Raila aendelea kujitenga na raia
KAULI ya kiongozi wa ODM Raila Odinga ya kuunga mkono mikataba tata kati ya serikali na kampuni ya Adani Group yenye asili na usuli wake nchini India inadhihirisha anavyozidi kujitenga na raia ambao alikuwa akiunga mkono na kutetea kwa miaka mingi.
Rais William Ruto alifuta mikataba hiyo baada ya shinikizo kali kutoka kwa raia ambao wamekuwa wakipinga kwa nguvu sera na mipango ya utawala wa Kenya Kwanza.
Katika hotuba yake kwenye kikao cha mawaziri na maafisa wakuu wa serikali kilichofanyika Ijumaa, Bw Odinga alielezea masikitiko yake kwa kufutwa kwa mpango wa kupanua Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA) na Adani Group, mkataba ambao uliibua shutuma kali kutoka kwa wananchi wakihisi ulijaa ufisadi na kupendelea wawekezaji wa kigeni.
“Nilihuzunika sana tuliposhindwa kuendeleza mkataba wa uwanja wa ndege. Adani alipoletwa, siasa ziliingilia na mkataba ukafutwa. Tukikosa kuutekeleza, Nairobi itabaki nyuma,” alisema Raila, akipuuza kabisa hofu kuu ya Wakenya kuhusu uadilifu wa kampuni hiyo na madhara ya kiuchumi kwa wafanyakazi wa ndani.
Hii ni licha ya kampuni hiyo kupatikana na hatia ya kutoa hongo kupata zabuni katika nchi nyingine na kushtakiwa kwa maafisa wake kwa ufisadi.
Kauli ya Raila ilijiri miezi michache tu baada ya maandamano makubwa ya wananchi, hususan vijana wa kizazi cha Gen-Z, waliokuwa wakipinga sera kandamizi kama kodi ya makazi na matumizi mabaya ya fedha za umma.
Raila ambaye hapo awali alionekana kuunga mkono maandamano hayo na ‘kusimama’ na wananchi, sasa anaonekana kubadilika na kusimama upande wa serikali ambayo imekuwa ikikosolewa kwa ukatili, ukiukaji wa haki za binadamu, ufisadi na kupuuza utawala wa sheria.
Katika mkutano wa Ijumaa, Bw Odinga pia aliunga mkono Mpango wa Nyumba za Bei Nafuu ambao raia wengi wameupinga kwa kuwaumiza kwa ushuru, akipongeza serikali kwa juhudi zake, na kusema kuwa ushuru huo ni muhimu kwa maendeleo.
Hii ni tofauti na awali alipokosoa serikal vikali kwa kubebesha raia mzigo wa ushuru.
Hii ilikuwa mara ya kwanza kwa Bw Odinga kuhudhuria kikao rasmi cha serikali tangu vyama hivyo viwili kutia saini Mkataba wa Maelewano (MoU) ulioainisha mipango ya pamoja ya maendeleo.
Katika hotuba yake, alisisitiza umuhimu wa viongozi kufanya yaliyo sahihi kwa taifa, badala ya kutafuta umaarufu wa kisiasa.
“Tumewaona viongozi wakikimbia wajibu wao kwa kutafuta njia rahisi ili wapendwe. Lakini wakati mgumu ndio unaohitaji uongozi wa kweli,” akasema.
Rais Ruto aliunga kauli hiyo na kusema kuwa inalingana na msingi wa utawala wake.
“Wito wake kwa viongozi kufanya lililo sahihi badala ya umaarufu unawiana kikamilifu na maadili ya serikali yetu,” alisema Rais Ruto.Wachanganuzi wanasema hii inaonyesha wazi Raila ameasi raia.
“Kwa muda mrefu, Raila Odinga alijijenga kama mtetezi wa haki za raia, mpinzani mkuu wa serikali dhalimu, na sauti ya wanyonge. Hata hivyo, mtazamo wake mpya wa kuunga sera za utawala wa Kenya Kwanza, ambazo wengi wanazitilia shaka, unaashiria mabadiliko makubwa ya kisiasa ya kujitenga na raia wale ambao alikuwa akitetea na kujiunga na tabaka la watawala ambao alijijenga kwa kukosoa,” asema mchambuzi wa siasa Muli Koli.
Wadadisi wa siasa wanasema kuwa hatua ya Odinga kushirikiana na Rais Ruto haikuwa tu ya kutuliza joto la kisiasa, bali pia ya kujiweka karibu na mamlaka. huku akiachana na maslahi ya wananchi wa kawaida.
Mitazamo ya hivi karibuni kutoka kwa Wakenya mitandaoni inaonyesha hali ya kutoridhika na Raila, wengi wakisema kuwa amegeuka na kujiunga na tabaka la viongozi wanaoweka maslahi yao mbele badala ya watu.
‘Raila alikuwa tumaini letu, sasa anaonekana kujiunga na wale waliotusaliti,’ aliandika mmoja wa wananchi kwenye mtandao wa X (zamani Twitter).
Wengine wanahoji kuwa Odinga hana tena uhalali wa kuzungumza kwa niaba ya upinzani, wala kupokea sifa za mwanamageuzi, ikiwa ataendelea kuunga mkono mikataba na sera ambazo wananchi wamezikataa waziwazi.
“Kwa sasa, ni wazi kuwa Raila Odinga amehamia kambi ya serikali, si kwa maneno tu, bali kwa vitendo. Kwa kuunga mkono mikataba tata kama ile ya Adani, na kupigia debe sera za ushuru, Odinga amejitenga na raia na hasa kizazi cha Gen Z ambacho kinahisi serikali haiwakilisha maslahi yao” asema Koli.