kuwachunguza polisi wanaodaiwa kuhusika.

Majukumu ya IPOA hayajajikita katika kuwachunguza polisi pekee lakini kwa makosa waliyoyatenda wakiwa kazini.

Wakosoaji wanasema hii ni mbinu ya serikali ya kuwakinga wanasiasa ambao huenda walihusika katika kufadhili ghasia hizo.

Upinzani ulikuwa umetaja visa 23 ambavyo Bw Gachagua alivamiwa na kuwataka polisi waliohusika wachukuliwe hatua kali.

Bw Gachagua ameshutumu hatua hiyo akisema serikali haina nia ya kuwachukulia hatua waliomvamia na kuwadhulumu waumini.

“Nina ushahidi kuwa uvamizi huo ulipangwa siku mbili Nairobi kabla ya kutekelezwa. Nimeambiwa mkutano huo ulihudhuriwa na maafisa wawili wa ngazi ya juu wa polisi na wanasiasa watatu waliochaguliwa kutoka Mlima Kenya,” akasema Bw Gachagua.

Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka alisikitika na kushutumu serikali kwa kuacha uchunguzi huo ushughulikiwe na IPOA akisema wahuni waliohusika sasa hawatanyakwa.

“Baya zaidi ni kwamba serikali imeonyesha kuwa imeungana katika kutukuza uhuni ambapo wanasiasa, wahuni, raia wanaoshiriki uhuni na wafadhili wao sasa hawatachukuliwa hatua,” akasema Bw Musyoka.

Kwa mujibu wa wakili Timothy Kariuki, IPOA huwachunguza tu polisi ambao wako kazini wala si wale wanaoshiriki uhalifu wa kiraia.

“Hili ni tukio ambalo sasa linafunikwa kwa sababu serikali imekiri polisi walishiriki uhalifu lakini hakuna uchunguzi ambao utawahusisha wanasiasa na wahuni waliomvamia Bw Gachagua.”