Shahbal: Ningekuwa gavana saa hii kama sio Raila na Uhuru kuniwekea presha niachie Nassir
MBUNGE wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Bw Suleiman Shahbal, amefichua matukio yaliyompelekea kujiondoa kwenye kinyang’anyiro cha ugavana Mombasa wakati wa Uchaguzi Mkuu mwaka wa 2022.
Bw Shahbal alisema alishurutishwa kujiondoa kwenye uchaguzi huo na aliyekuwa kiongozi wa chama cha ODM hayati Raila Odinga na aliyekuwa rais, Bw Uhuru Kenyatta.
“Najua kuna wafuasi wangu wengi sana ambao walikasirika sana nilipojiondoa kwenye kinyang’anyiro hicho. Lakini leo nataka niwafahamishe kitu kimoja, kampeni ya mwisho ilikuwa Tononoka na tulikuwa tumewaendesha mbio wapinzani wangu,” alisema Bw Shahbal.
Bw Shahbal ambaye alikuwa akiwania tikiti ya ODM dhidi ya Bw Abdulswamad Nassir ambaye alikuwa mbunge wa Mvita wakati huo, alisema aliitwa Nairobi na viongozi wa chama hicho kuelezewa kuhusu umaarufu wake.
Kulingana naye, aliambiwa umaarufu wake uko asilimia 45 nyuma ya mpinzani wake, Bw Nassir.
Hii ni licha ya kufanya utafiti wake wa kibinafsi ambao ulimuonyesha akiwa asilimia 22 mbele.
“Nikasema hakuna shida twende kwa mchujo. Lakini nikaelezewa mambo mengi sana, nikashikilia msimamo wangu. Nikasisitiza twende kwenye mchujo kama wanaume. Nikaambiwa mchujo utagawanya chama lakini nikasisitiza,” alisema.
Bw Shahbal alisema angelikubali matokeo ya mchujo na kumuunga mkono mshindi.
Alisema ilibidi apasue mbarika kuhusu matukio hayo baada ya kuulizwa maswali na wafuasi wake. Wafuasi wake wameanza kumshawishi kurudi debeni.
“Tukakubali kumleta Bw Odinga kusikiza msimamo wake. Tulikuwa tumekaa sote viongozi wa Mombasa, Baba alikuja akanichukua na kuniingiza kwenye nyumba ya Bw Hassan Joho (Waziri wa Madini na Uchumi Samawati). Akaniambia anataka niende kwa siasa za kitaifa, nichukue uwaziri wa viwanda.”
Hata hivyo, Bw Shahbal alisema alimwambia Bw Odinga kuwa hataki kuwa waziri bali azma yake ni kuwa gavana ili kubadilisha kaunti ya Mombasa.
Alisema alimsihi kiongozi wake wa chama kuheshimu msimamo wake hata hivyo alisema Bw Odinga alikasirika.
Mfanyabiashara huyo alisema Bw Odinga alimwambia kuwa taifa ni kubwa kuliko azma yake.
“Ningesema nini tena baada ya kuambiwa hivyo? Mara simu ikalia akanipatia, ilikuwa ni Rais (mstaafu) Bw Uhuru Kenyatta akinitaka nifuate uwamuzi wa Bw Odinga. Sasa sijui wangapi wamepata kuongea na Rais. Bw Uhuru alikuwa rafiki yangu kabla awe Rais vile vile Dkt William Ruto. Usicheze na urais,” alisema.
Alisema alikuwa kwenye njia panda baada ya kuongea na Rais Kenyatta.
“Ile presha nilipata ni Mungu ndio anafahamu, lakini tuwache yaliyopita tugange yajayo,” alisema.