UDA watia bidii kunasa kura 1.9 milioni ukanda wa Pwani 2027
JUHUDI za mirengo ya kisiasa kutaka kunasa kura zaidi ya milioni 1.9 za Pwani, zimeshika kasi huku viongozi wa chama cha United Democratic Alliance (UDA) wakiandaa mikutano ya kuwafikia wananchi ili kumpigia debe Rais William Ruto.
Mikutano hiyo, inayoandaliwa kama hamasisho kwa Awamu ya Pili ya Uchaguzi wa Mashinani wa chama uliopangwa kufanyika Aprili 23, imetoa nafasi kwa viongozi wa UDA eneo hilo kueleza mafanikio ya serikali tangu ilipoingia madarakani mwaka wa 2022.
Hii inajiri baada ya viongozi wa mrengo wa Linda Mwananchi kutumia malalamishi ya muda mrefu ya wakazi wa Pwani kujitafutia umaarufu kutoka kwa wananchi wakati wa mkutano wao katika uwanja wa Tononoka mjini Mombasa Jumapili.
Wakiongozwa na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, Seneta wa Siaya James Orengo miongoni mwa wengine, viongozi hao walitaja kufungwa kwa viwanda, umiliki wa ardhi na ukosefu wa ajira kama baadhi ya changamoto zinazoendelea kushuhudiwa Pwani.
Kwa muda mrefu, eneo la Pwani lilikuwa ngome ya kisiasa ya chama cha ODM chini ya aliyekuwa kiongozi wake Raila Odinga.
Chama hicho kimekuwa kikishinda kura nyingi za urais na viti vingi vya kisiasa, huku ngome zake kuu zikiwa Kaunti za Mombasa na Kilifi, ambazo zina idadi kubwa ya wapigakura katika eneo hilo.
Jumatano, viongozi wa UDA walizuru Kaunti ya Lamu, ikiwa ni ya pili katika eneo hilo kutembelewa wiki hii, baada ya mkutano kama huo kufanyika Taita Taveta Jumanne.
Mikutano mingine ilipangiwa Tana River Alhamisi na Kilifi Ijumaa, kisha Kwale Jumamosi kabla ya kuhitimisha Mombasa Jumapili.
Wanasiasa wa UDA wa Pwani wakiongozwa na Waziri wa Michezo, Bw Salim Mvurya, walipuuza kauli za viongozi wa upinzani, wakizitaja kuwa siasa duni na za ukabila.
Bw Mvurya alisema tawala zilizopita, ambazo viongozi wake ni miongoni mwa walioko upinzani, hazikutekeleza miradi ya maana katika eneo la Pwani.
Kulingana naye, Rais Ruto amejumuisha eneo hilo katika ajenda ya maendeleo ya Kenya, akihakikisha halitazamwi tena kama lililotengwa bali kama kichocheo muhimu cha maendeleo ya kitaifa.
“Maeneo ya Pwani ambayo hayakuwa na barabara za lami tangu uhuru kama Lamu Mashariki sasa yanafaidika nazo, yote ni kutokana na Rais Ruto. Tuna nyumba za bei nafuu zinazojengwa Mokowe pamoja na kuunganishwa kwa umeme katika visiwa vya mbali kama Ndau. Tuendelee kuwa pamoja katika kuunga mkono uongozi huu wa mabadiliko wa Rais Ruto,” akasema.
Katibu Mkuu wa UDA, Bw Omar Hassan, alitaja miradi ya mabilioni katika uchumi wa baharini, miundomsingi na umiliki wa ardhi kama ushahidi wa dhamira ya serikali kwa eneo hilo.
Alipuuza wakosoaji na kusisitiza hitaji la umoja wa eneo hilo ili kuepuka kutengwa kisiasa siku zijazo.
“Kama watu wa Pwani, tulibaguliwa katika masuala ya vitambulisho vya kitaifa. Kulikuwa na mauaji mengi ya kiholela yaliyofanywa na tawala zilizopita. Ardhi zetu zilinyakuliwa na hatukuwa na cha kufanya.
“Rais Ruto amehakikisha hayo yote yanakomeshwa. Tusidanganywe tena bali tumchague Ruto anayethamini sisi na eneo letu,” alisema Bw Hassan.
Mbali na kutafuta muhula wa pili kwa Rais Ruto, wanasiasa wa UDA pia wanakabiliwa na changamoto nyingine ya kushindana na ODM kwa nafasi za uongozi katika eneo hilo.
Wachambuzi wa siasa wanasema UDA kitakuwa na nafasi nzuri zaidi ya kupenya katika eneo hilo iwapo itafanikiwa kushirikiana na ODM.
Changamoto ya kushinda viti vya eneo hilo itaongezeka iwapo ODM itasisitiza UDA isiwe na wagombea katika ngome zake.
Iwapo mazungumzo ya muungano kabla ya uchaguzi yatashindikana, “Kubadilisha eneo la Pwani kutoka ngome ya ODM kwenda UDA ni ndoto ambayo haitatimia,” kulingana na Bw Khaldun Vae, mchambuzi wa siasa kutoka Lamu.
Mchambuzi mwingine Emmanuel Wanyoike Kimwa alisema mikutano ya uhamasishaji kuhusu uchaguzi wa msingi ni sehemu ya mikakati ya UDA kupanua ushawishi wake katika ngome za ODM kama vile Pwani ili kuhakikisha ushindi wa viti vya eneo hilo mwaka 2027 huku pia ikihakikisha Rais Ruto anachaguliwa tena.
Bw Jimmy Kahindi, mjumbe wa Bodi ya Kitaifa ya Uchaguzi ya UDA (NEB), alisema uchaguzi wa mashinani wa chama hicho unalenga kuwawezesha wanachama katika ngazi ya chini na kuhakikisha viongozi wanawajibika moja kwa moja kwa wafuasi wa chama.