Siasa za kurukaruka vyama zarejea wanasiasa wakishiriki hamahama haramu
TUKIO la wiki jana ambapo chama cha UDA kilibuni jukwaa la wawaniaji wanaolenga kutumia tiketi yake kuwania viti vya kisiasa katika uchaguzi mkuu wa 2027, limeonyesha wazi jinsi wanasiasa wanavyokiuka sheria zinazoongoza vyama vya kisiasa.
Rais William Ruto alikuwa mwenyeji wa mkutano huo katika Ikulu ya Nairobi ambapo viongozi wanaoshikilia nyadhifa za umma ambao wamezuiwa kujihusisha na kampeni za mapema, walitangaza kuwa wanalenga viti vya kisiasa 2027.
Waziri wa zamani Moses Kuria wa Chama cha Kazi, Naibu Gavana wa Kakamega Ayub Savula wa DAP-K na Mbunge wa Kiminini Bisau Kakai pia wa DAP-K ni kati ya viongozi waliochaguliwa ambao walihudhuria mkutano wa UDA katika Ikulu ya Nairobi.
Wote walionyesha nia yao ya kuwania vyeo mbalimbali kupitia UDA kwenye uchaguzi mkuu ujao.
Bw Kuria alithibitisha kuwa amejiuzulu kutoka Chama cha Kazi na kujiunga na UDA. Alikuwa kiongozi wa chama hicho lakini akajiuzulu baada ya uchaguzi mkuu wa 2022 kujiunga na Baraza la Mawaziri.
Naibu Mwenyekiti wa Tume ya Huduma za Mahakama (JSC) Isaac Rutto na Katibu wa Wizara Shadrack Mwadime pia wamejisajili kama wawaniaji wa UDA.
Bw Rutto analenga kuchaguliwa kuhudumu muhula wa pili kama Gavana wa Bomet huku Bw Mwadime akilenga ugavana wa Taita Taveta.
Aidha, Maseneta John Methu (Nyandarua), Joe Nyutu (Murang’a), Karungo Thang’wa (Kiambu) na James Murango (Kirinyaga) nao wameonekana kuasi UDA waliyochaguliwa kwayo na kujiunga na DCP kinachohusishwa na aliyekuwa naibu wa rais Rigathi Gachagua.
Viongozi wengine waliochaguliwa ambao wanaunga mkono DCP ni wabunge Benjamin Gathiru maarufu kama Mejja Donk (Embakasi ya Kati), James Gakuya (Embakasi Kaskazini), Mohamed Ali (Nyali) na Edward Muriu (Gatanga).
Kanini Kega aliyedhaminiwa na Jubilee kwenye Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA) naye amejiunga na DCP.
Mbunge Maalum wa Jubilee Sabina Chege amekuwa akihudhuria mikutano ya UDA kikiwemo kikao cha Baraza la Uongozi (NGC) kilichoandaliwa mnamo Januari.
Kifungu cha 14 cha Sheria ya Vyama vya Kisiasa kinasema kuwa mtu ambaye ni mwanachama wa chama cha kisiasa, akiunga au kuendeleza ajenda ya chama kingine, basi atachukuliwa kama aliyejiuzulu katika chama chake cha awali.
Aidha, Kifungu cha 12 cha Sheria ya Vyama vya Kisiasa kinasisitiza kuwa afisa wa umma hastahili kushiriki shughuli za kisiasa ambazo zinaonyesha kuwa ana miegemeo au kujitokeza hadharani kuunga au kupinga chama cha kisiasa au mwaniaji katika uchaguzi.
Msajili wa Vyama vya Kisiasa, John Cox alipoulizwa ni kipi taasisi yake inafanya kuzima ‘ukahaba’ wa kisiasa, aliahidi kujibu baada ya muda lakini alipofikiwa tena hakujibu.
Waziri wa zamani Justin Muturi alisema ukiukuaji wa Sheria za Vyama vya Kisiasa umezidi katika utawala huu wa Rais Ruto.
“Ni kinyume cha katiba na pia sheria ya vyama vya kisiasa. Adhabu ni kuwatimua lakini katika Kenya ya Ruto hakuna mtu anafuata sheria,” akasema.
“Kumbuka aliunda UDA wakati ambapo alikuwa Naibu Kiongozi wa Jubilee,” akaongeza.
Wakati wa kikao cha Ikulu, Bw Savula ambaye alichaguliwa kupitia DAP-K alitangaza kuwa atawania ugavana wa Kakamega dhidi ya bosi wake Fernandes Barasa wa ODM.
Mbunge wa Kiminini, Bisau Kakai ambaye pia alichaguliwa kupitia DAP-K pia amejisajili kuwania ugavana wa Trans Nzoia kupitia UDA 2027.
Katibu wa DAP-K, Dkt Eseli Simiyu aliambia Taifa Leo kuwa chama hicho kimeanza mchakato wa kuwatimua wanasiasa hao wawili baada ya tangazo lao kuwa watawania viti kupitia UDA.
Alisema kamati simamizi ya kitaifa pia imetoa pendekezo la kuwatimua waasi hao na Baraza Kuu la Chama linatarajiwa kuidhinisha pendekezo hilo.
“NEC itakutana wiki mbili zijazo kuidhinisha hatua ya kuwatimua katika chama,” akasema Dkt Eseli.
Bw Savula alisema kushiriki shughuli za UDA kunaonyesha kuwa ameanza mchakato wa kujiondoa DAP-Kenya lakini bado hajajiuzulu rasmi.
Wanasiasa waliochaguliwa wamekuwa wakitumia muundo wa sheria ambao unawapa mwanya wa kukata rufaa wakihama chama ili kusalia afisini.
Wapo wanasiasa wengi hapo awali ambao waliwahi kutimuliwa na vyama vyao lakini wakaokolewa na mahakama.