Siasa

Ruto sasa achanganya Raila

Na BENSON MATHEKA June 15th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

UCHAGUZI mkuu wa mwaka wa 2027 unavyokaribia, mivutano ya kimkakati inazidi kusukwa huku Rais William Ruto akionekana kugeuza mkondo wa siasa za ngome za Kiongozi wa ODM Raila Odinga kwa kutumia maendeleo kama chombo cha siasa.

Na sasa, Raila anakabiliwa na changamoto ya wazi: kubaki na wafuasi wake au kufanya maamuzi ya kihistoria ya kumuunga Ruto anayetarajiwa kusaka muhula wa pili.

Kwa mujibu wa wachambuzi wa siasa, hali ya sasa imemchanganya Raila ambaye analazimika kujivuta kukosoa serikali inayoendelea kulaumiwa kwa maovu ikiwemo ukatili na ufisadi.

“Raila amefumbwa mdomo kiasi, ana moyo upande wa Ruto lakini akili yake iko na wafuasi wake. Ananufaika na serikali huku akitaka kudumisha wafuasi wake wanaohisi hali sio nzuri,” asema mchanganuzi wa siasa Francis Odhiambo.

Anaongeza kuwa Raila anawaacha wafuasi wake njia panda makusudi ili kuendelea kuwa na udhibiti wa chama cha ODM, na kukitumia kama chombo cha kujadiliana kisiasa mwishoni.

Raila bado hajatangaza rasmi kama atagombea urais kwa mara ya sita. Kimya hiki kimeacha chama cha ODM katika hali ya kutotabirika. Hata hivyo, baadhi ya matamshi kutoka kwa washirika wake wa karibu yanaonyesha dalili kuwa bado hajafunga ukurasa wa kuwania urais. Ruth Odinga, dada yake, alisema hivi karibuni, “Tusubiri neno kutoka kwa Baba. Yeye peke yake ndiye ataamua kama ODM itagombea kama chama. Na hajawahi kusema hatagombea tena.”

Matamshi hayo yalitolewa wakati wa mazishi ya Mama Silvia Lusi, mama mzazi wa Afisa Mkuu wa Afya wa Kisumu, ambapo viongozi wa Nyanza walihudhuria kwa wingi. Katika mazishi hayo, viongozi wengine kama Naibu Gavana wa Kisumu Mathews Owili na Mbunge wa Nyakach Aduma Owuor waliunga mkono kauli hiyo ya Ruth, wakisisitiza kuwa Raila bado ndiye kiongozi wa ODM na uamuzi wake ndio wa mwisho.

Kwa upande wake, kaka mkubwa wa Raila, Seneta wa Siaya Oburu Odinga, amekuwa wazi zaidi kuhusu hofu yao kwa mwenendo wa serikali ya Ruto licha ya juhudi za maendeleo katika eneo la Nyanza. “Ni kweli maendeleo yanafanyika, lakini vitendo vya kutisha kama utekaji nyara, watu kupotezwa na mauaji ya viongozi wetu hayawezi kuvumiliwa. Kama haya yataendelea, basi uhusiano wetu na serikali hii utahitaji kutathminiwa upya,” alisema Oburu katika mkutano wa hadhara.

Dkt Pius Kitema mhadhiri na mchanganuzi wa siasa anasema Raila tayari ameonyesha nia ya kumuunga mkono Ruto hata kama hajatangaza wazi. “Vitendo vyake na lugha ya mwili vinaonyesha kuwa tayari ameamua upande atakaokuwa 2027. Lakini tofauti na zamani, safari hii huenda asifuatwe na wafuasi wake wote. Kuna hali ya mgawanyiko mkubwa ndani ya wafuasi wa ODM na imesababishwa na uhusiano wake na Ruto,” asema Dkt Kitema.

Huku Raila akipoteza wafuasi, Rais Ruto anaendelea kujipenyeza kisiasa na kimaendeleo katika Nyanza. Kwa chini yam waka mmoja, amefanikisha miradi kadhaa ikiwemo ya nyumba za bei nafuu, kuboresha miundombinu ya barabara, kuongeza usambazaji wa umeme na kufufua bandari ya Kisumu. Aidha, hatua ya kujenga Ikulu ndogo ya serikali huko Homa Bay ni ishara ya nia ya kudumu kushirikiana na uongozi wa eneo hilo.

Wakati wa ziara ya hivi karibuni ya Ruto katika Kisumu, Raila alionekana kumkaribisha kwa heshima na hata kupongeza juhudi zake. “Rais anafanya kazi nzuri kwa watu wa Nyanza, hasa katika sekta ya maendeleo ya uchumi.” Kauli hii kutoka kwa Raila iliwashangaza wengi ikizingatiwa alikuwa akieneza injili kwamba maendeleo ni haki ya kila eneo na sio hisani ya rais.

Wachanganuzi wanasema kwamba Rais Ruto amemchanganya Raila hivi kwamba ngome zake hasa Nyanza zinaonekana kuwa kwenye mpito wa uongozi wa kisiasa japo hisia za wakazi zinaonekana kutounga ushirikiano wao.

“Maendeleo kutoka kwa serikali ya Ruto yanaonekana kutikisa misingi ya uaminifu wa kisiasa wa muda mrefu wa wakazi kwa Raila. Raila yuko katika wakati mgumu wa kufanya uamuzi: kubaki na wafuasi wake akidumisha misingi yake ya kutetea haki za raia, demokrasia na utawala wa sheria au kuunga Ruto 2027,” asema Odhiambo.