Siasa

Utamu wa mamlaka: Vigogo wa miaka mingi waunga 12,000 wanaomezea tiketi UDA

Na MOSES NYAMORI February 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

ZAIDI ya wanasiasa 12,000 wakiwemo vigogo walioshindwa katika uchaguzi wa 2022 na wengine wanaohudumu sasa lakini wanalenga nyadhifa za juu, wamejitokeza kuwania tiketi za chama tawala cha United Democratic Alliance (UDA), hali inayoongeza presha kwa viongozi walio madarakani.

Takwimu za chama hicho zinaonyesha kuwa jumla ya watu 149 wamewasilisha maombi ya kugombea nyadhifa 47 za ugavana, huku wengine 279 wakitaka kuwania nafasi 47 za useneta.

Katika kinyang’anyiro cha Mwakilishi wa Kike, wawaniaji ni 323, huku maeneo bunge 290 yakivutia wawaniaji 1,372. Idadi kubwa zaidi ya watu 10,230 imejitokeza kuwania tiketi ya chama katika wadi 1,450 kote nchini.

Kwa jumla, waombaji ni 12,353.

UDA imeunda tovuti ya UDA Aspirants Forum na kuwaagiza wanaotaka kuwania tiketi ya chama katika Uchaguzi Mkuu wa 2027 wajisajili kabla ya mkutano unaopangwa kufanyika Ikulu leo (Jumatano) ukiongozwa na Rais William Ruto.

Awali, usajili huo ulionekana kama mkutano wa kawaida wa kisiasa, lakini sasa umechochea rasmi mbio za 2027 huku watu wakitangaza azma za nyadhifa mbalimbali.

Miongoni mwa majina makubwa yanayowania ugavana ni Evans Kidero (Nairobi), Isaac Ruto (Bomet) na Mbunge wa Tinderet Julius Melly (Nandi), aliyekuwa gavana Cleophas Lagat (Nandi), Mbunge wa Kimilili Didmus Barasa (Bungoma), aliyekuwa Waziri Peninah Malonza (Kitui), aliyekuwa gavana Granton Samboja (Taita Taveta) na Mbunge wa Thika Town Alice Ng’ang’a (Kiambu).

Wengine ni aliyekuwa Mbunge wa Rarieda Nicolas Gumbo (Siaya), Naibu Gavana wa Kakamega Ayub Savula, Mbunge wa Pokot Kusini David Pkosing, Mbunge wa Maara Kareke Mbiuki na Mbunge wa Tharaka George Murugara (Tharaka-Nithi).

Aliyekuwa Waziri wa Utumishi wa Umma Moses Kuria pia ameomba kuwania ubunge Gatundu Kusini, kiti alichowahi kushikilia.

Zoezi la usajili pia limepatia UDA fedha taslimu kupitia ada za usajili.

Kulingana na tangazo la Mwenyekiti wa Bodi ya Uchaguzi ya Kitaifa ya UDA, Anthony Mwaura, la Januari 21, wanaowania udiwani (MCA) wanatakiwa kulipa Sh2,000 kuhudhuria mkutano wa Ikulu; wanaotaka ubunge, uwakilishi wa kike na useneta wanalipa Sh5,000; wagombea ugavana Sh10,000; na wanaotaka kumpinga Rais Ruto kwa tiketi ya urais wa chama Sh100,000.

Kwa mujibu wa takwimu, chama kimekusanya Sh20,460,000 kutoka kwa wanaowania udiwani, Sh1,490,000 na Sh9,870,000 kutoka kwa wabunge (Maseneta, Wawakilishi wa Kike na Wabunge wa Kitaifa). Kwa jumla, zoezi hilo limeingizia chama Sh31,820,000.

Nairobi, Gavana Johnson Sakaja atakutana na wapinzani wanane kuwania tiketi ya chama, wakiwemo Naibu wake James Njoroge Muchiri na Dkt Kidero.

Dkt Kidero alikuwa gavana wa kwanza wa Nairobi kabla ya kushindwa na Mike Sonko mwaka 2017, na baadaye akagombea Homa Bay 2022 bila mafanikio.

Wengine ni Lucheri Milton, Mark Ng’ang’a, Wilfred Nyaera, Kendrick Orony, Stephen Otieno na Patrick Musili.

Katika kaunti ya Baringo, aliyekuwa gavana Stanley Kiptis amerejea UDA baada ya kugombea kama mgombea huru 2022. Gavana Benjamin Cheboi anahudumu muhula wa mwisho. Jumla ya watu 16 wanawania ugavana; useneta (6), Mwakilishi wa Wanawake (30), ubunge (84) na udiwani (479).

Katika kaunti ya Bomet, Makamu Mwenyekiti wa Tume ya Huduma za Mahakama (JSC) Isaac Ruto ameacha Chama Cha Kazi na kuomba kuwania ugavana kwa tiketi ya UDA. Ugavana umevutia waombaji watatu; useneta (9), Mwakilishi wa Wanawake (17), ubunge (55) na udiwani (366).

Huku Bungoma, Mbunge Didmus Barasa anataka kumrithi Gavana Ken Lusaka aliye katika muhula wa mwisho. Wengine ni Jenepher Chemtai, Dennis Nyongesa na Sophy Waliaula.

Useneta na Mwakilishi wa Wanawake vina waombaji watano kila kimoja; ubunge (42) na udiwani (263).

Kaunti ya Busia haina mgombea wa ugavana anayesaka tiketi ya UDA, lakini ina 8 wa useneta, Mwakilishi wa Wanawake (13), ubunge (27) na udiwani (213).

Kaunti nyingine zinaonyesha mwelekeo mseto: Embu haina mpinzani wa UDA dhidi ya Gavana Cecily Mbarire; Garissa aliyekuwa gavana Ali Korane ndiye pekee kwa sasa; Homa Bay ina waombaji watatu wa ugavana; Isiolo wawili; Kajiado mmoja; Kakamega watatu; Kericho 13; Kiambu watatu; Kilifi mmoja; Kirinyaga mmoja; Kisii mmoja; Kisumu hakuna; Kitui watatu; Kwale wawili; Laikipia hakuna; Lamu wawili; Machakos hakuna; Makueni wawili; Mandera sita; Marsabit watatu; Meru mmoja; Migori wanne; Mombasa watatu; Murang’a hakuna; Nakuru watatu; Nandi kumi; Narok wanne; Nyamira wawili; Nyandarua hakuna; Nyeri mmoja; Samburu mmoja; Siaya wawili; Taita Taveta wawili; Tharaka-Nithi wawili; Trans Nzoia wanne; Turkana mmoja; Uasin Gishu watano; Vihiga mmoja; Wajir wanne; na West Pokot watatu.