Safari ya Orengo na uhusiano wake na familia ya Odinga
UAMINIFU wake haujawahi kutiliwa shaka, lakini msimamo wake huru mara nyingi umeibua mijadala.
Gavana wa Siaya James Aggrey Bob Orengo kwa miaka mingi amekuwa akiunga mkono familia ya Odinga kisiasa na wakati mwingine kupinga mwelekeo wake.
Alizaliwa Februari 22, 1951, katika kizazi kilichoshuhudia kuporomoka kwa mfumo wa chama kimoja na kuzuka kwa siasa za vyama vingi.
Akiwa mwanasheria na mtetezi wa haki za binadamu, Bw Orengo alijijengea jina katika siasa za upinzani, huku uhusiano wake na familia ya Odinga ukiwa wa kupanda na kushuka, ushirikiano wa karibu, mgawanyiko mkali, maridhiano ya kisiasa, na tena tofauti za kiitikadi.
Mizizi yake ya kisiasa inahusiana kwa karibu na aliyekuwa Makamu wa Rais wa kwanza Jaramogi Oginga Odinga, ambaye baadaye aligeuka kuwa kinara wa upinzani nchini.
Kupitia chama cha Forum for the Restoration of Democracy (Ford) mwanzoni mwa miaka ya 1990, Bw Orengo alishirikiana na Raila Odinga na viongozi wengine kupinga utawala wa Daniel arap Moi.
Hata hivyo, Ford iligawanyika na kuzua siasa za makundi.
Bw Orengo alibaki Ford–Kenya akiwa mshirika wa karibu wa familia ya Odinga.
Lakini baada ya kifo cha Jaramogi mwaka 1994, swali la nani angechukua uongozi wa kisiasa wa jamii ya Waluo lilizua mvutano.
Katika mzozo wa uongozi kati ya Raila na Michael Kijana Wamalwa, Bw Orengo alimuunga mkono Wamalwa, hatua iliyotafsiriwa na baadhi kama usaliti kwa familia ya Odinga.
Raila aliondoka Ford–Kenya na kuanzisha National Development Party (NDP), huku Bw Orengo akiendelea na Wamalwa.
Katika uchaguzi wa 1997, Raila alipata kura nyingi zaidi kuliko wapinzani wake, akionyesha nguvu zake kisiasa, huku Bw Orengo akihifadhi kiti chake cha Ugenya.
Hata hivyo, mgawanyiko huo uliathiri uhusiano wao binafsi na kisiasa.
Kuelekea uchaguzi wa 2002, Raila aliungana na Mwai Kibaki kupitia muungano wa National Rainbow Coalition (Narc) chini ya kaulimbiu “Kibaki Tosha”.
Bw Orengo, hata hivyo, alisalia nje ya muungano huo na kugombea urais kupitia Social Democratic Party (SDP), lakini akapata kura chache na kupoteza kiti chake cha ubunge.
Kipindi hicho kilimlazimu kutafakari upya mkakati wake wa kisiasa. Kufikia 2005, alirejea katika kambi ya Raila wakati wa kura ya maamuzi ya Katiba, akitoa hata huduma za kisheria bila malipo, hatua iliyorejesha uhusiano wao.
Mwaka 2007, chini ya Orange Democratic Movement (ODM), Bw Orengo alikumbana na ushindani mkali katika kura za mchujo dhidi ya Stephen Mwanga, ambaye alidai kushinda. Hata hivyo, Raila aliingilia kati na kuhakikisha Orengo alipata tiketi, akirejea bungeni.
Baada ya uchaguzi wenye utata wa 2007, Orengo aliteuliwa kuwa Waziri wa Ardhi katika serikali ya muungano kati ya Raila na Kibaki, akapata wadhifa wa kitaifa.
Mwaka 2018, makubaliano ya maridhiano kati ya Raila na Uhuru Kenyatta—maarufu kama ‘Handshake’, yalibadili siasa za taifa.
Awali Orengo alipinga, lakini baadaye aliunga mkono hatua hiyo, jambo lililomwezesha kushinda kiti cha ugavana wa Siaya mwaka 2022.
Hata hivyo, kufikia 2024, alijitokeza tena kama mkosoaji mkali baada ya Raila kujiunga na serikali pana ya William Ruto.
Kifo cha Raila mwaka 2025 kilitikisa siasa za nchi, na uongozi wa ODM ukachukuliwa na Oburu Oginga.
Tofauti mpya ziliibuka huku Orengo akipinga mwelekeo wa chama na uhusiano wake na United Democratic Alliance (UDA).
Wachambuzi wanasema safari ya kisiasa ya Orengo na familia ya Odinga imejaa mchanganyiko wa ushirikiano, ushindani na tofauti za kiitikadi.
Licha ya changamoto hizo, Orengo ameendelea kujitambulisha kwa sifa moja kuu – uthubutu wa kisiasa, hata pale unapomweka kinyume na washirika wake wa karibu.