Sifuna atangaza mkutano mkubwa wa hadhara saa chache baada ya kutemwa na ODM
KAMATI Kuu ya Kitaifa (NEC) ya chama cha ODM jana ilimtimua Katibu Mkuu wa chama hicho, Seneta Edwin Sifuna, kufuatia kile ilichotaja kuwa kuongezeka kwa viwango vya utovu wa nidhamu ndani ya chama.
Wakati huo huo, asasi hiyo ya juu zaidi imeamua kuitisha Mkutano wa Kitaifa wa Wajumbe (NDC) utakaofanyika Nairobi Machi 27, 2026.
Bw Sifuna, ambaye pia ni Seneta wa Nairobi, hakuhudhuria kikao kilichopitisha kuondolewa kwake katika wadhifa huo kilichofanyika Mombasa.
Katika uamuzi huo, Naibu Katibu Mkuu, Bi Catherine Omanyo, atashikilia wadhifa huo kama kaimu hadi Katibu Mkuu mpya atakapochaguliwa rasmi.
Kupitia taarifa iliyosomwa kwa niaba ya NEC na Bi Omanyo, uongozi wa juu wa chama ulieleza wasiwasi mkubwa kuhusu kuongezeka kwa utovu wa nidhamu, hasa katika ngazi za juu za uongozi.
NEC ilisisitiza kuwa ODM inaongozwa na Katiba yake, misingi ya utawala wa sheria na maamuzi ya pamoja kupitia kamati halali za chama.
“Baada ya kujadili mwenendo wa Katibu Mkuu, Seneta Sifuna, NEC imeamua kumuondoa madarakani mara moja kwa mujibu wa Katiba ya chama na sheria husika. Kwa sasa, Bi Omanyo atashikilia wadhifa huo hadi katibu mkuu mwingine atakapoteuliwa rasmi,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo.
Mapema jana, Kiongozi wa chama, Dkt Oburu Oginga, alionya kuhusu kile alichokiita uasi wa baadhi ya viongozi na wanachama. Alifananisha chama na klabu yenye kanuni zinazopaswa kuheshimiwa.
“Hiki chama ni kama klabu, na lazima ufuate kanuni zake. Hauwezi kuwa mwanachama halafu upinge maamuzi ya klabu. Demokrasia haimaanishi vurugu; lazima kuwe na nidhamu. Katika demokrasia kuna walio wengi na walio wachache, na uamuzi wa wengi hufuatwa,” alisema Dkt Oginga.
Kwa muda sasa, Seneta Sifuna amekuwa mkosoaji mkubwa wa utawala wa Rais William Ruto, licha ya uamuzi wa ODM kujiunga na serikali jumuishi na chama tawala cha UDA.
Sifuna ameonekana kuunga mkono hisia za vijana wanaopinga utawala wa sasa, akiongoza kundi linalojiita “Kenya Moja” linalodai Rais Ruto anapaswa kuhudumu muhula mmoja pekee.
Amekuwa akikosoa sera za kiuchumi za serikali na serikali ilivyoshughulikia maandamano ya vijana na matumizi ya nguvu kupitia polisi.
Licha ya msimamo wa chama chake kushirikiana na serikali, Sifuna amesisitiza kuwa hataunga mkono azma ya Rais Ruto kuwania muhula wa pili, hata kama chama kitaamua kufanya hivyo.
Kutokana na msimamo huo, amekuwa akikabiliwa na shinikizo kutoka kwa baadhi ya viongozi wa ODM kumtaka aunge mkono msimamo wa chama au ajiuzulu.
Baada ya majadiliano ya kina, NEC pia imeamua kuitisha NDC jijini Nairobi Machi 27, 2026.
Mkutano huo utajadili mwelekeo wa kimkakati wa chama, kupitisha maamuzi muhimu ya kamati za chama na kukiandaa kwa Uchaguzi Mkuu ujao.
Aidha, NEC imempa rasmi Kiongozi wa chama mamlaka ya kuongoza mazungumzo kwa niaba ya ODM kuhusu miungano ya kabla ya uchaguzi, kwa kuzingatia misingi ya chama, maslahi ya kimkakati na matarajio ya wanachama.
“NEC imethibitisha tena kujitolea kwa ODM kwa misingi ya demokrasia, utawala wa kikatiba, haki ya kijamii na kuendeleza serikali jumuishi inayoakisi matakwa ya Wakenya,” alisema Bi Omanyo.
Uongozi huo pia ulipokea na kujadili ripoti ya utekelezaji wa Ajenda ya vipengele 10 na kazi ya kamati inayosimamia utekelezaji wa ajenda hizo na mapendekezo ya Kamati ya Mdahalo wa Kitaifa (NADCO).
Kuhusu fidia kwa waathiriwa wa ukiukaji wa haki za binadamu, ODM ilisisitiza dhamira yake ya haki na uwajibikaji, ikiitaka serikali kutenga fedha za kutosha katika bajeti ya ziada ili kufanikisha fidia hiyo kupitia Tume ya Kitaifa ya Haki za Binadamu (KNCHR) kwa uwazi na ufanisi.