Siasa

Ndoto telezi ya Kenya Kwanza vyama tanzu vikikaidi agizo la Ruto kuvunjwa

Na JUSTUS OCHIENG' April 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 3

NIA ya Rais William Ruto kuunganisha vyama tanzu ndani ya Kenya Kwanza chini ya chama cha UDA imeanza kugonga ukuta.

Licha ya baadhi ya viongozi kutangaza hadharani kuwa vyama vyao vitaunga UDA, wamekwamilia vyama hivyo hata kama havitakuwa na wagombeaji wa viti vya kisiasa katika uchaguzi wa 2027.

Licha ya kuvunjwa na kujiunga na UDA mwaka jana, ANC ya Kinara wa Mawaziri Musalia Mudavadi bado iko hai kisheria.

Hii ni baada ya Mahakama Kuu kufuta kuvunjwa kwa chama hicho na hata chama chenyewe hakijakata rufaa kuhusu uamuzi huo.

Hali hii imeibua maswali kuhusu iwapo ANC ilikuwa kweli na nia ya kuvunjwa au ilikuwa tu hadaa ya kisiasa dhidi ya UDA.

“Baada ya uamuzi wa mahakama, ANC iko hai kisiasa na chama kiko kisheria,” akasema Msajili wa Vyama vya Kisiasa, John Cox Lorionokou.

Mnamo Januari Mahakama ilifuta notisi ya Gazeti la Serikali nambari 3449 ambayo ilikuwa imeidhinisha kuvunjwa kwa ANC.

Korti iliamua kuwa mchakato uliofuatwa haukufuata sheria kwa sababu baadhi ya wanachama hawakushirikishwa.

“ANC inasalia chama ambacho kimesajiliwa na hakijawahi kuvunjwa kisheria,” akasema Jaji Bahati Mwamuye huku akiamuru chama kirejeshewe hadhi na mali yake.

Rais William Ruto, wakati wa kuvunjwa kwa ANC, alikuwa amesema kuwa wao kama Kenya Kwanza, hawawezi kusonga mbele iwapo kutakuwa na vyama vingi tanzu vidogo vidogo.

PAA inayoongozwa na Spika wa Seneti Amason Kingi, imetangaza kuwa haitakuwa na wawaniaji 2027 na itaunga wawaniaji wa UDA.

Chama hicho hata hivyo hakitavunjwa na kitasalia kuwepo kisheria.

Wachanganuzi wa kisiasa wanasema hii ni mbinu ya kusaka hifadhi iwapo mkondo wa siasa utabadilika hasa wakati huu ambapo ushirikiano na ODM umevitungua baadhi ya vyama vidogo ndani ya Kenya Kwanza.

Baadhi ya wabunge kutoka Magharibi wamemwonya Bw Mudavadi kuwa kuvunja ANC kunadhoofisha ushawishi wake ndani ya muungano hasa wakati huu ODM inalenga kudhibiti siasa za eneo hilo.

Ndani ya serikali, duru zinaarifu kuwa hatua ya ANC ya kutokata rufaa kuhusu uamuzi wa Mahakama Kuu ilikuwa na malengo ya kisiasa.

“Inaonyesha wanalenga kusalia na chama chao na wakati huo huo wanajifanya wanaonyesha uaminifu kwa UDA,” akasema afisa wa ngazi ya juu serikalini.

Ford Kenya, chini ya Moses Wetang’ula nayo wiki jana ilisema kuwa haitavunjwa na kusema hiyo ni siasa ya kufumbwa macho na jaribio la kurejesha nchi kwenye uongozi wa chama kimoja.

“Kutaka Ford Kenya ivunjwe ni kuuma mkono uliokulisha hapo awali,” Katibu Mkuu wa Ford-K, John Chikati akaambia Rais Ruto.

Katika eneo la Ukambani, kumekuwa na tofauti kali za kisiasa kati ya Mbunge wa Mwingi Magharibi, Mwengi Mutuse na Waziri wa Leba Alfred Mutua kuhusu iwapo Maendeleo Chapchap itavunjwa au la.

Bw Mutuse ambaye aliwasilisha hoja ya kumtimua aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua, ashawaongoza baadhi ya madiwani wa MCC kujiunga na UDA huku Mutua akichelea kuvunja chama hicho.

“Kwa kusalia na vyama vyao, viongozi hao wanasalia na haki ya kubuni miungano mipya au kuwadhamini wawaniaji kupitia njia nyingine,” akasema mchanganuzi wa masuala ya kisiasa Chris Omore.

Seneta wa Nandi, Samson Cherargei naye amekuwa akionya kuwa vyama ambavyo vimekataa kuvunjwa na kujiunga na UDA vitaachwa nje ya serikali.

“Lazima wavunje vyama hivyo vidogo ili tuwe na chama kimoja kikubwa,” akasema.

Hata hivyo, onyo lake linaonekana kutokuwa na athari na kuibua wazo kuwa wito wa vyama kuvunjwa unaongozwa na udhibiti badala ya umoja.

Wachanganuzi wa masuala ya kisiasa Dismas Mokua na Ishamael Oyoo nao wanasema kuwa chini ya chama kimoja, UDA itawezeshwa kushinda viti vingi.

“Hatua hiyo itamaliza ushindani wa kiti kimoja na vyama tanzu ndani ya muungano. Ushindani huu ndio umezua mgogoro wa ndani na kusababisha viti vitwaliwe na wapinzani,” akasema Bw Mokua.

Naye Bw Oyoo akasema, “Vyama tanzu vinadhoofisha UDA na muungano unastahili ili kuhakikisha wanashinda viti vingi vya ubunge na pia kumaliza uhasama wa ndani kwa ndani wa wabunge kutoka vyama tanzu.”