Ni kutumia na kutema Kenya Kwanza uchaguzi wa 2027 ukikaribia
BAADHI ya waliokuwa washirika wakuu wa Rais William Ruto katika kampeni ya urais ya 2022 wamegeuka kuwa wapinzani wake wakali huku uchaguzi mkuu wa 2027 ukikaribia.
Wengi wa washirika wake waligeuka kuwa wapinzani baada ya kutopata nyadhifa muhimu za serikali, hali iliyochukuliwa kama mfano wa “kutumiwa na kisha kutema.”
Kabla ya uchaguzi wa 2022, baadhi ya watu hao walijitahidi kumpigia debe Dkt Ruto dhidi ya mawimbi ya kisiasa katika maeneo yao.
Pia walipinga Rais wa wakati huo Uhuru Kenyatta kumuunga aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga badala ya naibu wake Ruto.
Lakini mara Kenya Kwanza ilipoingia madarakani, baadhi yao walipoteza nyadhifa zao kutokana na migongano ndani ya utawala, huku wengine wakiwa wahasiriwa wa maandamano ya Gen Z ya Juni 2024 yaliyowatupa kwenye baridi na kugeuka kuwa wakosoaji wakali.
Orodha ya waliobadilika kuwa wapinzani inajumuisha miongoni mwao ni aliyekuwa naibu Rais Rigathi Gachagua, Katibu Mkuu wa zamani wa UDA Cleophas Malala, na Mawaziri wa zamani Justin Muturi (Huduma za Umma), Eliud Owalo (ICT) na Ezekiel Machogu (Elimu).Wengine ni miongoni mwao Boni Khalwale ( kiranja wa Seneti), Naibu kinara wa Kamati ya Bajeti ya Bunge la Kitaifa, Mbunge wa Nyali Mohammed Ali na Seneta wa Laikipia John Kinyua.
Hata hivyo, Rais Ruto na wafuasi wake wanasema waliobadilika kuwa wapinzani ni watu waliotawaliwa na tamaa zao binafsi.
Wanasema baadhi ya watu hao waliharibiwa na matokeo ya matendo yao wenyewe.
“Kazi yangu imekuwa rahisi kwa sababu leo nina msaidizi mkuu anayeelewa masuala ya serikali; anafahamu barabara, umeme, bima ya afya, elimu na hata akiba. Sasa tunagawana kazi, na ninafurahi,” alisema Dkt Ruto alipokuwa akihutubia wagombea wa UDA katika Ikulu Jumatano.
Vincent Kawaya, Katibu wa UDA anayeshughulikia ushirikiano na Mbunge wa Mwala, alisema baadhi ya viongozi waliondoka kwenye serikali kutokana na tamaa zao binafsi.
Alisema mabadiliko hayo ni jambo la kawaida katika siasa yoyote.
“Katika demokrasia yoyote, kuna kuingia na kutoka. Hakuna kitu cha kudumu katika siasa, na kama unaweza kudhibiti zaidi ya asilimia 90 ya timu yako, hiyo inatosha,” alisema.
Aliongeza kuwa baadhi ya watu walijifukuza wenyewe, akirejelea Ndindi Nyoro ambaye alikataa kuunga mkono Rais licha ya kushikilia wadhifa muhimu bungeni kupitia UDA.
“Wapinzani hao wengi hatimaye watarudi. Raila na kundi lake karibu walitutwanga 2022, na sasa wako pamoja nasi,” alisema.
Naibu Gavana wa Kakamega, Ayub Savula, aliyejiunga na UDA kutoka DAP-K, alisema baadhi ya waliotimuliwa kutoka serikali hawakuwa waaminifu kwa Rais. Alisema yuko tayari kuchukua nafasi za Khalwale na Malala kuhakikisha eneo hilo linaunga mkono Rais Ruto.
Mbunge wa Gatanga, Edward Muriu, aliye rafiki wa Gachagua, alidai kuwa wafuasi wengine wa Ruto wataondoka kabla ya uchaguzi ujao, baada ya kubaini Rais ni “mdanganyifu wa kawaida.”
Eliud Owalo, ambaye hivi karibuni amegeuka mkosoaji wa sera za Kenya Kwanza, alikuwa mmoja wa wachache kutoka Luo Nyanza waliounga mkono Rais dhidi ya mawimbi makubwa ya kisiasa.
Aliteuliwa waziri wa ICT hadi Rais Ruto alipovunja Baraza la Mawaziri baada ya maandamano ya Gen Z Juni 2024.
Baada ya kuondolewa, aliteuliwa kama Naibu Mkuu wa Idara ya Utekelezaji na Ufanisi Serikalini akihudumu kutoka Ikulu, hadi Januari 12, 2026 kabla ya kutangaza azma yake ya urais.
Katika Magharibi, Malala na Khalwale walihimili wimbi la Azimio kuunga mkono Ruto.
Dkt Khalwale alishinda kiti cha useneta Kakamega, na Kenya Kwanza ikamchagua kiranja wa wengi, lakini aliondolewa Desemba 2025 baada ya matokeo ya uchaguzi mdogo wa Malava.
Malala alipoteza kiti cha ugavana Kakamega, kisha akajiunga na UDA na kuwa Katibu Mkuu.
Hata hivyo aliondolewa Agosti 2024 na sasa amejiunga na Gachagua kuunda chama cha Democracy for Citizens (DCP) kushindana na Ruto 2027.
Muturi, aliyeungana Dkt Ruto kupitia Democratic Party, alisema anajuta kumpigia debe Ruto.
Aliteuliwa Mwanasheria Mkuu kisha akahamishiwa Wizara ya Huduma za Umma, na hatimaye akafutwa,Mbunge wa Nyali, Mohammed Ali, amegeuka mkosoaji wa serikali huku akishirikiana na Gachagua, akipendekeza siasa zinazojikita kwenye utendaji badala ya heshima kwa wanasiasa wenye nguvu.