Serikali inavyojilowesha matope
KENYA imetikiswa na matamshi na matukio ya kusikitisha ya viongozi na maafisa wa serikali hali ambayo baadhi ya wananchi na wachambuzi wa siasa wanasema yanaonyesha serikali imejaa matope.
Hali hii inajitokeza kufuatia misururu ya matukio ya mauaji ya waandamanaji, wakosoaji wa serikali, ukiukaji wa haki za binadamu, utekaji nyara wa kiholela, tuhuma nzito za ufisadi, na ukosefu wa uwajibikaji kutoka kwa baadhi ya viongozi wa serikali ya Kenya Kwanza, inayoongozwa na Rais William Ruto.
Kauli za Waziri wa Usalama wa Ndani, Kipchumba Murkomen, na Naibu Rais Kithure Kindiki zilizoashiria kwamba serikali haitavumilia wanaoikosoa, wakiwemo mabalozi wa nchi za kigeni, zimezua taharuki, zikiwa sehemu ya ushahidi wa pengo kati ya ahadi za utawala bora na hali halisi ya mambo.
Hii ni licha ya kwamba serikali hii ilijisawiri kama ya kuleta mageuzi, ikiahidi vita vikali dhidi ya ufisadi na kukumbatia utawala wa sheria.
Kinyume chake, hali ya sasa inaonyesha serikali inayozama kwenye tuhuma za kumwaga damu kupitia maafisa wa polisi inayounga mkono hadharani licha ya kuua kiholela, ikigubikwa na kashfa baada ya nyingine, ukatili dhidi ya raia, uhusiano wa kidiplomasia wa kushtua na sera zinazofanya raia wakose imani nayo. Ukatili dhidi ya waandamanaji na wimbi la utekaji nyara na mauaji ya watu yanayodaiwa kutekelezwa na maafisa wa usalama au kwa msaada wao, limezua hisia kali miongoni mwa Wakenya. Kwa maafisa wa serikali, ni kawaida.
“Ninawapongeza polisi wetu kwa kufanya kazi nzuri ya kuokoa nchi na ninataka kuwahakikishia kwamba ninawaunga mkono kwa dhati,” alisema Bw Murkomen.
Wanaharakati wa haki za binadamu na viongozi wa makanisa wametoa sauti zao wakilaani matukio haya na kuitaka serikali kuwajibika. Hata hivyo, majibu ya serikali yamekuwa ya kupuuza, viongozi wakipinga hali inayoonekana wazi, huku uchunguzi wa kina ukikosekana.
Matukio ya watu kupotea, au kuokotwa wakiwa wamefariki katika mazingira ya kutatanisha, yameibua taswira ya serikali isiyoheshimu maisha ya raia wake na kusherehekea mauaji ya wakosoaji.
“Serikali imejipaka matope na inaendelea kufanya hivyo, imejichafua kwa raia na jamii ya kimataifa na sasa inatumia taasisi za usalama kama zana ya hofu badala ya ulinzi,” asema mchanganuzi wa masuala ya utawala na kidiplomasia, George Theuri.
Kibaya zaidi, asema Theuri, ni kwamba viongozi wa muungano wa Kenya Kwanza wamekuwa wakitetea maovu ya wenzao badala ya kuhimiza uwajibikaji.
“Ni wazi kuwa serikali hii imezama ndani ya matope ya ufisadi isiyoweza kujisafisha,” asema.
Katika kile kinachotafsiriwa kama hali ya kushindwa kuvumilia tena, mabalozi wa mataifa ya kigeni wameanza kutoa kauli kali dhidi ya mwenendo wa serikali.
Kupitia matamshi yao, wameeleza wasiwasi kuhusu ukiukaji wa haki, kupuuza utawala wa sheria na ufisadi.
Kauli hizi, aeleza Bw Theuri, haziwezi kupuuzwa kirahisi, kwani zinaathiri moja kwa moja uhusiano na uwekezaji wa kimataifa na hadhi ya Kenya katika jukwaa la kimataifa.
“Kuna pia kuhusishwa kwa Kenya katika vita vya ndani vya Sudan, kutambua nchi ambazo hazitambuliwi kimataifa kama Somaliland na kutokuwa na kauli za kukera za viongozi kukosoa mabalozi. Hivi ndivyo serikali inajipaka matope nyumbani na ugenini,” alisema.
Viongozi wa kidini, kwa upande wao, wamekuwa mstari wa mbele kuibua masuala ya mateso ya raia, kupanda kwa gharama ya maisha, na kukosekana kwa mikakati ya kusaidia wanyonge. Lawama zao zinawakilisha sauti ya wananchi waliokata tamaa, wanaohisi kusalitiwa na serikali waliyoichagua kwa matumaini makubwa.
Badala ya kusikiliza ushauri wao, viongozi na maafisa wa serikali wamekuwa wakiwakemea.
“Ninajua hakuna askofu wala kiongozi wa kanisa yeyote, iwe wa Kanisa Katoliki au Anglikana, atakayesimama kutetea polisi. Hakuna atakayezungumzia majeraha ya polisi. Na pia ninajua hakuna mwanadiplomasia atakayekemea hayo. Hii ni kwa sababu hawataki kuona Kenya ikiwa salama,” Murkomen alisema kwa ukali
Kulingana na mchambuzi na mtaalamu wa masuala ya utawala na mchambuzi wa siasa Muli Koli, maafisa hawa wanatetea uchafu wa serikali.
“Badala ya kuwa sauti za utulivu na matumaini, viongozi wameonekana kutetea serikali kwa misingi ya kisiasa badala ya ukweli na maadili. Kauli zao mara nyingi huongeza mpasuko baina ya serikali na wananchi, badala ya kuimarisha mshikamano,” asema.
Anasema matope inayojipaka serikali yanatokana na kiburi, uzembe na ufisadi, serikali inapaswa kujisafisha, viongozi wakumbuke waliyoapa, na kuacha kauli za kuudhi.