Raundi 2 ya miereka ya UhuRuto yanukia dalili zikionyesha ubabe baina yao unaendelea
KUANZIA Azimio la Umoja One Kenya mnamo 2022 hadi wakati huu ambapo kampeni za Wantam zimeibuka kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027, alama za kisiasa na uwepo wa Rais (mstaafu) Uhuru Kenyatta zinaonekana wazi katika siasa za Kenya.
Ushirikiano wake na marehemu kiongozi wa ODM, Raila Odinga, ushawishi wake kwa kiongozi wa Wiper Patriotic Front, Kalonzo Musyoka hadi akabaki kwenye kambi ya Odinga licha ya kupoteza nafasi ya mgombea mwenza kwa Martha Karua, pamoja na tetesi za uhusiano wake na vuguvugu la Linda Mwananchi kumegeuza uchaguzi ujao wa Kenya kuwa marudio ya ubabe wa Uhuru na Rais Ruto.
Mnamo 2022, Kenyatta alimuunga mkono Raila Odinga, na sasa, kuelekea uchaguzi wa 2027, wachambuzi wa siasa wanasema anajaribu kulinda urithi wake dhidi ya Rais William Ruto.
Huku Katibu Mkuu wa ODM, Edwin Sifuna, ambaye pia ni kiongozi wa Linda Mwananchi, akisema yuko tayari kushirikiana na upinzani kumshinda Ruto, tetesi zinaenea kuwa Kenyatta yupo nyuma ya juhudi hizi.
Wachambuzi wanasema kuwa katika siasa za Kenya, “migongano mara nyingi haishii kwenye kura, bali hubadilika, kusukwa upya na kurudi chini ya bendera mpya.”
Kwa sasa, karibu miaka minne baada ya uchaguzi mkali wa 2022, ushindani kati ya Kenyatta na Ruto unaendelea kuunda mjadala wa kitaifa kupitia muungano mpya wa kisiasa, migongano ndani ya ODM, na kuibuka kwa vuguvugu linaloongozwa na Sifuna.
Hii inaelezwa kama pambano la pili la UhuRuto, ambapo masuala ya kisiasa yanaendelea kuamsha mjadala wa kitaifa na hisia za kisiasa za wananchi.
Mnamo 2022, Kenyatta alichukua hatua isiyo ya kawaida ya kumsaidia Raila Odinga kupitia Azimio la Umoja One Kenya, akivunja ushirikiano wake wa miaka 10 na Dkt Ruto.
Alitumia mashirika ya kisiasa, viongozi wa maoni wa Mlima Kenya na miundo ya Jubilee kurai wapiga kura, huku wabunge wa Jubilee wakipewa mwelekeo wa kisiasa kutojiunga na Ruto.
Miundo ya kampeni ilibadilishwa, na wafuasi wake waliendeleza ujumbe wa “injili ya Azimio” kote Mlima Kenya, akijitahidi kubadilisha mitazamo ya wapiga kura.
Raila Odinga alipotangaza Martha Karua kuwa mgombea mwenza wake, Musyoka alihisi kushushwa heshima na hata kutishia kugombea peke yake, jambo ambalo lingedhoofisha Azimio kwenye kura.
Duru za karibu na viongozi hao zinasema Kenyatta alimuomba binafsi Musyoka kubaki katika kambi ya Odinga.
Wakati huo, Kenyatta alisisitiza kwamba ustawi wa taifa ulihitaji kuendelea bila Dkt Ruto, huku Raila akitaja ushawishi wa Kenyatta kama sababu ya mafanikio yake kupata kura za Mlima Kenya kwa mara ya kwanza.
Hata hivyo, mpango huo haukufaulu kikamilifu. Dkt Ruto alishinda kwa kura 7,176,141 dhidi ya 6,942,930 za Odinga.
Malumbano ya hivi majuzi kati ya Kiongozi wa Wachache Bungeni, Junet Mohamed, na Sifuna, yamechochea mjadala kuhusu ufadhili wa kampeni na madai ya usimamizi mbaya wa fedha zilizotolewa na Kenyatta.
Sifuna alidai hadharani kwamba, fedha hizo, zilizokusudiwa kwa maajenti wa Azimio, zilitoka kwa Kenyatta.
Mohamed alijibu akidai kuwa fedha zilisimamiwa na ndugu wa Kenyatta, Muhoho Kenyatta, kupitia mfumo ambao ulitenga ODM.
Mara baada ya kifo cha Raila, mizozo ya ndani ya ODM haiko tena chini ya mamlaka yake. Katika pengo hili, vuguvugu la Sifuna la Linda Mwananchi limeibuka, likisisitiza ulinzi wa wananchi dhidi ya umasikini na kile anachokitaja kama sera mbaya za Rais Ruto.
Msaidizi wa Rais Ruto, Farouk Kibet, alidai Kenyatta anafadhili siasa za migawanyiko. Viongozi wengine wa Magharibi mwa Kenya pia walisema rais huyo mstaafu anahusika na mzozo wa ODM.
Kenyatta pia amehimiza vijana kushirikiana kisiasa, jambo ambalo wachambuzi wanasema analenga kizazi cha Gen Z kupinga serikali ya Ruto.