Siasa

Oburu asaka upatanishi kuokoa mkutano wa wajumbe, NDC

Na MOSES NYAMORI March 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KIONGOZI wa chama cha ODM, Dkt Oburu Oginga, ameanzisha harakati za upatanishi huku akipambana na jitihada za kuzima Mkutano Mkuu wa Wajumbe wa Kitaifa (NDC) unaopangwa kufanyika Machi 27.

Mkutano huo wa wajumbe unaokusudiwa kuidhinisha maafisa wa muda wa chama – akiwemo Dkt Oginga – sasa umegeuka kuwa mzozo wa kisheria baada ya baadhi ya wanachama kupinga uhalali wake kwa kutumia vipengele vya katiba ya chama hicho.

Kampuni ya mawakili ya Kimani & Muriithi Associates inayomwakilisha mwanachama wa chama hicho Vincent Chepkwony iliandikia uongozi wa ODM Machi 6 ikihoji uhalali wa notisi iliyotangaza mkutano huo pamoja na wajumbe watakaoshiriki.

Kutokana na hilo, chama hicho kupitia Mkurugenzi Mkuu wake Oduor Ong’wen kimemwandikia mlalamishi kikimwalika katika kikao cha upatanishi ili kutatua mzozo huo.

Katika barua aliyoandika Machi 8, Bw Ong’wen alimwalika Bw Chepkwony kuhudhuria mkutano wa mazungumzo unaotarajiwa kufanyika wiki hii.

Wakosoaji wa serikali jumuishi ndani ya ODM wakiongozwa na Katibu Mkuu Edwin Sifuna, Gavana wa Siaya James Orengo, Naibu Kiongozi wa chama Godfrey Osotsi na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino wamekuwa wakidai kuwa Dkt Oginga yuko afisini bila kufuata taratibu za chama.