Siasa zatokota Meru Linturi akidai alichangisha Sh100 milioni kutimua Mwangaza
ALIYEKUWA waziri wa Kilimo Mithika Linturi ametangaza kuwa atawania kiti cha ugavana wa Meru na kuibua mjadala kuhusu mchango wake katika harakati zilizomng’oa aliyekuwa Gavana Kawira Mwangaza.
Mnamo Jumapili, Bw Linturi alichemsha kwa kudai kuwa kutimuliwa kwa Bi Mwangaza kulishirikisha matumizi ya pesa.
“Niliongea na marafiki na tukapata zaidi ya Sh100 milioni ambazo tulitumia kumngóa madarakani Bi Mwangaza. Pesa hizo zilipelekwa kwenye Seneti kugharimia mchakato,” akasema Bw Linturi.
“Hatua hiyo ilistahili kwa sababu tulitaka kurejesha Meru katika mkondo mzuri wa uongozi,” akaongeza kwenye mazungumzo na runinga ya Weru.
Hata hivyo, hatua ya Bw Linturi kujitosa katika kinyángányiro hicho pia imemfanya amulikwe kuhusu sakata ya mbolea feki iliyomwandama wakati alipokuwa kwenye wizara ya Kilimo.
Bw Linturi ambaye alikabiliwa na hoja ya kumtimua katika Bunge la Kitaifa, mwishowe aliondolewa lawama na maseneta.
Tangazo lake kuwa atawania ugavana linatarajiwa kuibua joto kali zaidi la kisiasa katika gatuzi hilo.
Hii ni kwa sababu Kinara wa PNU Peter Munya, Kiongozi wa UMP Kawira Mwangaza pia wanalenga kiti hicho ambacho kwa sasa kinashikiliwa na Gavana wa sasa Isaac Mutuma.
Wafanyabiashara Godfrey Mwika na Kinoti Marete pia wametangaza kuwa wanalenga kiti cha ugavana.
Mabw Linturi na Munya walitekeleza jukumu muhimu katika kuondolewa kwa Bi Mwangaza na kufanya Bw Mutuma awe gavana.
Hata hivyo, viongozi hao wawili sasa watamenyana licha ya kwamba wote kwa sasa wapo mrengo wa upinzani.
Bi Mwangazi tayari amesema kuwa analenga kutumia uchaguzi wa 2027 kulipiza kisasi dhidi ya waliombandua mamlakani.
“UMP itawasilisha wawaniaji dhidi ya wanasiasa ambao walinisaliti na nina imani wakazi wa Meru watawatuma nyumbani. Mpango wetu ni kwa Bunge la Kaunti kuwa na idadi ya juu ya wawakilishi,” akasema Bi Mwangaza akifichua mpango wake katika uchaguzi mkuu wa 2027.
Bw Munya na Gavana wa zamani Kiraitu Murungi, pia walikiri hadharani kuwa walikuwa na mkono katika kutimuliwa kwa Bi Mwangaza.
“Uamuzi wa kumtoa uliafikiwa na viongozi waliochaguliwa pamoja na wazee wa Njuri Ncheke na viongozi wa kidini,” Bw Murungi akaambia runinga ya NTV mwaka jana.
Mabw Munya na Linturi tayari wametangaza kuwa hawamuungi Gavana Mutuma lakini Bw Kiraitu na wandani wake wameahidi kumuunga mkuu huyo wa kaunti.
Wandani wa Bw Murungi ambao waliondoka katika chama cha DEP tayari wamejiunga na kile cha TEPA ambacho kinahusishwa na Gavana Mutuma.
“Tulipomsaidia kupata mamlaka tulikuwa na imani angefuata ushauri wetu. Gavana Mutuma haelewi ugatuzi na jukumu lake. Amekuwa akitaja tu miradi ya serikali lakini hawezi kuzungumza jinsi ambavyo mgao wa Sh14 bilioni kwa kaunti ulivyotumika,” akasema Bw Linturi.