Siasa

Upinzani sasa wapanga kuvamia ngome ya Ruto baada ya ‘mapokezi mema’ Bomet

Na RUTH MBULA February 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

VINARA wa Muungano wa Upinzani walihitimisha ziara ya siku tatu katika eneo la Gusii jana, wakiapa kuendelea kushirikiana katika jitihada zao za kumshinda Rais William Ruto katika Uchaguzi Mkuu wa Mwaka wa 2027.

Viongozi hao walisema kuwa watalazimika kuweka kando tofauti za kisiasa kwani ni upinzani ulioungana pekee na wenye nidhamu tu utakaoweza kushinda serikali ya sasa.

Muungano huo umeapa kuunganisha wafuasi wao chini ya mgombea urais wa pamoja huku wakisema wanapanga kuvamia ngome ya Rais Ruto ya Bonde la Ufa.

Viongozi wa muungano huo walihutubia maelfu ya wakazi katika miji ya Ogembo, Kenyenya, Nyamache na Masimba, Kaunti ya Kisii na kufichua kuwa tayari wameanza kuzungumza na wanasiasa wa Bonde la Ufa, ngome ya kisiasa ya Rais Ruto, na wanapanga kupiga kambi huko hivi karibuni ili kupanua msingi wa wafuasi wao katika juhudi za kumng’oa Rais madarakani.

Mgombea urais wa chama cha Jubilee, Dkt Fred Matiang’i, Kiongozi wa DCP Rigathi Gachagua, Kalonzo Musyoka wa Wiper Patriotic Front, Martha Karua wa People’s Liberation Party, Eugene Wamalwa wa Democratic Action Party of Kenya na Peter Munya wa Party of National Unity, waliandamana na wabunge na maseneta kadhaa kutoka kote nchini.

Viongozi hao waliwahimiza wakazi wa Gusii kumuunga mkono Dkt Matiang’i aliyeidhinishwa kuwa msemaji wa jamii hiyo Jumatatu iliyopita.

Walisema kuwa malengo ya kitaifa lazima yaanze na msingi thabiti nyumbani.

Muungano huo ulitoa wito kwa wakazi kupinga viongozi wa eneo hilo ambao hawamuungi mkono Dkt Matiang’i.

Bw Gachagua alisisitiza kuwa yeyote anayejaribu kuzungumza na jamii ya Gusii lazima afanye hivyo kupitia Dkt Matiang’i.

Alilalamika pia kuhusu baadhi ya viongozi waliochaguliwa kutoka eneo hilo waliodaiwa kujaribu kudhoofisha ushawishi wa naibu kiongozi huyo wa Jubilee.

“Hakuna kitu kinachotuunganisha zaidi kuliko lengo letu la kumuondoa Dkt Ruto mamlakani. Amefika hapa mara nyingi na amewaongoza vibaya wananchi. Wakati wa kupima rekodi ya viongozi, tutamtathmini kwa rekodi yake, lakini amebobea katika udanganyifu wa kisiasa. Kwa hivyo, nawahimiza Abagusii kuungana nyuma ya Dkt Matiang’i,” alisema Gachagua.

Bw Kalonzo Musyoka aliwataka viongozi wa Gusii wanaounga Rais Ruto kubadilisha msimamo na kumuunga Dkt Matiang’i, akionya kwamba kushindwa kusoma hali ya kisiasa kutawafanya wakataliwe na wapigakura mwaka wa 2027.

Kwa upande wake, Bi Karua alisema kuwa muungano huo utapinga aina yoyote ya udikteta na kuhakikisha sheria inaheshimiwa.

“Hatutaruhusu viongozi katika Afrika Mashariki kuendeleza utawala mbaya au kukwamilia madarakani. Sheria lazima itumike,” alisema.

Kalonzo alisema muungano wa upinzani haukubali udanganyifu katika kupiga kura na una lengo la kurekebisha sera za Rais Ruto ambazo zimesababisha shida kwa wananchi.

Kikundi kimeahidi kushirikiana kuhakikisha haki, kupambana na ufisadi na kuhimiza uwajibikaji wa viongozi.