Uhuru sasa mbioni kufufua Azimio baada ya kifo cha Raila
HATUA ya aliyekuwa Rais Uhuru Kenyatta ya kufufua na kufanya mabadiliko katika uongozi wa muungano wa Azimio La Umoja imezua mwelekeo mpya katika siasa kuelekea uchaguzi wa 2027.
Lengo kuu la mpango huo ni kujenga upinzani ulioungana vyema dhidi ya Rais William Ruto, ambaye alimrithi mwaka 2022.
Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana na Taifa Leo kuhusu kikao kilichotangulia kutangazwa kwa mabadiliko hayo, Uhuru, anayejulikana kuwa na uwezo mkubwa wa kifedha, yuko tayari kufadhili Azimio upya na pia kuwavutia wanasiasa wote wanaompinga Rais Ruto, wakiwemo wale wanaotajwa kama waasi ndani ya ODM.
Aidha, mpango huo unahusisha kuwashirikisha wafanyabiashara wakubwa na wenye uwezo wa kugharamia kampeni za kisiasa.
Uhuru alikuwa mhimili muhimu katika kuundwa kwa Azimio, muungano uliomuunga Raila Odinga katika uchaguzi wa 2022 lakini ukashindwa na UDA ya Ruto.
Baada ya ODM kuingia katika serikali jumuishi, Azimio ilisinzia kisiasa.
Hata hivyo, Taifa Jumapili imebaini kuwa katika mkutano ulioongozwa na Uhuru kwa njia ya mtandao Jumatatu katika kituo cha SKM Command Centre, Karen, viongozi wa Azimio walikubaliana kuanzisha mwelekeo mpya.
Mkutano huo uliamua mabadiliko ya uongozi wa wachache bungeni na kuanza kuwasiliana upya na mitandao ya kisiasa ya marehemu Raila Odinga.
Mkakati unalenga kuhakikisha wafuasi wa Raila wanaendelea kujitambulisha na Azimio katika uchaguzi ujao, huku muungano huo pia ukijadiliana na wahusika wengine wa kisiasa kama aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua wa chama cha DCP, ili kupanua uungwaji mkono.
Inasemekana Uhuru analenga kuhakikisha upinzani utakuwa na mgombea mmoja wa urais pekee, ili kuepuka makosa ya kihistoria ya uchaguzi wa 1992 ambapo upinzani uliwasilisha wagombea wengi na kumpa Rais Daniel Moi ushindi.
Katika mkutano huo, Kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka aliteuliwa kuwa kiongozi wa Azimio( soma makala ukurasa 5), akichukua nafasi ya marehemu Raila Odinga. Hatua hii inalenga kuimarisha nafasi ya Kalonzo kisiasa na kuongeza msukumo wa kampeni ya “Ruto Wantam” ( Ruto muhula mmoja)”.
Cha kushangaza, Rigathi Gachagua ambaye awali alionekana kama angepinga mkondo huu mpya – aliupongeza uamuzi huo. Kupitia chama chake cha DCP, alisema uteuzi wa Kalonzo ni hatua sahihi kuelekea “kuzaliwa upya kwa taifa” mwaka 2027.
Wakosoaji, hata hivyo, wanaonyesha wasiwasi wakisema miungano ya kisiasa nchini Kenya mara nyingi hudumu kwa muhula mmoja pekee wa uchaguzi. Wanahoji kama Azimio inaweza kufufuliwa kwa ufanisi baada ya kudhoofika.
Mkutano huo pia uliamua mabadiliko ya nyadhifa muhimu ndani ya muungano. Mbunge wa Suba Kusini Caroli Omondi aliteuliwa Katibu Mkuu mpya wa Azimio, huku aliyekuwa Waziri Raphael Tuju akiondolewa kama Mkurugenzi Mtendaji na nafasi yake kuchukuliwa na aliyekuwa Karani wa Jiji la Nairobi Philip Kisia.
Msemaji wa Uhuru, Kanze Dena, alisema Rais mstaafu alitekeleza jukumu lake kama mwenyekiti wa baraza la muungano, na kwamba Kalonzo sasa atasimamia shughuli zote za Azimio ikiwemo maandalizi ya uchaguzi.
Bw Omondi alisisitiza kuwa mkutano huo ulifanyika baada ya mashauriano mapana yaliyohusisha familia ya Odinga na washirika wake wa kisiasa. Alisema lengo ni kulinda urithi wa Raila na kuunganisha upinzani ili kumshinda Ruto.
Katika mkakati mpana, Azimio inapanga kujivunia sura mpya itakayowavutia vijana wa Gen Z na washirika wapya wa kisiasa. Pia kuna mipango ya kufungua milango kwa wanachama binafsi au vyama vilivyojiondoa awali, kama vile PLP ya Martha Karua na DAP-K ya Eugene Wamalwa.
Kwa jumla, mpango wa Uhuru unaonekana kuwa jaribio la kuunganisha upinzani uliosambaratika na kuupa mwelekeo mmoja.
Swali kubwa linalosalia ni iwapo upinzani utakubaliana chini ya Azimio na kumkubali Kalonzo kama mgombea mmoja wa urais, au kama mgawanyiko utaendelea na kumpa Rais Ruto nafasi ya kunufaika.